1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Magazetini.

Mtullya, Abdu Said23 Septemba 2008

Magazeti ya Ujerumani leo yanazungumzia juu ya watalii waliotekwa nyara nchini Misri.

https://p.dw.com/p/FNOT
Wanaposhikiliwa watalii wa kijerumani.

Mkasa wa kutekwa nyara watalii wa kijerumani nchini Misri ni pamoja na masuala yanayozingatiwa na wahariri wa magazeti katika maoni yao leo.

Magazeti hayo pia yanazungumzia juu ya mgogoro wa fedha nchini Marekani na juu ya kashfa ya maziwa ya sumu, kutoka China.

Watalii kutoka Italia, Romania,wamisri wanane na watalii watano kutoka Ujerumani bado wamo mnamo mikono ya wateka nyara nchini Misri.Juu ya hayo mhariri wa gazeti la Heilbronner anaeleza ,kuwa Misri ni nchi yenye utamaduni wa karne nyingi unaowavutia watalii kutoka kote duniani. Lakini anasema pale ambapo utalii unastawi, panashtadi pia hatari ya watalii kutekwa nyara kwa sababu mbalimbali.

Gazeti la Südkurier linasema , aghlabu wanachotaka wahalifu hao ni fedha tu ,kama jinsi dunia inavyoshuhudia kwenye upembe wa Afrika.Na kutokana na hayo mhariri wa gazeti la Südkurier anaeleza kuwa ni muhimu kwa watalii kutambua kwamba usalama wao hauhatarishwi na magaidi tu.Anasema imethibitika mara nyingi kwamba wateka nyara wanalenga shabaha za kujipatia fedha.

Masoko ya fedha ya Marekani kwa mara nyingine yanakabiliwa na mgogoro mkubwa .Na utawala wa Bush unatayarisha mpango kamambe wa dola bilioni 700 ili kuyasaidia masoko hayo. Jee itakuwa sawa kwa nchi zingine nazo ,kama Ujerumani kusaidia?Gazeti la Mitteldeutsche linatilia maanani kwamba Ujerumani na nchi zingine za kundi la G 8 hazikuonesha uchangamfu kwa waziri wa fedha wa Marekani Henry Paulson. Lakini ,gazeti linasema msimamo huo ni sahihi kabisa, linauliza kwa nini nchi zingine zishiriki kwa kutoa mabilioni ya fedha, ambayo hatimaye yataingia katika mabenki ya Marekani? Mhariri wa Mitteldeutsche anasema kila mtu ana dhamira ya kusaidia ili uchumi wa Marekani uwe imara tena, lakini katika dhamira hiyo pia, pana mipaka.

Juu ya kashfa ya maziwa nchini China,gazeti la Mannheimer Morgen linasema wakomunisti wa China wapo tayari kutambuka maiti ili kufikia shabaha zao. Gazeti linasema serikali ya China ilijua kabla ya mashindano ya Olimpiki juu ya kuwepo maziwa yenye sumu, lakini iliendelea na propaganda za kutangaza michezo hiyo, badala ya kuchukua hatua.