1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Erdogan asema hatageuka nyuma

12 Mei 2016

Wahariri wanatoa maoni juu ya mvutano baina ya Uturuki na Umoja wa Ulaya na juu ya ziara ya Rais Obama katika mji wa Hiroshima.

https://p.dw.com/p/1ImLm
Picha: Getty Images/AFP/A. Altan

Uturuki imesema imeshayatimiza masharti yote yaliyotolewa na Umoja wa Ulaya ili wananchi wake waweze kuingia katika nchi za Umoja wa Ulaya bila ya kuhitaji vibali. Lakini Umoja wa Ulaya inaitaka Uturuki iibadilishe sheria yake juu ya kupambana na ugaidi.

Juu ya mvutano huo gazeti la "Thüringischen Landeszeitung" linasema mvutano huo unayatishia makubaliano yaliyofikiwa na Uturuki juu ya kuwadhibiti wakimbizi. Mhariri wa gazeti hilo anasema hayo ni matokeo ya kushirikiana na dikteta.

Mhariri wa gazeti la "Nordwest" anahoji kwamba kiongozi wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan ni mpenda madaraka anaevichukia vyombo vya habari huru.

Mhariri huyo anasema kiongozi kama huyo anapenda kuwatisha watu wengine na kwa hivyo ,anaemini kwamba Erdogan anaweza kuwa suluhisho la mgogoro wa wakimbizi ama ni mpumbavu kisiasa au ameraibuka mapenzi ya Uturuki.

Gazeti la "Westfälische Nachrichten" linasema mvutano baina ya Uturuki na Umoja wa Ulaya ni la jambo hatari. Gazeti hilo linatahadharisha kwamba, mkataba juu ya wakimbizi unaweza kusambaratika ikiwa suala la vibali kwa Waturuki halitatuliwa .

Hata hivyo litakuwa shauri zuri kwa Umoja wa Ulaya kumwonyesha Erdogan mipaka yake.Mhariri wa gazeti la "Westfälische" anasisitiza kwamba serikali ya Uturuki bado haijayatekeleza masharti yanayotakiwa na Umoja wa Ulaya.Asilani Erdogan asiachiwe uwanja wa kujimwaga anavyotaka.

Wakimbizi wasongamana nchini Ugiriki
Wakimbizi wasongamana nchini Ugiriki

Spika wa Bunge Mwislamu

Gazeti la "Südwest Presse linayatilia maanani mageuzi yaliyotukia katika jimbo la Baden-Württemberg".

Kwa mara ya kwamba Bunge la jimbo hilo litakuwa na Spika mwanamke ambae ni Mwislamu. Mhariri wa gazeti hilo anasema kuchaguliwa mama huyo, Muhterem Aras kuwa Spika wa jimbo hilo kunathibitisha moyo wa stahamala na mabadiliko makubwa ya kijamii.Kuchaguliwa kwake kunaashiria uwazi na uhuru wa dini katika nyakati hizi nchini Ujerumani ambapo chama kipya cha wapinga Uislamu kinajaribu kuchochea mitazamo mipya.

Rais Barack Obama anatarajiwa kufanya ziara katika mji wa Hiroshima baadae mnamo mwezi huu.

Hiyo itakuwa ziara ya kwanza katika mji huo wa Japan kufanywa na Rais wa Marekani aliemo madarakani.Mji huo ulipigwa bomu la atomiki na Marekani wakati wa vita vikuu vya pili.

Juu ya ziara hiyo gazeti la "Sächsische" linasema hata ikiwa Rais Obama anataka kutoa ishara ya kupigania kuondolewa silaha zote za nyukulia duniani, Rais huyo anajenga matumaini mengine. Hata hivyo matumaini ya watu wa Japan juu ya Rais wa Marekani kuomba radhi hayatatimizwa.

Lakini mhariri wa gazeti la "Sächsiche" anasema ziara ya Obama nchini Japan ina lengo la kuukabili ushawishi wa kisiasa wa China katika eneo la Pasifik.

Mwandishi:Mtullya Abdu./Deustche Zeitungen.

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman