1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Magazetini

Abdu Said Mtullya21 Januari 2010

Chama cha rais Obama chapata pigo kutokana na kupoteza kiti cha seneti katika jimbo la Massachusetts.

https://p.dw.com/p/LcTu
Rais Barack Obama apata pigo kutokana na kupoteza kiti cha seneti katika jimbo la Massachusetts.Picha: AP

Chama  cha Demokratik cha rais  Barack Obama  kimepoteza  kiti cha  seneti katika jimbo la Massachusetts ambalo hadi  sasa lilikuwa ngome thabiti ya chama hicho nchini Marekani. Jee kupoteza kiti hicho kuna maana gani kwa rais  Obama.?

Wahariri  wa magazeti  ya Ujerumani wanatoa maoni yao.

Gazeti la Frankfurter Rundschau linasema matokeo ya uchaguzi katika jimbo la Massachusetts ni maafa kwa rais Obama. Mhariri wa  gazeti hilo anasema  ikiwa chama cha  rais Obama  kimepoteza kiti  katika jimbo ambalo hadi  sasa lilikuwa ngome  ya  chama hicho, hiyo  ni  ishara kwamba chama hicho kimo katika  hatari  ya kupigwa radi katika uchanguzi wa  bunge utakaofanyika  baadae mwaka huu nchini Marekani.

Mhariri wa gazeti la Frankfurter Allgemeine anaeleza wazi juu ya kushindwa  kwa chama cha rais Obama katika uchaguzi wa seneti kwenye  jimbo la Massachusetts:

Kuchaguliwa kwa mjumbe wa chama cha Republican kuwa  seneta wa  jimbo la Massachusetts , lililokuwamo mnamo mikono ya akina Kennedy kwa dahari  za miaka, kutagubika  siasa za Marekani na za rais Obama. Mhariri wa gazeti hilo anasema matokeo ya uchaguzi huo ni tetemeko la ardhi la kisiasa  nchini Marekani. 

Gazeti hilo pia linatilia maanani kwamba chama  cha Obama kilipoteza kiti hicho  jana, siku  ambapo  aliadhimisha muda wa mwaka mmoja tokea aingie madarakani.

Maana ya kupoteza  kiti hicho ni kwamba chama  cha Demokratik sasa kimepoteza wingi  wake  katika seneti.


Gazeti la Märkische Oderzeitung linasema ushindi wa mjumbe wa  chama cha Republican katika jimbo la Massachusetts  ni pigo kubwa   kwa wananchi milioni  45 wa Marekani  wasiokuwa na bima ya afya.

Na gazeti la Wetzlarer linakubaliana  na tathmini hiyo kwa kusema kwamba watu  wa jimbo la Massachusetts  wametumia vikaratasi kuupinga  mpango wa rais Obama wa kuleta mageuzi  katika mfumo wa afya. Gazeti hilo linasema  chama Demokratic hakikupoteza tu, ngome yake kuu,  bali pia kimepoteza wingi wake katika  seneti.

Ndiyo kusema, mhariri  wa gazeti hilo anaeleza, sasa kuna hatari ya  kushindikana kwa  mpango  wa rais Obama  wa kuleta mageuzi katika mfumo wa afya.

Na gazeti  la Thüringische Landeszeitung linatathmini  ifuatavyo matokeo ya  uchaguzi katika  jimbo  la  Massachusetts:
"Yumkini watu katika  sehemu  zingine  za dunia  wanashindwa  kuelewa  kwa  nini Wamarekani  wengi  wanaipinga  bima  ya afya itakayotolewa    na serikali.

Lakini msimamo wa watu hao una maana gani kwetu?"  Gazeti  la Thüringische Landeszeitung linafafanua kwa kusema, ikiwa rais Obama  anashindwa nchini mwake kuchukua hatua zilizopaswa  kuchukuliwa siku nyingi, ni hatua gani  atakazoweza kuzichukua katika medani  ya  kimataifa-yeye kama  rais mwenye nguvu.?

Mwandishi Mtullya Abdu/Duetsche Zeitungen.

Mhariri: Miraji Othman