Hali ya nchini Iran.
25 Juni 2009
Mwanasiasa wa upinzani Mehdi
Karroubi aliegombea urais na
kushindwa nchini Iran ameahirisha
mpango wa kuomboleza vifo vya watu
wapatao 17 waliouawa kufuatia
maandamano ya kupinga matokeo ya
uchaguzi.
Wakati huo huo mvutano wa kugombea mamlaka unaendelea ndani ya uongozi wa Iran.
Mwanasiasa huyo wa upinzani aliekuwa miongoni mwa wagombea watatu walioshindwa katika uchaguzi wa rais amesema ameahirisha mpango wa kuomboleza vifo vya watu hao 17 kwa sababu hajapata mahala la kufanyia maombolezo hayo. Hatahivyo amesema katika tovuti kwamba atafanya maombolezo hayo wiki ijayo.
Wizara ya mambo ya ndani ya Iran imepiga marufuku mikutano ya makundi na jumuiya zote ambazo zimekuwa zinafanya maandamano kupinga wanachoita udanganyifu katika matokea ya uchaguzi.
Katika uchaguzi huo, rais wa hadi sasa Mahmoud Ahmadinejad alitangazwa kuwa mshindi na alisherehekea ushindi huo hapo jana lakini vyombo vya habari vya Iran vimeripoti kuwa idadi kubwa ya wabunge waliisusia ghafla hiyo.
Habari zinasema wabunge wote 290 walialikwa lakini 105 hawakuhudhuria. Wachunguzi wanasema hatua ya wabunge hao kukataa kwenda kwenye sherehe za ushindi wa rais Mahmoud Ahmadinejad inadhihirisha mvutano wa kugombea mamlaka ndani ya uongozi wa Iran.
Wakati huo huo tamko lilitolewa kwenye mtandao na mpinzani mkuu bwana Mir Hossein Mousavi limeeleza kuwa wasomi na wawakilishi wa vyuo vikuu wapatao 70 wametiwa ndani.
Wakati mvutano wa kugombea mamlaka unaendelea kushtadi nchini Iran habari zaidi zinasema kuwa kiongozi mkuu wa upinzani bwana Mousavi anashinikizwa ili aache msimamo wake wa kutaka kubatilishwa kwa matokeo ya uchaguzi.Lakini mwanasiasa huyo amesema mapambano yataendelea.
Mwandishi:Fahimeh Farsie/DW Persisch/A.Mtullya
Mhariri:M.Abdul-Rahman