1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wahariri wazungumzia juu ya elimu.

Mtullya, Abdu Said10 Septemba 2008

Wahariri wa magazeti walalamika juu ya kiwango cha elimu nchini Ujermani.

https://p.dw.com/p/FFPB
Kansela Angela Merkel wa Ujerumani akitembelea chuo cha mafunzo mjini Berlin.Picha: AP



Katika maoni  yao wahariri  wa  magazeti ya   Ujerumani leo  wanazungumzia juu ya ripoti kuhusu   kiwango cha elimu nchini Ujerumani iliyotolewa na  shirika la ushirikiano wa kiuchumi  na maendelo OECD.

Gazeti la  Aachener  Nachrichten linasema mfumo  wa  elimu wa Ujerumani  unakabiliwa  na matatizo kwa sababu ya  muundo  wa shirikisho.Ujerumani ina majimbo  16 na kila  jimbo  lina  utaratibu wake wa elimu.

Hatahivyo  gazeti linasema  dawa ni moja tu-  kuongeza  bajeti ya sekta hiyo.

Na mhariri  wa gazeti  la Honnoversche Allgemeine analalamika  kwamba kinachofanyika  sasa  hakitoshi katika kurekebisha hali ya elimu nchini Ujerumani.

Mhariri huyo anasema jambo  baya zaidi kwa  Ujerumani  ni, kwamba wasomi wanatoeka nchini.

Gazeti linasema  habari hizo ni za kushtusha kwa  wote  wanaoitakia mema Ujerumani, kwani nchi  isiyokuwa na watu wenye ujuzi asilani haitaweza kushindana na nchi zingine  duniani.


Gazeti la Südwest Presse  pia limetathmini ripoti  ya   shirika  la ushirikiano wa kiuchumi  na maendeleo OECD,  juu ya  kiwango  cha elimu nchini Ujerumani.

Gazeti hilo linasema , ripoti hiyo inaonesha kuwa   kwa mara nyingine Ujerumani  imeanguka katika  mtihani wa elimu. Gazeti  limekariri ripoti iliyotolewa   hivi karibuni inayoonesha kuwa  Ujerumani ipo nyuma  katika kutoa  fursa  za kujiendeleza kwa  watu wenye elimu  ya chini kulinganisha na nchi zingine  za Umoja wa Ulaya.

Mhariri wa  gazeti Südwest Presse anasema suluhisho ni  kuongeza fedha kwa ajili ya elimu.