1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri

29 Januari 2007

Wananchi wa Marekani sasa wameanza kumhinikiza Rais George Bush juu ya vita vya nchini Irak wakimtaka rais huyo andoe majeshi mara moja. Katika maoni yao leo wahariri wa magazeti ya hapa nchini pia wanazungumzia juu ya hatua ya serikali kufunga migodi ya makaa.

https://p.dw.com/p/CHTs

Gazeti la MANNHEIMER MORGEN linasema juu ya maandamano yaliyofanywa mjini Washington kuhusu kumtaka rais George Bush aondoe majeshi ya Marekani kutoka Irak kwamba idadi ya wananchi wa Marekani wanaotaka kukomeshwa vita vya Irak bado ni ndogo lakini, anasisitiza mhariri huyo hatua ya kufanyika maandamano hayo mjini Washington ni muhimu sana. Gazeti hilo linatilia maanani kwamba wawakilishi wa utawala wa bwana Bush pamoja na wabunge hawana tena muda wa kutosha katika kutayarisha mkakati wa kuzuia kuondolewa majeshi ya Marekanai haraka sambamba na kuleta utengemavu nchini Irak.

Mhariri anasema ikiwa utawala wa bwana Bush utashindwa kuonesha mafanikio ya haraka,idadi ya wapinzani wa vita hakika itaongezeka na kusababisha kimbunga cha kisiasa.

Naye mhariri wa gazeti la mjini Bonn GENERAL-ANZEIGER anatabiri kuwa mjumbe yeyote wa chama cha Demokratik atakaesimama kidete kupinga vita vya nchini Irak, atakuwa na uwezekano mkubwa wa kushinda katika uchaguzi wa rais mwaka ujao. Mhariri huyo pia anatilia maanani kuwa hadi sasa idadi ya wananchi wa Marekani wanaotaka kurejeshwa nyumbani majeshi ya nchi yao bado ni ndogo. Lakini upinzani wa watu hao wachache unaweza kugeuka tashi la kisiasa lisiloweza kuepeka asilani!

Mhariri wa gazeti hilo, GENERAL ANZEIGER anatabiri kuwa mwaka huu wa tano ambapo majeshi ya Marekani yanapigana nchini Irak hautamalizika bila ya baadhi ya vikosi kuanza kuondolewa.

Akisisitiza juu ya hinikizo la wananchi wa Marekani kumtaka bwana Bush amalize vita nchini Irak, mhariri wa gazeti la ABENDZEITUNG la mjini Munic anasema kuwa kampeni za kupinga vita hivyo siyo jambo jipya asilani nchini Marekani , lakini mhariri anahoji kuwa kampeni hiyo imeingia katika upeo wa juu zaidi. Wahusika katika Ikulu wanahofia kuwa idadi ya wapinzani wa vita hivyo inaweza kufikia nusu milioni mnamo miezi michache ijayo.

Jambo jingine la kutilia maanani , anasema mhariri huyo ni kwamba , kwa mara ya kwanza idadi kubwa ya wanasiasa wanawaunga mkono wapinzani wa vita.

Aidha, kwa mara ya kwanza , rais Bush anakabiliwa na bunge lenye idadi kubwa ya wajumbe wa chama cha Demokratik.

Bunge hilo sasa linapaswa kuchukua hatua katika kumshinikiza rais Bush.

Rais huyo hawezi kupuuza upinzani wa wananchi.

Gazeti hilo la ABENDZEITUNG la mjini Munic limemkariri mjumbe mmoja wa chama cha Demokratik John Conyers akisema kuwa rais Bush anaweza kuwafukuza kazi majerali wake, au mawaziri wake lakini hawezi kuwafukuza kazi wananchi wa wanaposema kuwa Marekani imeshindwa nchini Irak.

Wahariri wa magazeti pia wanazungumzia juu ya kufungwa kwa migodi ya makaa ya mawe nchini Ujerumani.

Juu ya hayo mhariri wa gazeti la MÄRKISCHE ALLGEMEINE kutoka mjini Potsdam anakumbusha kuwa, kwa dahari za miaka serikali kuu na za mitaa zimekuwa zinatoa fedha zinazotokana na kodi ili kufidia uzalishaji makaa nchini , japo ni kiasi kidogo tu cha fedha kingeliweza kutumika katika kuagiza makaa hayo kutoka nje.

kipingamizi .

Hadi kufikia mwaka wa 2018 uzalishaji utafikia mwisho chini ya msingi wa programu itakayoleta manufaa kwa wahusika wote. wanachama wa a SPD hawakubaliani na uamuzi huo. Mhariri anasema hakuna sababu ya kuendelea kutoa ruzuku ili kufidia uzalishaji wa makaa hapa nchini.Anasema kuwa fedha hizo ni bora zingetumika kwa ajili ya kuzalisha nishati mbadala.

Mhariri wa gazeti la FINANCIAL TIMES la Ujerumani anaafikiana na hoja hiyo kwa kusema kwamba sekta ya uzalishaji makaa imekuwa inamiminiwa mabilioni ya fedha kama ruzuku. Sasa sekta hiyo imepewa muda wa kukata roho kiungwana na kwamba inatayarishiwa maziko ya daraja la mbele. Lakini,mhariri anasema haitafaa , kuifanya sekta hiyo iwe na uhai wa milele.

Kufanya hivyo hakutakuwa uwajibikaji.

Abdu Mtullya