1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wahariri waonya dhidi ya siasa kali.

Abdu Said Mtullya20 Mei 2009

Wahariri wa magazeti ya Ujerumani leo wanazungumzia juu ya ripoti ya serikali kuhusu itikadi kali nchini.

https://p.dw.com/p/Hu5N

Leo hii wahariri wa magazeti ya Ujerumani wanazungumzia juu ya taarifa ya mwaka ya serikali ya Ujerumani juu ya siasa kali nchini.Wahariri hao pia wanatoa maoni yao juu ya umasikini hapa nchini.
Taarifa inayotolewa na serikali ya Ujerumani kila mwaka juu ya siasa kali nchini, inaonyesha kuwa uhalifu ulitotendwa na makundi ya mrengo mkali wa kulia umeongezeka kwa asilimia 16.

Mhariri wa gazeti la Neue Osnabrücker anasema makundi yenye siasa za mrengo mkali kama vile, mafashisti mamboleo , yanazidi kuwa katili, yanazidi kuua, yanaendelea kujaribu kuua na kuteketeza mali za umma kwa moto. Gazeti hilo linasema jamii lazima iwe na jibu thabiti katika kukabiliana na hali hiyo.

Gazeti linasema jibu hilo lianzie mitaani. Polisi asilani wasisubiri mpaka chuki na ghasia zilipuke . Lakini la muhimu zaidi ni kuwekwa kwa sera ya busara itakayowarudisha vijana katika maadili ya demokrasia.

Gazeti la Ostsee linatahadharisha juu ya hatari ya itikadi kali kwa kusema kuwa hali iliyopo inatisha. Mtu haitaji kuwa nabii ili kuweza kutabiri kwamba siasa za itikadi kali zinaweza kustawi katika mazingira magumu ya uchumi. Kwa hiyo kila mwenye dhamira ya kupambana na baa la siasa kali, hana budi aonyeshe dhamira hiyo kwa kupiga kura tarehe 7 mwezi ujao , katika uchaguzi wa bunge la Umoja wa Ulaya.

Gazeti la Main Post leo linazungumzia taarifa juu ya umasikini nchini Ujerumani.Gazeti hilo linatilia maanani kwamba ripoti hiyo inaonyesha takwimu za mwaka 2007- yaani kabla ya kuanza kwa mgogoro wa uchumi. Mhariri wa gazeti hilo anaeleza kuwa kiwa idadi ya masikini itaongezeka na ikiwa umasikini wa watu hao utazidi kuwa mkubwa,wakati matajiri wanazidi kuwa tajiri, basi ni wazi kwamba pana kasoro katika mfumo wa kijamii.Hali kama hiyo inaweza kuhatarisha usalama wa ndani .Wanasiasa asilani wasipuuze hayo. Lazima wachukue hatua sasa, na siyo baada ya uchaguzi mkuu.

Mkutano mkuu wa 32 wa kanisa la kiprotestanti nchini Ujerumani unafanyika mjini Bremen.Hizo ni habari za kufurahisha anasema mhariri wa gazeti la Stuttgarter Nachrichten.Sababu ni kwamba asilimia 40 ya washiriki kwenye mkutano huo ni vijana wenye umri uliopo chini ya miaka 30. Mhariri wa Sttugarter Nachrichten anasema hiyo ni ishara ya matumaini, mtu anapotambua kwamba waumini wengi walilihama kanisa katika miaka ya hivi karibuni.