1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

MAONI YA WAHARIRI

Abdu Said Mtullya1 Septemba 2011

Baraza la Mpito la Libya lakasirishwa na hatua ya Algeria ya kuipa hifadhi familia ya Gaddafi.

https://p.dw.com/p/12QXI
Mapambano ya kumng'oa Gaddafi yaingia katika hatua za mwisho katika mji wa SirtePicha: dapd

Wahariri wa magazeti leo wanazungumzia juu ya uhusiano baina ya Algeria na Baraza la Mpito la nchini Libya kufuatia hatua ya Algeria ya kuipa familia ya Gaddafi hifadhi ya kisiasa.

Mhariri wa gazeti la Sächsiche anasema kiongozi wa Algeria Bouteflika ameikaribisha familia ya Gaddafi kwa shabaha maalumu.

Mhariri huyo anaeleza kuwa lengo la Bouteflika ni kujenga kizingiti kati ya watu wa Algeria na waasi wa Libya.Nia yake ni kuhakikisha kwamba watu wake hawawaungi mkono waasi wa Libya.

Gazeti la Badische pia limetoa maoni juu ya uhusiano kati ya Algeria na Baraza la Mpito la waasi wa Libya. Mhariri wa gazeti hilo anautilia maanani uwezekano wa Kanali Gaddafi pia kukimbilia Algeria. Mhariri huyo anaeleza kwamba watu nchini Libya wanahofia kwamba huenda Gaddafi mwenyewe na wanawe Saadi na Saif al Islam pia wakakimbilia Algeria, licha ya uvumi huo kukanushwa. Lakini jambo la kushangaza ni kwamba nchi za magharibi mpaka sasa hazijasema lolote juu ya Algeria kuipa familia ya Gaddafi hifadhi , hasa mtu akitambua kwamba mtoto wa Gaddafi Hannibal anapaswa kufikishwa mbele ya sheria. Msimamo wa nchi za magharibi wa kunyamaza kimya juu ya matukio hayo unaweza kutathimiwa na Algeria kuwa ni kuiunga mkono nchi hiyo. Na hayo yatakuwa na maana ya kuwa tayari kumpa Gaddafi hifadhi vile vile. Ikiwa Gaddafi hatakamatwa, basi wafuasi wake wataendelea kuleta ghasia nchini Libya.

Mhariri wa gazeti la Münchner Merkur anasema Baraza la Mpito la Libya linapaswa kuwa na uangalifu juu ya kauli linazozitoa kuhusu msimamo wa Algeria.Mhariri huyo anesema ikiwa Gaddafi ataamua kuenda Algeria,nchi hiyo itamkaribisha na itampa ulinzi. Baraza la Mpito la Libya linatambua kwamba zipo taratibu za kikabila zinazopaswa kuheshimiwa. Waasi wa Libya wanayajua hayo vizuri! Kwa hiyo wanapaswa kuwa na nadhari ulimini wanapotoa kauli juu ya msimamo wa Algeria .Madai yaliyotolewa na waasi kwamba hatua ya Algeria kuipa familia ya Gaddafi hifadhi, ni kitendo cha uchokozi, yanaweza kuzisogeza Libya na Algeria kwenye mvutano wa hatari.

Lakini mhariri wa gazeti la Schwäbische analalamika kwamba nchi za magharibi zimenyamaza kimya juu ya hatua iliyochukuliwa na Algeria ya kuipa familia ya Gaddafi hifadhi ya kisiasa. Ukimya wa nchi za magharibi utaipa Algeria nguvu ya kumpa Gaddafi hifadhi vile vile. Lakini nchi za magharibi zinapaswa kujua kwamba Gaddafi ataendelea kuwa hatari ikiwa hatatiwa mbaroni.

Mwandishi Mtullya abdu/ Deutsche Zeitungen/

Mhariri/Josephat Charo