1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri

Abdu Said Mtullya4 Desemba 2014

Wahariri leo wanazungumzia juu ya mfungamano dhidi ya kundi la dola la kiislamu , haki za wakimbizi nchini Ujerumani. Pia wanatahadharisha juu ya hatari ya vinu vya nyuklia vilivyochakaa, nchini Ukraine.

https://p.dw.com/p/1Dz92
Wajumbe kwenye mkutano dhidi ya dola la Kiislamu
Wajumbe kwenye mkutano dhidi ya dola la KiislamuPicha: Reuters/Eric Vidal

Gazeti la "Flensburger Tageblatt" linatoa maoni juu ya mkutano wa nchi zaidi ya 60 zilizofungamana katika harakati za kupambana na ugaidi wa kundi la dola la kiislamu. Mhariri wa gazeti hilo anashauri kwamba mchango mkubwa kabisa katika harakati za kuapambana na magaidi hao unapaswa kutoka kwa nchi za kiislamu. Ni wajibu wa nchi kama Saudi Arabia na Uturuki kusisitiza kwa nchi zenye imani kama zao kwamba Uislamu ni dini ya amani .

Uturuki yapaswa kuutambua mchango wa Wakurdi

Mhariri wa gazeti la "Flensburger Tageblatt" anaitaka Uturuki itambue kwamba, wapiganaji wa kikurdi wa kaskazini mwa Iraq, wanaopambana na magaidi wa dola la kiislamu wanastahiki kuungwa mkono na Uturuki. Gazeti la "Südwest Presse" linatilia maanani kwamba mfungamano wa kupambana na kundi la dola la kiislamu sasa umezileta pamoja nchi nyingi.

Mhariri wa gazeti hilo anaeleza zaidi kwamba jambo la kutia moyo ni kwamba Waziri wa mambo ya nje wa Marekani John Kerry angeliweza kuijumuisha Iran katika mfungamano wa kupambana na magaidi wa dola la kiislamu. Unyama unaofanywa na magaidi hao umewafanya hata maadui waje pamoja katika lengo la kuwatokomeza magaidi hao.

Ajali ya nyuklia nchini Ukraine

Ajali ndogo kwenye kinu cha nishati ya nyuklia ilitokea hapo jana nchini Ukraine.Na kwa mujibu wa habari za idara husika, ajali hiyo haikusababisha madhara yoyote. Hata hivyo mhariri wa gazeti la "Nürnberger" anasema ajali hiyo inakumbusha maafa yaliyotokea kwenye kinu cha Tschernobyl.

Mhariri huyo anasema mpaka sasa bado vipo vinu vya nyuklia 15 nchini Ukraine vinavyokidhi mahitaji ya nishati kwa kiwango kikubwa. Lakini vinu hivyo vipo tokea enzi za Umoja wa kisoviet . Jambo la kulitilia maanani ni kwamba ajali hiyo imetokea katika mji uliopo karibu na sehemu ambapo waasi wanaotaka kujitenga wanapambana na majeshi ya serikali ya Ukraine.Hiyo ndiyo sababu kwamba Waziri Mkuu wa nchi hiyo Arseny Yatsenyuk alihamanika baada ya kupata habari juu ya jali hiyo.

Haki za wahamiaji nchini Ujerumani.

Gazeti la "Kieler Nachrichten" linazungumzia juu ya haki za wahamiaji nchini Ujerumani. Gazeti hilo linasema wageni ambao wameishi kwa muda mrefu nchini wanastahiki haki ya kupewa kibali cha kuishi nchini baada ya kuwapo kwa muda wa zaidi ya miaka sita .Mradi tu watu hao wanayatimiza masharti yaliyopo, ikiwa pamoja na kuielewa na kuizungumza lugha ya kijerumani.Pia mradi wawe na njia ya kuyakimu maisha yao bila ya kutegemea msaada wa serikali.

Mwandishi:Mtullya Abdu./Deutsche Zeitungen.

Mhariri: Iddi Ssessanga