1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Makubaliano ya biashara huria yanazilazimisha nchi masikini kuwa masikini zaidi.

Sekione Kitojo21 Machi 2007

Makubaliano mapya ya biashara huria yanayotiwa saini baina ya mataifa tajiri na masikini yanaonyesha hali ya uharibifu mkubwa kwa mataifa hayo masikini kuliko kitu chochote kinachofikiriwa katika mazungumzo ya shirika la biashara la dunia WTO, linasema shirika la kutoa misaada la Oxfam katika ripoti iliyotolewa Jumanne.

https://p.dw.com/p/CHHr

Mataifa masikini yanalazimishwa kupunguza ushuru wake wa forodha , Emily Jones , mwandishi wa ripoti ya shirika hilo la Oxfam, inayojulikana kama , utiaji saini unaopoteza maisha ya baadaye, ameliambia shirika la habari la IPS.

Ushuru mara nyingi unapunguzwa hadi kufikia sifuri chini ya makubaliano ya pamoja yanayoitwa makubaliano ya biashara huru ambayo wanalazimika kutia saini na mataifa tajiri.

Hii ina maana mataifa masikini yanalazimika kufungua masoko yake kwa ajili ya bidhaa za kilimo zinazopatiwa ruzuku kutoka maeneo kama umoja wa Ulaya , amesema.

Tayari kuna zaidi ya makubaliano 250 ya kimkoa na makubaliano ya pamoja na mengine bado yanaendelea kujadiliwa, ripoti hiyo inasema.

Makubaliano ya kimkoa na ya pamoja hivi sasa yanaongoza zaidi ya asilimia 30 ya biashara duniani, na mataifa 25 yanayoendelea hivi sasa yametia saini makubaliano ya biashara huru na mataifa yaliyoendelea.

Wastani wa makubaliano ya uwekezaji wa pamoja yanatiwa saini kila wiki , ripoti hiyo imesema.

Hakuna nchi ambayo , hata kama ni masikini kiasi gani ambayo imeachwa.

Makubaliano hayo , kwa mujibu wa ripoti hiyo yanaharibu hatua za maendeleo.

Katika dunia ambayo inaendelea kukumbatia utandawazi, makubaliano haya yanataka kuwafaidia wauzaji nchi za nje kutoka mataifa tajiri na makampuni kwa kuwakandamiza wakulima masikini pamoja na wafanyakazi, na kuleta maafa makubwa kwa mazingira na maendeleo, ripoti hiyo imesema.

Marekani na umoja wa Ulaya zinapitisha sheria kuhusu haki miliki ya mali za kitaalamu, hali inayopunguza uwezo wa watu masikini kuweza kupata dawa za kuokoa maisha , kuongeza bei ya mbegu na pembejeo nyingine za kilimo ambazo wakulima wadogo hawawezi kuzipata, na kufanya kuwa vigumu kwa makampuni ya nchi zinazoendelea kuweza kupata teknolojia mpya, ripoti hiyo imesema.

Serikali katika baadhi ya nyakati zinaonyesha kuwa hazina nguvu dhidi ya hatua hizo.

Baadhi ya mataifa ya dunia ya tatu yanajikuta baina ya jiwe na sehemu ngumu, amesema Jones. Mataifa mengi yanatia saini kile kinachojulikana kama makubaliano ya kiuchumi ya ushirikiano kwa woga wa kupoteza upendeleo fulani, Jones amesema. Mengi ya mataifa haya yamepewa upendeleo katika uuzaji wa bidhaa zake katika mataifa hayo, ili yaweze kupunguza ushuru wa forodha kwa bidhaa zitokazo kutoka katika mataifa hayo yanayoendelea.

Makubaliano ya biashara huru ya Amerika ya kaskazini NAFTA, yameleta upotevu wa nafasi milioni 1.3 za kazi nchini Mexico katika muda wa miaka kumi, anasema Jones. Mauzo zaidi kwa Marekani yameshindikana kuleta ukuaji, na baadhi ya uchunguzi unaonyesha kuwa mishahara halisi katika mwaka 2004 ilikuwa chini kuliko mwaka 1994, Jones anadokeza.

Sheria katika ubinafsishaji wa huduma katika makubaliano ya aina hiyo yanatishia kuyaondoa makampuni ya mataifa masikini kutoka katika biashara, kupunguza ushindani, na kuongeza uwezo wa ukiritimba wa makampuni makubwa, ripoti hiyo imesema.

Serikali katika mataifa yanayoendelea kwa kawaida yanakuwa katika mbinyo mkali kisiasa ili kutia saini makubaliano ya aina hii, Simon Ticehurst kutoka Oxfam nchini Bolivia ameliambia shirika la habari la IPS. Lakini pia inategemea sana juu ya aina ya mfumo wa maendeleo ambao serikali zinaupeleka kwa wananchi wake. Colombia na Peru zimetia saini makubaliano haya. Wengine wanasita. Nchi ndogo kama Bolivia na serikali nyingi mpya katika Latin Amerika zinaanza kupinga mantiki ya biashara huria.