1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hali ya nchini Iran.

Abdu Said Mtullya25 Juni 2009

Mousavi asema mapambano yataendelea.

https://p.dw.com/p/Iays
Wapinzani wataka uchaguzi wa rais ufanyike tena nchini Iran.Picha: AP


Mwanasiasa  wa upinzani Mehdi Karroubi aliegombea  urais na kushindwa  nchini  Iran  ameahirisha mpango wa kuomboleza  vifo vya  watu wapatao   17  waliouawa  kufuatia maandamano  ya  kupinga  matokeo  ya uchaguzi.

Wakati  huo huo mvutano  wa kugombea mamlaka  unaendelea  ndani  ya uongozi  wa  Iran.

Mwanasiasa  huyo  wa   upinzani aliekuwa  miongoni  mwa  wagombea watatu  walioshindwa  katika  uchaguzi wa rais  amesema  ameahirisha mpango wa  kuomboleza vifo vya  watu  hao 17 kwa  sababu  hajapata  mahala  la kufanyia maombolezo  hayo. Hatahivyo amesema  katika tovuti  kwamba atafanya   maombolezo hayo  wiki ijayo.

Wizara  ya  mambo  ya   ndani ya Iran imepiga  marufuku  mikutano  ya makundi  na  jumuiya  zote  ambazo zimekuwa  zinafanya  maandamano kupinga  wanachoita  udanganyifu katika matokea  ya uchaguzi.

Katika uchaguzi  huo,  rais  wa hadi sasa  Mahmoud  Ahmadinejad alitangazwa kuwa mshindi  na alisherehekea  ushindi  huo  hapo  jana lakini  vyombo  vya habari  vya  Iran vimeripoti kuwa  idadi  kubwa  ya wabunge  waliisusia  ghafla  hiyo.

Habari  zinasema  wabunge  wote  290 walialikwa  lakini  105  hawakuhudhuria. Wachunguzi  wanasema  hatua ya wabunge hao  kukataa kwenda kwenye sherehe  za ushindi  wa  rais  Mahmoud Ahmadinejad  inadhihirisha  mvutano wa kugombea  mamlaka  ndani  ya  uongozi wa Iran.

Wakati huo huo tamko lilitolewa kwenye mtandao  na mpinzani  mkuu  bwana Mir Hossein Mousavi  limeeleza  kuwa wasomi  na  wawakilishi  wa vyuo vikuu wapatao  70 wametiwa  ndani.

Wakati  mvutano wa  kugombea mamlaka unaendelea  kushtadi  nchini Iran  habari zaidi zinasema kuwa kiongozi mkuu  wa  upinzani  bwana Mousavi anashinikizwa  ili aache msimamo wake  wa kutaka kubatilishwa kwa matokeo ya  uchaguzi.Lakini mwanasiasa  huyo  amesema mapambano  yataendelea.


Mwandishi:Fahimeh Farsie/DW Persisch/A.Mtullya

Mhariri:M.Abdul-Rahman