1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Miaka mitano baada ya vita vya Irak

Mtullya, Abdu Said20 Machi 2008

Miaka mitano ya kuivamia Irak rais George W.Bush bado anashikilia kusema kuwa uamuzi wake kuivamia nchi hiyo ulikuwa sahihi.

https://p.dw.com/p/DRjk
Rais G Bush wa Marekani.Picha: AP

Hotuba ya rais Bush kuadhimisha miaka mitano ya vita vya Irak ilikuwa sanduku la mkakasi, sawa na vita vyenyewe alivyoanzisha pamoja na washauri wake bila ya sababu ya kueleweka.

Katika hotuba hiyo Bush alijaribu kuhalalisha aumuzi wa Marekani katika kuivamia Irak. Amezungumzia juu ya ushindi dhidi ya wanaitikadi kali wa kiislamu nchini Irak. Bush ameeleza kuwa,  kama Marekani  isingechukua hatua ya kuivamia nchi hiyo,wanaitikadi kali hao wangelitenda mauaji halaiki.


Katika jitihada za aherini,kuhalalisha uvamizi wake, rais Bush alitoa picha ya kutisha,kumithilisha mandhari ambapo mtandao wa Alkaida nchini Irak unadhibiti  sekta ya mafuta na hivyo kuweza kupata  lukuki za fedha za kununulia ama kuunda  silaha za maangamizi.

Kauli hiyo, juu ya silaha  za maangamizi ndiyo iliyotumiwa miaka mitano iliyopita kama sababu ya majeshi ya Marekani kuingia Irak. Bush na washauri wake walikuwa wanarudia kauli hiyo mara kwa mara kama mashine iliyotiwa ufunguo.

Katika hotuba yake  jana, kuadhimisha mwaka  wa tano  tokea  majeshi yake yaingie Irak,Bush angalau angeliweza kujishika kifua na kutamka wazi  ,kuwa silaha hizo za maangamizi  hazikuwapo nchini Irak. Iwapo angesema hayo,huo ungelikuwa wasaa wa kihistoria,katika hatua za mwisho za utawala wake-huo ungelikuwa wasaa  wa nadra wa kusema ukweli.

Bush angeliweza,kuonesha  historia ya kutia moyo ,japo kwa dakika chache.Lakini  hakutumia fursa hiyo, lakini ni vizuri kwamba hakufanya hiyvo,kwani hata kama angelikiri kosa,huo ungelikuwa nusu ukweli.

Bush na washauri wake walijua kwamba hapakuwa na silaha  za maangamizi nchini Irak na wala nchi hiyo haikuwa kambi ya magaidi wa Alkaida waliopanga na kufanya mashambulio ya tareje 11 mwezi septemba nchini Marekani.

Kutokana na kutokuwapo sababu ya kweli ya kuivamia Irak Bush alimtumia waziri  wake wa mambo ya nje wa wakati huo Powell -alieheshimika sana- kuidanganya  dunia kwa kupitia kwenye Umoja wa Mataifa.

Katika hotuba yake Bush hakuonesha majonzi juu ya askari wake alfu nne waliouliwa na wala hakusema  chochote juu ya wairaki laki moja na alfu hamsini waliongamia ikiwa pamoja na watoto.

Vita vya Bush nchini Irak vinapaswa kuwa funzo kwa watakaomfuatia Ikulu.

Marekani asilani isianzishe balaa  jingine wakati mzuka uliopo sasa bado haujapugwa.