1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mapigano yasababisha vifo Sudan

10 Januari 2011

Zaidi ya watu 20 wameuawa kufuatia mapigano yaliyozuka kati ya makabila mawili yanayopingana katika mkoa ulio na mvutano wa Abyei. Mapigano hayo yametokea wakati zoezi la kura ya maoni likiendelea Sudan ya kusini.

https://p.dw.com/p/zvvJ
Zaidi ya polisi 20 wauawa katika mapigano AbyeiPicha: picture-alliance /dpa

Msemaji wa jeshi la Sudan ya kusini SPLA Philip Aguer amesema zaidi ya polisi 20 na vijana wameuawa katika eneo hilo, kufuatia mapigano kati ya Wasudan ya kaskazini wenye asili ya kiarabu wa kabila la Misseriya na kabila la Ngok Dinka la Sudan ya kusini, ambao ndio wenyeji katika eneo hilo la mpakani lenye utajiri wa mafuta.

Usalama mdogo

Kwa upande wake, mkuu wa utawala katika mkoa huo wa Abyei Deng Arop Kuol amelalamikia kutokuwepo na usalama katika eneo hilo sasa, kwani hawafahamu kama ni majeshi ya serikali, wanamgambo ama watu wa kabila hilo la Misseriya ndio wamekuwa wakiwashambulia, na kuonya kwamba wamekuwa wakiandaa shambulio lingine.

Bundeswehr Fortsetzung der Beteiligung deutscher Streitkraefte an der Friedensmission der Vereinten Nationen im Sudan
Walinda amani wa Umoja wa Mataifa nchini SudanPicha: AP

Kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Mataifa, kimetumwa katika eneo hilo kwa ajili ya kuchunguza chanzo cha mapigano hayo.

Hali ya wasiwasi imekuwa ikiongezeka katika wilaya hiyo ya Abyei iliyoko mpakani mwa Sudan ya kusini na kaskazini, katika wakati huu zoezi la kura ya maoni likiwa linaendelea.

Bado kumekuwa na mvutano juu ya eneo hilo la Abyei kubakia Sudan ya kaskazini ama kujiunga na taifa la Sudan ya kusini, iwapo kura ya maoni itaonesha hivyo.

Katika taarifa yao ya pamoja waliyoitoa jana, kupongeza siku ya kwanza ya upigaji kura, Uingereza, Norway na Marekani, ambao ni washirika wakubwa kutoka nchi za magharibi katika mazungumzo ya kutafuta amani Sudan ya kusini na kaskazini, walielezea wasiwasi wao juu ya hali ilivyo katika wilaya hiyo ya Abyei.

Kiir aongoza zoezi la upigaji kura

Referendum Südsudan
Rais wa Sudan ya kusini Salva KiirPicha: AP

Wakati hali ikiwa ya wasiwasi katika eneo la mpaka wa Sudan ya kusini na kaskazini, zoezi la upigaji kura ya maoni, ambalo hii leo limeingia siku yake ya pili limeelezewa kuendelea vizuri, kwa watu wengi kujitokeza kushinda vile ilivyotarajiwa, huku rais wa eneo hilo Salva Kiir akiwahimiza watu waliokosa nafasi, kutokata tamaa, kwani bado siku zipo kuweza kushiriki zoezi hilo:

"Napenda kutoa wito kwa watu wote wa Sudan ya kusini kuwa na subira iwapo mtu hataweza kupata muda wa kupiga kura yake leo..."

Kwa mujibu wa Paulinoo Wanawilla Unango kutoka katika Tume ya kura ya maoni Sudan ya kusini, kwa siku ya jana tu watu waliojitokeza kupiga kura ilikuwa ni asilimia 20 katika eneo huilo la kusini na huku katika majimbo ya kaskazini ikiwa ni asilimia 14.

Mwandishi: Halima Nyanza (dpa, afp)
Mhariri: Josephat Charo