1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri wa magazeti ya Ujerumani.

Abdu Said Mtullya28 Januari 2010

Wahariri wa magazeti wanazungumzia juu ya mkutano kuhusu Afghanistan unaofanyika mjini London.

https://p.dw.com/p/Lim6
Rais Hamid Karzai wa Afghanistan.Picha: AP

Mkutano  wa kimataifa  juu ya Afghanistan unafanyika mjini  London leo , pamoja na masuala mengine, kujadili njia  za  kuwakaribia wataliban.

Wahariri wa magazeti  ya hapa nchini wanatoa maoni yao juu ya mkutano huo.
Wahariri hao  pia wanazungumzia juu  ya hotuba iliyotolewa jana na rais Shimon  Peres wa  Israel kwenye bunge la Ujerumani katika  maadhimisho ya mwaka wa  65  tokea  kukombolewa  kwa watu waliokuwa  wamefungwa katika kambi ya Auschwitz nchini  Poland.

Juu ya mkutano unaojadili  suala  la Afghanistan mjini London  gazeti la Rhein-Necker linasema , kuwa mkutano huo hautaisogeza Afghanistan kwenye hatua  ya  amani, badala yake mkutano huo unatumiwa na nchi  za magharibi kwa maslahi yao ya kisiasa.Gazeti hilo linaeleza kuwa mkutano huo ni  jukwaa  la kisiasa linalotumiwa na nchi za magharibi kwa  lengo  la kufafanua mkakati  wa kujiondoa Afghanistan.
Gazeti la Süddeutsche Zeitung  linatilia maanani kwamba rais  Karzai anajaribu kutafuta njia  ya kuwakaribia  wataliban. Gazeti linasisitiza kwamba hilo ni jukumu la rais huyo kwa sababu haiwezekani  kwake  kuendelea  kwa muda mrefu zaidi kutegemea kulindwa na majeshi  ya  nchi za nje.  Gazeti hilo linaeleza kwamba kinachowezekana  kufanyika  nchini Afghanistan ni kujaribu  kuwaingiza wataliban katika jamii  na kujaribu  kuwatengenaisha na  alkaida;  lakini zaidi  ya hayo  hakuna kinachoweza kufanyika nchini humo.

Gazeti la Märkische Oderzeitung linazungumzia juu ya mkutano uliofanyika jana , pia mjini London, kuhusu Yemen. Gazeti hilo linasema Yemen imegeuka kuwa nchi isiyokuwa na matumaini kama Somalia kwa  sababu kwa muda mrefu, hakuna   alietaka kujua kilichokuwa kinaendelea katika nchi hiyo. Lakini sasa wakati dunia inataka kujua kinachotokea, mambo yameshaenda mrama.

Umasikini unaongezeka kutokana na kupungua kwa mapato yanayotokana na mauzo ya mafuta. Mhariri wa gazeti la  Märkische Oderzeitung anasema   umasikini ndio unaowafanya watu zaidi na zaidi  wajiunge na makundi ya wanaitikadi kali wa   kiislamu. Gazeti linasema, ndiyo serikali ipo nchini humo, lakini  inazidi kupoteza  udhibiti  wa nchi.
Rais Shimon  Peres wa Israel  jana  alilihutubia bunge la  Ujerumani katika  maadhimisho  ya mwaka  wa 65 tokea kukombolewa kwa kambi ya Auschwitz iliyotumika kuwaangamiza maalfu  kwa maalfu  ya watu na hasa wayahudi. Katika hotuba yake rais huyo alitoa mwito wa kuendelea kuwakumbuka wahanga wa  Auschwitz. Gazeti la Kieler Nachrichten linaeleza kuwa sababu  ya kutoa mwito huo ni kwamba wapo watu nchini Ujerumani wanaofikiri  kwamba kumbukumbu juu ya maangamizi   ya wayahudi siyo jambo la lazima sana. Lakini mhariri  wa gazeti la Aachener anasema asietaka kuyakumbuka maangamizi  ya   wayahudi hasikii vizuri.

Mhariri wa gazeti hilo anasisitiza umuhimu  wa hotuba ya rais Peres pia kutokana na kutambua ukweli kwamba wapo watu nchini  Ujerumani wanaojaribu kufananisha unyama  waliofanyiwa wayahudi na masaibu ya wapalestina.

Mwandishi/Mtullya Abdu /Deutsche  Zeitungen.

Mhariri/Othman Miraji