1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri juu ya Ukraine na Afghanistan

Abdu Said Mtullya12 Desemba 2013

Wahariri wanatoa maoni juu ya mgogoro wa nchini Ukraine na juu ya Afghanistan baada ya kuondoka majeshi ya kimataifa mwakani

https://p.dw.com/p/1AXo8
Maandamano ya kuipinga serikali nchini Ukraine
Maandamano ya kuipinga serikali nchini UkrainePicha: DW/L. Gryschko

Gazeti la "Hannoversche Allgemeine linazungumzia juu ya mgogoro wa kisiasa unaoikabili Ukraine. Mhariri wa gazeti hilo anasema suala la nchi hiyo kujiunga na Umoja wa Ulaya halitatatuliwa kwenye makao makuu ya Umoja huo na wala halitatuliwa kwa njia ya maandamano.Ukraine inahitaji kufikia mwafaka juu ya suala hilo.Na wajibu wa Umoja wa Ulaya ni kusaidia tu.

Gazeti la "Cellesche" linasema Ukraine inakabiliwa na matatizo makubwa ya kiuchumi, na ndiyo sababu sasa inajaribu kuigonganisha Urusi na Umoja wa Ulaya, kwa kutumai kwamba mwenye mfuko mkubwa ndiye atakaelipa. Utakuwa ushauri mzuri kwa Umoja wa Ulaya kujiweka kando ya mashindano hayo.

Naye mhariri wa "Der Tagesspiegel" anasema siyo jambo la kushangaza kwamba Rais Viktor Yanukovych amekataa kuutia saini mkataba na Umoja wa Ulaya.Mhariri huyo anaeleza kwamba mkataba uliowasilishwa kwa Ukraine si kitu kingine zaidi ya makubaliano ya biashara huru kwani ,Umoja wa Ulaya una mikataba kama hiyo na nchi kama Tunisia,Mexico na Afrika ya Kusini, na kwa hivyo hauna umuhimu mahsusi kwa nchi ya Ulaya kama Ukraine.

Usalama wa Afghanistan

Na sasa tugeukie Afghanistan ambako majeshi ya kimataifa yanayoongozwa na NATO yanajitayarisha kuondoka nchini humo mwakani.Jee usalama wa nchi hiyo utakuwaje majeshi hayo yakiondoka? Gazeti la "Augsburger Allgemeine" linalijibu swali hilo kwa kuizingatia kauli iliyotolewa na Waziri wa ulinzi wa Ujerumani Thomas de Maizere.

Waziri de Maizere amesema taliban wanaweza kuleta vurumai, lakini hawawezi kuidhibiti Afghanistan yote. Mhariri wa gazeti la" Augsburger Allgemeine" anasema kauli ya Waziri huyo inasumbua kidogo kwa sababu anajaribu kutoa picha ya kuliwaza. Yawezekana kwamba taliban hawana tena uwezo wa kuiteka nchi nzima ya Afghanistan, lakini baada ya kuondoka kwa majeshi ya kimataifa nchini Afghanistan,taliban watakuwa na uwezo wa kijeshi wa kusababisha vurumai na kukwamisha mambo.


Mwandishi: Mtullya Abdu/Deustche Zeitungen

Mhariri: Mohammed Khelef