1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wahariri waonya dhidi ya deni kubwa.

Abdu Said Mtullya23 Desemba 2009

Wahariri wa magazeti ya Ujerumani watoa maoni juu ya bajeti.

https://p.dw.com/p/LCTm
Waziri wa fedha wa Ujerumani Wolfgang Schäuble akifafanua juu ya bajeti.Picha: AP

Wahariri wa magazeti ya Ujerumani leo wanatoa maoni yao juu ya kodi na bajeti ya matumizi ya kawaida, na wengi wao wanatahadharisha juu ya hatari ya kuongezeka kwa matumizi hayo.

Ni siku chache tu zilizopita ambapo waziri wa fedha wa Ujerumani Wolfgang Schäuble aliwasilisha bajeti inayoonyesha kwamba serikali ya Ujerumani itaendelea kukopa na kutenga mfuko mkubwa kwa ajili ya matumizi ya kawaida.

Wahariri wa magazeti wanatahadharisha juu ya hatari ya deni kubwa.Kwa mfano mhariri wa gazeti la Oldenburgische Volkszeitung anasema hali ya fedha nchini siyo nzuri kabisa lakini njia ya kukabiliana na hali hiyo siyo kupandisha mchango wa bima ya wasiokuwa na ajira.

Mhariri huyo anaeleza kwamba deni kubwa, mapendekezo duni juu ya kupunguza gharama pamoja na uchumi dhaifu ni mambo yanayochangia kuifanya hali ya fedha iwe mbaya nchini.Lakini haitakuwa sawa kuingiwa na kiherehere.Kwa hiyo kujaribu kukabiliana na hali hiyo kwa kuongeza mchango wa bima ya wasiokuwa na ajira hakuteleta manufaa.

Hatahivyo mhariri wa gazeti la Münchner Merkur hakubaliani na hoja hiyo na anasema haitawezekana kupunguza daima, mchango wa bima ya ajira kwa asilimia 2.8. Gazeti hilo linafafanua kuwa wataalamu wanaonya dhidi ya kupunguza mchango wa bima ya ajira kutokana na kuongezeka kwa idadi ya watu wanaopoteza nafasi za kazi.

Kutokana na hali hiyo serikali italazimika kuongeza mfuko wa matumizi kwa ajili ya posho za watu hao wasiokuwa na ajira ikiwa kiwango cha mchango wa bima hakitapandishwa.

Gazeti la Braunschweiger Zeitung linasema ongezeko kubwa la bajeti ya matumizi ya kijamii ni sumu kwa uchumi wa nchi.

Gazeti hilo linaeleza kuwa matumizi makubwa ya kijamii yatayadhoofisha makampuni nchini na hivyo kuathiri ustawi wa uchumi.

Gazeti linasema kudhoofika kwa uchumi maana yake ni kuongezeka kwa idadi ya watu wanaopoteza nafasi za ajira na pia kuongezeka kwa deni la nchi.

Na mhariri wa gazeti la Rhein-Zeitung anasisitiza ulazima wa kuanza kuchukuliwa kwa hatua za kupunguza matumizi.Anasema wananchi wote wanapaswa kutambua kwamba serikali haitaweza kuendelea kutoa hisani.

Katika maoni yake, gazeti la Emder linatanabahisha juu ya hali mbaya inayozikabili serikali za mitaa.Gazeti linasema serikali hizo zinakabiliwa na tatizo la mapato ya chini ya kodi na ongezeko la matumizi ya kijamii.Gazeti linatilia maanani kwamba serikali hizo zinakabiliwa na nakisi ya Euro bilioni 6.7

Gazeti linasema hizo ni nyendo za hatari katika maendeleo ya nchi.Wanasiasa wote lazima wayatilie hayo maanani.

Mwandishi/Mtullya Abdu/Duetsche Zeitungen.

Mhariri/Othman,Miraj