1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Berlusconi awakashifu wahanga wa tetemeko!

Abdu Said Mtullya9 Aprili 2009

Waziri mkuu wa Italia Silvio Berlusconi awakashifu wahanga wa tetemeko la ardhi.

https://p.dw.com/p/HTXJ
Waziri Mkuu wa Italia S Berlusconi aliewakashifu watu waliokumbwa na maafa ya tetemeko la ardhi.Picha: AP

Wahariri wa magazeti ya Ujerumani leo wazungumzia juu ya maadili ya familia na juu ya maafa yaliyosababishwa na matetemeko ya ardhi nchini Italia.

Kuhusu Italia wahariri hao hawazungumzi hasa juu ya maafa yenyewe bali juu ya kauli iliyotolewa na waziri mkuu wa nchi hiyo Silvio Berlusconi juu watu waliofikwa na maafa hayo.

Juu ya maadili ya familia nchini Ujerumani mhariri wa gazeti la Dresdener Neueste Nachrichten anasema wazazi wakati wote wanataka wanachosema na wanachofanya kionekane kuwa ni sahihi kwa watoto wao.

Mhariri huyo anasema ,inawawia vigumu wazazi hao kujaribu kusimama katika safu moja na watoto wao kwa njia ya mawasiliano.Kutokana na hayo mambo huenda mrama-wazazi wanashindwa kuwasilisha maadili ya heshima,stahamala na desturi. nzuri.

Lakini vipi wazazi wataweza kuwasilisha maadili kwa watoto wao ili kujenga familia nzuri ? Gazeti la Neue Presse linasema katika maoni yake kwamba enzi za mkono wa chuma zimeshapita!Hatahivyo gazeti linasema zipo familia nzuri katika sehemu fulani japo mazingira ni tofauti.Na ndiyo sababu kwamba serikali inaweza kusaidia katika kuweka mazingira mazuri ili kuziendeleza familia.

Watu zaidi ya 270 wamekufa kutokana na tetemeko la ardhi nchini Italia. Maalfu ya watu wengine wamepoteza makazi yao.Serikali ya Italia inatoa misaada kwa watu hao ikiwa pamoja na kuwaweka katika mahema.

Waziri mkuu wa nchi hiyo Silvio Berlusconi amewaambia watu hao waliofikwa na maafa wajione kana kwamba wapo kwenye kambi ya likizo tu !Kauli hiyo imewakasirisha watu nchini Italia na kwengineko.

Gazeti la Die Glocke linasema watu huropokwa mara nyingine. Hayo yametokea kwa wanasiasa wa Ujerumani vilevile.Hatahivyo kauli yake imetoa picha mbaya juu ya Italia.

Na gazeti la Nürnberg linasema kauli ya waziri mkuu Berlusconi kuwaambia watu waliofikwa na janga wafurahi kama watu waliopo kwenye kambi ya likizo ni maafa.

Lakini gazeti hilo linasema mtu kama huyo hawezi kufikwa tena na maafa kwa sababu yeye mwenyewe tayari ni maafa.Kwa usemi mwingine,maafa hawezi kufikwa na maafa.


Mwandishi: A.Mtullya

Mhariri:M.Abdul-Rahman