1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

MAONI YA WAHARIRI JUU YA MISRI

Abdu Said Mtullya11 Oktoba 2011

Wahariri wa magazeti ya Ujerumani wasema wana wasi wasi juu ya mapinduzi ya nchini Misri!

https://p.dw.com/p/12q4F
Wakristo wa madhehebu ya Coptic wakiandamana mjini Cairo.Picha: picture-alliance/dpa

Wahariri wa magazeti leo wanatoa maoni juu ghasia zinazoendelea nchini Misri ambapo wakristo wa madhehebu ya Coptic wanadai haki zao.

Wahariri hao pia wanazungumzia juu ya uchaguzi wa bunge uliofanyika katika nchi jirani ya Poland. Matokeo ya uchaguzi huo yamethibitisha kuwa Poland ni sehemu thabiti ya Umoja wa Ulaya.

Juu ya matukio ya nchini Misri ,mhariri wa gazeti la Dithmarscher Landeszeitung anazitaka nchi za magharibi ziyafuatilie matukio hayo kwa makini,na ikiwa itadibi zichukue hatua za haraka. Mhariri wa Dithmarscher Landeszeitung anasema nchi za magharibi zinayo turufu ya shinikizo, yaani fedha. Kwa hiyo anasema lazima watawala wa Misri wa sasa na wa siku za usoni watambue kwamba,misaada ya kiuchumi itapelekwa katika nchi yao ikiwa haki za wananchi wao wote zitatambuliwa na kuheshimiwa

Mhariri wa gazeti la Westfälische Nachrichten anasema wasi wasi unazidi kuongezeka juu ya hali ya nchini Misri. Na anauliza: jee mapambazuko ya Kiarabu sasa yanafuatiwa na mapukutiko ya Kimisri? Mhariri huyo anafafanua kwa kueleza kwamba pana wasi wasi huenda matumaini ya kuleta mabadiliko yakazimwa kikatili nchini Misri. Nchi hiyo sasa imesimama katika njia panda. Mchakato wa demokrasia hauwezi kujileta wenyewe. Hakuna uhakika iwapo wakristo wa madhehebu ya Coptic wataishi kwa amani baada ya uchaguzi kufanyika nchini Misri.

Mhariri wa Westfälische Nachrichten anasena ikiwa jumuiya ya Undugu wa Kiislamu itashika hatamu, ni wazi kwamba stahamala ya kidini haitakuwa miongoni mwa masuala ya kipaumbele katika ajenda ya mapambazuko ya Kiarabu! Naye mhariri wa Nürnberger anakubaliana na hoja ya Shirika la Kimataifa la kutetea haki za binadamu kwamba kinachotokea nchini Misri siyo ghasia za kidini. Bali kinachoshuhudiwa ni kwamba jeshi linawashambulia wakristo wanaoandamana kwa amani.

Mhariri wa gazeti la Hannoversche Allgemeine anazungumzia juu ya uchaguzi wa Bunge uliofanyika nchini Poland. Mhariri huyo anasema kuwa uchaguzi huo ni muhimu kwa sababu umetoa ishara kwamba Poland ni sehemu thabiti ya Umoja wa Ulaya. Jambo la pili ni kwamba umeonyesha kuwa zile enzi za kuendesha kampeni za chuki dhidi ya Ujerumani ili kujipatia kura sasa zimeshapita.

Hayo ameweza kuyaona kiongozi wa upinzani Jaroslav Kaczynski aliejaribu katika kampeni zake, kumshambulia Kansela wa Ujerumani Angela Merkel. Hoja hiyo inaungwa mkono na Mhariri wa gazeti la Volksstimme anaesema kuwa enzi za kutoa vidokezo vya propaganda dhidi ya Ujerumani ili kujipatia kura , sasa zimeshapita nchini Poland. Hata hivyo,gazeti la Volksstime linasema Poland inakabiliwa na mikingamo ,kati ya usasa na ukale, ujana na uzee na utajiri na umasikini. Ikiwa Poland italeta uelewano wa kitaifa, nchi hiyo itaweza kuwa nguzo muhimu katika Umoja wa Ulaya.

Mwandishi:Mtullya, Abdu/Deutsche Zeitungen.

Mhariri: Othman Miraji