1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Magazetini.

Mtullya, Abdu Said16 Septemba 2008

Wahariri wa magazeti ya Ujerumani leo wanatoa maoni yao juu ya mgogoro mwingine wa fedha uliosababishwa na benki ya vitega uchumi, Lehmann Brothers ya nchini Marekani.

https://p.dw.com/p/FJ9t
Soko la hisa la New York muda mfupi baada ya hisa kuanguka kutokana na mgogoro wa Lehmann Brothers.Picha: AP

Katika  maoni  yao leo wahariri  wa magazeti ya Ujerumani wanazungumzia juu ya mgogoro mwingine wa  fedha uliosababishwa  na benki ya vitega uchumi, Lehmann  Brothers nchini Marekani.


Lakini  wahariri hao pia  wanazungumzia juu ya   makubaliano ya kugawana mamlaka yaliyofikiwa  baina ya rais Robert Mugabe na mpinzani wake mkuu Morgan Tsvangirai nchini  Zimbabwe. Gazeti la Passauer Neue Presse linasema  makubaliano hayo  maana yake ni mwisho wa  damu kumwagika nchini  Zimbabwe.


Kuhusu mgogoro  mwingine  wa  fedha uliosababishwa na benki ya vitega uchumi  Lehmann Brothers ya Marekani gazeti la Berliner Zeitung linaonya  dhidi ya  serikali kuingilia kati na kujaribu kuyasaidia  mabenki ama mashirika ya fedha  yanayokabiliwa na matatizo.

Mhariri wa gazeti la Berliner Zeitung anakumbusha  historia ndefu ya benki ya Lehman Brothers,  iliyoweza kuhimili misukosuko ya vita kuu mbili,na mgogoro wa uchumi wa miaka ya 30. Lakini licha ya kuweza kuhimili misukosuko hiyo mikubwa katika historia yake ndefu,  benki hiyo ,huenda ikatoeka. Mhariri anasema  waliokuwa wanafikiria kuisaidia benki hiyo  sasa wametambua kwamba msaada wa serikali  usingelikuwa  na manufaa.


Mhariri wa gazeti la Der neue  Tag anaunga  mkono  maoni ya gazeti la Berliner Zeitung kwa kukariri  usemi unaosema kuwa hakuna mwenye ukubwa  wa kuweza kuhimili misukosuko yote.

Mhariri wa gazeti hilo anaeleza kuwa sasa umefika wakati wa kuachana kabisa na tabia ya  kibinafsisha  mapato makubwa  yanayotokana na biashara za mashaka,  lakini wakati huo huo kutumia fedha za  walipa kodi kufidia hasara zinapotokea.


Mhariri wa gazeti la Nordsee  anasema ,mzigo siku  zote unabebwa na wateja, wadogo wadogo,  pamoja  na walipakodi.

Gazeti linafafanua kwa kusema kwamba walipa kodi  na wateja wenye akaunti katika benki  wanabeba  mizigo inayotakana na  migogoro ya fedha kwa sababu , mabenki na mashirika  yote ya fedha  yameungana katika mtandao kutokana  na  mfumo  wa dunia utandawazi. Gazeti  linasema kutokana na  mfumo huo, watu wote wanaathirika. Gazeti linasema hayo yataonekana katika siku za usoni  baada ya akaunti za watu kuteketea.

Lakini mhariri wa  gazeti la Fränkischer Tag anasema  hakuna haja ya kuwa na kiherehere  nchini  Ujerumani.

Gazeti linasema mfumo wa fedha wa Ujerumani  ni imara sana, na kwa hiyo hakuna  haja ya mtu kuwa na wasiwasi.