1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri wa magazeti

24 Julai 2007

Chama cha waziri Mkuu Erdogan AK kimeshinda uchaguzi wa bunge nchini Uturuki. Katika maoni yao leo wahariri wa magazeti ya Ujerumani wanazungumzia juu ya ushindi wa chama hicho.

https://p.dw.com/p/CHSK

Mhariri wa gazeti la LÜNEBURGER LANDESZEITUNG anasema ushindi huo maana yake ni kukubaliwa kwa sera za mageuzi zinazotekelezwa nchini Uturuki na chama cha waziri mkuu Erdogan.

Hivyo basi , anasema mhariri wa gazeti hilo , bwana Erdogan anastahili kuungwa mkono , kwani ushindi huo umeimarisha dhamira ya serikali yake katika kuilekeza Uturuki katika Umoja wa Ulaya.

Gazeti la LÜBECKER NACHRICHTEN linaunga mkono mtazamo huo kwa kutilia maanani kuwa waturuki wengi wamekichagua chama cha waziri Mkuu Erdogan kinachotetea na kutekeleza sera za mageuzi. Anaeleza kuwa wastahiki nchini Uturuki wamekichagua chama kinachoonesha kuwa inawezekana kwa maadili ya demokrasia na uhuru kutangamana na uislamu. Hiyvo basi mhariri wa gazeti hilo pia anautaka Umoja wa Ulaya uizingatie Uturuki kama mjumbe anaestahili kuwa mwanachama wa Umoja huo .

Lakini katika maoni yake gazeti la WESTFÄLISCHE RUNDSCHAU linatahadharisha juu ya viongozi wenye uzito kwenye Umoja wa Ulaya wanaoweza kuitibulia Uturuki , yaani Kansela Angela Merkel wa Ujerumani na rais Nicolas Sarkozy wa Ufaransa.

Mhariri wa gazeti hilo anatilia maanani kuwa viongozi hao wawili ni wapinzani wakubwa wa lengo la Uturuki kujiunga na Umoja wa Ulaya. Gazeti pia linatilia maanani kuwa mazungumzo juu ya Uturuki kuwa mwanachama wa Umoja huo yanaenda polepole , na aghalabu maswali mengi yanaulizwa juu ya mazungumzo hayo.

Lakini, mhariri anasema Umoja wa Ulaya sasa hauna budi uitikie ishara iliyotolewa na wananchi wa Uturuki: anasema Ulaya itanufaika sana na Uturuki inayotawaliwa katika misingi ya kidemokrasia ,sambamba na uislamu.

AM.