1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mapigano ya kuuania mji wa Misrata yanapamba moto

9 Mei 2011

Mapigano yameripuka karibu na Misrata-mji wa magharibi ya Libya unaodhibitiwa na waasi na kuzingirwa na vikosi vya serikali katika wakati ambapo waasi wanasubiri silaha kutoka Italy.

https://p.dw.com/p/11C4O
Moshi unafuka toka mji unaozingirwa wa MisrataPicha: AP

Kwa amujibu wa ripota wa shirika la habari la Ufaransa-AFP mapigano yamepamba moto katika maeneo matatu yanayouzunguka mji wa mwambao wa Misrata,umbali wa kilomita 200 mashariki ya mji mkuu Tripoli;Shintah upande wa mashariki,katika njia inayoelekea uwanja wa ndege ambayo inakutikana kusini na Bourgueya-upande wa magharibi.

Waasi wanasema wameimarisha ulinzi katika mji wa Bourgueya na mapigano yametuwama katika eneo la uwanja wa ndege."Tunajiandaa kusonga mbele na kuuteka uwanja wa ndege-jambo linaloweza kutokea wakati wowote kutoka sasa" amesema mkuu wa opereshini za kijeshi za waasi Omar Salem.

Mwenzake Ahmad Bassen ameongeza kusema wapiganaji wao wameshawekwa uwanja wa ndege na ghala za silaha zinakutikana kilomita tano tu kutoka hapo.Amesema wanataka jumuia ya kujihami ya NATO iziripue ghala hizo.

Frankreich Luftwaffe Kampfjet Dassault Rafale über Libyen
Ndege ya kijeshi ya Ufaransa Rafale katika anga ya LibyaPicha: AP

Bandarini visima vya mafuta vinaendelea kufuka moto baada ya hujuma za mabomu za jumamosi iliyopita.

Milolongo ya watu wanapiga foleni katika vituo vya mafuta wakihofia uhaba wa mafuta.

Vikosi tiifu kwa Gaddafi" vimevunja visima vilivyokuwa vimejaa" amesema mwanaharakati mmoja wa upande wa upinzani Ahmed Montasser.

"Ikiwa mashambulio kama haya yataendelea katika eneo la bandarini,tunaweza kukumbwa na shida ya kujipatia maji na chakula"-amesema kwa upande wake,msemaji wa waasi Saddoun al Misrati akiwa mjini Benghazi.Meli moja tuu ya misaada ya kiutu inatia nanga kwa wiki katika mji huo wa Misrata tangu hujuma kuanza bandarini,wiki mbili zilizopita.

Naibu mwenyekiti wa baraza la taifa la mpito-taasisi ya waasi yenye makao yake makuu mjini Benghazi-Abdel Hafiz Ghoga amesema wanasubiri silaha kutoka Italy.

NATO-Generalsekretär Rasmussen
Katibu mkuu wa jumuia ya kujihami ya NATO,Anders Fogh RasmussenPicha: AP

Na katibu mkuu wa jumuia ya kujihami ya NATO Anders Fogh Rasmussen amesema "Gaddafi hana tena njia"."Enzi zake zinakurubia kumalizika na anazidi kutengwa"amesema Rasmussens na kuongeza hata hivyo,mgogoro wa Libya unabidi ufumbuliwe kwa njia ya kisiasa na sio ya kijeshi.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir

Mhariri:Abdul-Rahman