1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri juu ya mkutano baina ya Merkel na Medvedev

Abdu Said Mtullya19 Julai 2011

Katika maoni yao wahariri wa magazeti pia wanazungumzia juu ya mkutano wa mashauriano baina ya Ujerumani na Urusi.

https://p.dw.com/p/11zQC
Kansela Merkel na Rais Medvedev mjini Hannover kaskazini mwa UjerumaniPicha: dapd

Katika maoni yao leo wahariri wa magazeti ya Ujerumani wanazungumzia juu ya mkutano wa mashaurino baina ya Ujerumani na Urusi, juu ya kashfa ya udakizaji wa simu nchini Uingereza na juu ya harakati za kuleta mapinduzi katika nchi za kiarabu.

Gazeti la Volksstimme linatoa maoni juu ya mkutano wa kilele baina ya Kansela wa Ujerumani Angela Merkel na Rais wa Urusi Dmitry Medvedev unaoendelea mjini Hannover kaskazini mwa Ujerumani.

Mhariri wa gazeti hilo anauangalia mkutano huo, kwa kutilia maanani kwamba unafanyika baada ya Ujerumani kuamua hivi karibuni kuacha kutumia nishati ya nyuklia. Anasema mahitaji ya gesi ya Ujerumani yataongezeka kutokana na uamuzi huo. Urusi inayo akiba kubwa ya gesi. Lakini wakati huo huo mhariri huyo anasema Urusi nayo pia ina malengo mengine juu ya Ulaya magharibi na siyo kuiuzia gesi tu.

Hali ya uchumi wa Ujerumani ni nzuri sana wakati ambapo wajerumani wanazisikia habari juu ya migogoro ya kiuchumi, na ya bajeti katika nchi nyingine.

Hayo anayasema mhariri wa gazeti la Bild, lakini pia anatahadharisha "Uchumi wa Ujerumani unaendelea kustawi na wataalamu wanatabiri kuwa hali itaendelea kuwa nzuri." Mhariri huyo anasema hayo ni mafanikio yanayotokana na ubunifu viwandani na ustadi wa wafanyakazi. Kutokana na mafanikio hayo Wajerumani wanao uwezo mkubwa wa kukabiliana na migogoro mikubwa kwa mafanikio. Lakini mhariri huyo anasema mafanikio hayo yasiwe sababu ya kuwafanya Wajerumani waridhike na wapunguze juhudi.

Naye mhariri wa gazeti la Express anasema wakati sarafu ya Euro inayumba, na wakati nchi kadhaa barani Ulaya zinakaribia kufilisika Ujerumani inazidi kustawi kiuchumi, lakini pia anatahadharisha kwa kusema kuwa Wajerumani wanapaswa kuushikilia uzi ule ule, kwa sababu washindani kutoka bara la Asia hawalali asilani.

Gazeti la Donaukurier linazugumzia juu ya kashfa ya udakizaji wa simu za watu nchini Uingereza, kwa kiwango cha aibu kubwa. Lakini linauliza jee nchini Ujerumani ,magazeti yanazingatia misingi ya staha?

Mhariri wa gazeti hilo anaeleza kuwa wadakuzi walidakiza hata barua za msichana alieuawa ,aliekuwa na umri wa miaka 13. Anasena ni jambo lisiloweza kueleweka nchini Ujerumani!Lakini inahalisi kulitilia mashaka gazeti la Bild. Kwani gazeti hilo limeshachapisha orodha ndefu ya kashfa. Gazeti hilo linalochapisha nakala milioni 2.8 kwa siku na linajitambulisha kuwa mlinzi wa demokrasia , lakini ukweli ni kwamba linachapisha zaidi mambo yanayohusu ngono na burudani!

Gazeti la Westfalen-Blatt linatoa maoni juu ya mapinduzi katika nchni za kiarabu. Gazeti hilo linasema nchi za magharibi zimeshiriki kijeshi na kwa diplomasia ya uangalifu. Lakini linatalia maanani kuwa wakati Nato inamshambulia dikteta wa Libya ,Gaddafi, Ujerumani inawauzia madikteta wa Saudi Arabia silaha.! Kwa hiyo wanaharakati wanaopigania demokrasia katika nchi za kiarabu wanahisi kuwa wamesalitiwa kwa mara nyingine tena.

Mwandishi/Mtullya abdu/Deutsche Zeitungen/

Mhariri/ Abdul-Rahman,Mohammed