1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Malaria yaendelea kutishia maisha Tanzania

6 Mei 2011

Huko Rungwe, Kusini Magharibi mwa Mbeya, Tanzania, malaria inachukua kwa haraka mahala pa maradhi ya kikohozi homa ya mapafu kama kama tatizo kubwa zaidi la kiafya katika eneo hilo.

https://p.dw.com/p/11AzL
Mbu anayesababisha malaria
Mbu anayesababisha malariaPicha: picture-alliance /dpa

Hali hiyo imewashangaza zaidi wakaazi wa eneo hilo ambao mbali kabisa na maeneo ya kawaida yanayosumbuliwa na Malaria nchini Tanzania.

Katika mwaka wa 2009, vituo vya afya katika wilaya ya Rungwe vilisajili visa vya Malaria 100 ambalo ni ongezeko la asilimia 25 kutoka mnwaka wa 2006.

Malaria ni tishio kubwa kwa sasa linaloikabili wilaya ya Rungwe ambayo inapatikana kusini Magharibi mwa mji mkuu Dar es salaam kwa mujibu wa kituo cha utafiti wa matibabu cha Tukuyu ambacho ni sehemu ya taasisi ya kitaifa ya utafiti wa matibabu.

Theluthi ya wagonjwa walioitembelea hospitali hiyo mnamo mwaka wa 2007 waligunduliwa kuwa na Malaria yanayoambukizwa na mbu.

Maeneo mengi ya nyanda za juu nchini Tanzania yanakabiliwa na mzigo mkubwa wa ongezeko la visa vya Malaria ambapo mratibu wa masuala ya Malaria katika wilaya ya Rungwe Gideon Ndawala anasema vinachangiwa na mabadiliko ya tabia nchi hasa uharibifu wa mazingira.

Ndawala anasema nyuzi joto zimepanda katika eneo hilo katika miaka ya hivi karibuni kuliko jinsi ilivyokuwa awali ambapo eneo hilo lilikuwa baridi na lenye unyevu. Anasema hali hiyo inawapa mbu mazingira mazuri ya kuzaana kwa wingi. Wilaya zinazokabiliwa na hali hiyo ni Tukuyu, Ikuti, Rungwe, Mission na Ilolo.

Mkaazi mmoja wa kijiji cha Bulyaga kule Rungwe kwa jina Ambakisye Mwakatobe mwenye umri wa miaka 76 anasema katika siku za kale hawakuwahi kuona vyandarua vya kuzuia mbu. Anasema liona kwa mara ya kwanza chandarua cha kuzuia mbu.

Anasema visa vya Malaria vilianza kushuhudiwa miongo kadhaa iliyopita lakini wakaazi hawakuvihusisha na ongezeko la joto, wakiamini kuwa mbu badala yake walikuwa wakiwasili katika eneo hilo wakiwa kwenye mabasi kutoka maeneo ya nyanda za chini.

Malaria huchangia asilimia 30 ya mzigo wa magonjwa nchini tanzania lakini serikali kwa sasa inachukua hatua za kukabiliana na tatizo hilo.

hatua hizo zinajumuisha elimu ya afya ya umma katika wilaya hizo mpya zinazokabiliwa na maradhi hayo kuhusu usafi wa nyumbani na uhifadhi wa maji, na kuyasafisha maeneo ambayo mbu huzaana na pia matumzii ya vyandarua vya kuwazuia mbu.

Shirika la afya ulimwenguni WHO liliidhinisha aina 12 ya dwa za kuuwa wadudu ambazo zinaweza kutumiwa katika mipango ya kukabiliana na malaria.

Takwimu zilizotolewa na shirika la misaada la Marekani USAID zilibaini kuwa Tanzania ni mojawapo ya mataifa yaliyoathirika vibaya zaidi na malaria ulimwenguni huku ikisajili kati ya visa milioni 14 hadi 18 kila mwaka na vifo 60,000, ambapo asilimia 80 kati ya visa hivyo ni watoto walio chini ya miaka mitano.

Mwandishi: Bruce Amani
Mhariri:Josephat Charo