1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Makampuni ya kuhudumia wazee yakumbwa na kashfa Ujerumani

Sylvia Mwehozi
31 Mei 2017

Polisi wa Ujerumani wanasema baadhi ya waendeshaji 230 wa nyumba za kuwahudumia wazee wanadhaniwa kuwa waliunda utaratibu wa mtandao wa udanganyifu ambao unahusishwa na Mafia.

https://p.dw.com/p/2dw6i
Deutschland Behinderter kümmert sich um Demenzkranke
Picha: picture-alliance/dpa

Madai hayo yamekuja baada ya ripoti ya ofisi ya shirikisho ya makosa ya jinai ya polisi BKA na jimbo la North Rhine-westphalia kuonyesha kwamba makampuni yapatayo 230 yako chini ya uchunguzi kwa udanganyifu.

Kwa mujibu wa ripoti iliyovujiswa kwa gazeti la Die Welt na kituo cha utangazaji cha Bavaria, makampuni hayo mara kwa mara yanadanganya kuhusu watoaji wa bima ya afya, wagonjwa na maduka ya dawa kwa madai ya huduma ambazo hawazitoi, kughusi nyaraka, kuajiri watoa huduma wasio na vigezo na kutoa madai mengi kwa mgonjwa mmoja.

Wacheza kamari na wauaji wa mikataba

Pamoja na baadhi ya makampuni, polisi wanashuku kuna mtandao na uhalifu wa kupangwa kutoka Urusi au Eurasia, kutokana na kutia shaka kwa fedha chafu, uwepo wa makampuni ya shell ndani na nje ya nchi pamoja na kuhusishwa na mitandao ya kamari.

Si hivyo tu, ripoti iliyovuja imebaini kwamba baadhi ya wakuu wa zamani wa makampuni walio chini ya uchunguzi walikuwa tayari wanajulikana na polisi kama watuhumiwa wa mauaji ya mikataba.

Karl-Josef Laumann, CDU
Karl-Josef Laumann kamishina wa wagonjwa wa serikaliPicha: picture-alliance/dpa/C. Seidel

Wakati wa mkutano wa ndani wiki iliyopita kati ya polisi, waendesha mashitaka na wawakilishi wa makampuni ya bima za afya, wachunguzi maalumu walisema kwamba wanaamini huduma ya kuwahudumia wazee ilikuwa ndio mlengwa wa udanganyifu kwasababu inatoa faida kubwa dhidi ya hatari ndogo . Si hivyo tu, ikizingatiwa idadi ya wajerumani inazidi kuwa wazee, fursa hizo zingeongezeka katika siku za usoni.

Wawakilishi kadhaa wa haki za wagonjwa walitangaza hasira zao dhidi ya ripoti hiyo. "Nikisia kitu kama hicho, napata hasira kwasababu udanganyifu katika sekta ya kuwahudumia wazee ni kitu cha kushutua", alisema kamishina wa wagonjwa wa serikali, Karl-Josef Laumann wakati akizungumza na SWR2.

Lakini Eugen Brysch mkuu wa taasisi ya ulinzi wa wagonjwa ya Ujerumani DSP, alionyesha zaidi ya hasira akidai kwamba mamlaka za serikali zimekuwa rahisi kwa uhalifu huo wa kupangwa hadi kufikia hivi sasa. Katika taarifa yake, Brysch anabainisha mfululizo wa mapungufu katika utekelezaji wa sheria na udhibiti uliopangwa wa kuyadaka madai ya uongo.

"Kunakosekana umakini kwa waendesha mashitaka na makundi ya wachunguzi maalumu", anasema Brysch. "Hapa ndio tunahitajika maelezo zaidi kutoka kwa mawaziri wa mambo ya ndani na wale wa sheria.  Lakini pia ni wajibu wa wataalamu wa tiba wa makampuni ya bima. Wakati madai ya mtuhumiwa yasipotazamwa, haishangazi kwamba mtu mmoja anapokea huduma chini ya majina mbalimbali."

Suluhisho tayari limepatikana

Tatizo hilo sio jipya. Udanganyifu huo mkubwa uliwahi kubainishwa muda kama huu mwaka jana, wakati serikali ya Ujerumani ilipoanzisha sheria zinazoruhusu makampuni ya bima ya afya kufanya uchunguzi mwingine.

Eugen Brysch, Vorsitzender Deutsche Stiftung Patientenschutz
Eugen Brysch mkuu wa taasisi ya kuwalinda wagonjwaPicha: Deutsche Stiftung Patientenschutz

Lakini DS, ambayo inasema inadhaminiwa na wahisani, mara zote imesema serikali inaweza kwenda mbali zaidi na siku ya Jumanne ilieleza mapendekezo kadhaa katika mpango uliobuniwa mwaka mmoja uliopita, ikiwa ni pamoja na kuwepo na mfumo wa taarifa ambao unahifadhi huduma zote zinazotolewa na kitambulisho cha maisha cha aina moja kwa wagonjwa wote.

Juu ya hilo DSP inadai kwamba wahalifu wanatumia mwanya wa kwamba waendesha mashitaka katika baadhi ya majimbo ya Ujerumani wanalishughulikia tatizo hilo tofauti kwasababu ni baadhi tu ya majimbo ambayo yamelipa uzito suala la kupambana na udanganyifu. Msemaji wa wizara ya sheria ya Ujerumani aliithibitishia DW kwamba majimbo yanayo haki ya kuamua ni uhalifu gani waufatilie.

Lakini Bernd Tews, mkuu wa taasisi binafsi ya watoa huduma ya ustawi wa jamii BPA, alikuwa na matumaini katika barua pepe aliyoituma kwa DW akisema tatizo halikuwa kwa wingi ikizingatia kwamba ni makampuni 230 kati ya 14,000 anbayo yako chini ya uchunguzi.

Si hivyo tu, ripoti mpya inaonyesha kwamba mfumo wa sasa ulikuwa na ufanisi." Kesi hizo za udanganyifu ambazo zinatakiwa kuchukuliwa hatua za kisheria, zilifichuliwa chini ya mfumo mzuri unaofanya kazi na zinafuatiliwa kisheria", alisema Tews.

Mwandishi: Sylvia Mwehozi/DW

Mhariri: Saumu Yusuf