1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Serikali ya mpito yapinduliwa

17 Septemba 2015

Rais wa mpito wa Burkina Faso Michel Kafando amepokonywa wadhifa wake na serikali yake kuvunjwa. Jumuia ya kimataifa imelaani mapinduzi hayo yaliyotokea chini ya mwezi mmoja kabla ya uchaguzi mkuu.

https://p.dw.com/p/1GXpq
Kasri la rais mjini OuagadougouPicha: picture-alliance/dpa/L. Koula

Ripoti za kupokonywa wadhifa wake rais wa mpito Michel Kafando pamoja na kuvunjwa serikali ya waziri mkuu Ishak Zida zimetolewa na mwanajeshi mmoja kupitia televisheni ya nchi hiyo.Mwanajeshi huyo ametangaza pia kuundwa kwa "baraza la taifa kwa ajili ya demokrasia "lililopewa jukumu la kuandaa uchaguzi.

Tangazo hilo limetolewa siku moja baada ya wafuasi wa kikosi maalum cha ulinzi wa rais kuwakamata rais wa mpito,waziri mkuu na mawaziri wawili.

Mamia ya waburkinabe wameteremka majiani mjini Ouagadougou kulaani mapinduzi hayo na kudai rais wa mpito na mawaziri wa serikali waachiwe huru.

Na wanajeshi wameuvamia uwanja wa uhuru,kati kati ya Ouuagadougou wakifyetua risasi kuwatawanya waandamanaji hao.

Milio ya risasi imesikika katika mitaa mengine pia ya mji mkuu.

Jumuia ya kimataifa imelaani matumizi ya nguvu

Mapinduzi haya yanayosemekana kufanywa na kikosi maalum cha ulinzi wa rais RSP-yamejiri chini ya mwezi mmoja kabla ya uchaguzi wa rais na bunge uliopangwa kuitishwa october 11 ijayo uchaguzi ambao wengi wanatarajiwa ungeimarisha mfumo wa kidemokrasi nchini humo.

Burkina Faso Protest gegen die Präsidentengarde in Ouagadougou
Waburkina walioingiwa na hasira wanateremka majiani mjini OuagadougouPicha: Reuters/J. Penney

Ufaransa,mtawala wa zamani wa kikoloni wa Burkina Faso, imesema imeingiwa na wasi wasi kutokana na hali namna ilivyo nchini Burkina faso.Msemaji wa wizara ya mambo ya nchi za nje amesema serikali ya Ufaransa inalaani matumizi ya nguvu na kutoa wito wa kuachiwa huru wale wote wanaoshikiliwa.

Wanajeshi 200 wa kikosi maalum cha Ufaransa wamewekwa katika kituo cha kijeshi mjini Ouagadougou kuambatana na opereshini Barlhane dhidi ya waasi wa itikadi kali nchini Mali.

Umoja wa Ulaya pia umelaani mapinduzi hayo.Mkuu wa siasa ya nje wa Umoja wa Ulaya bibi Federica Mogherini ametoa wito waachiwe huru haraka rais Michel Kafando na maafisa wote wa serikali yake wanaoshikiliwa.

Rais wa zamani Blaise Kompaore anaishi uhamishoni Côte d'Ivoire

Itafaa kusema hapa kwamba kikosi maalum cha ulinzi wa rais RSP ni mojawapo ya mihimili ya utawala wa rais wa zamani wa Burkina faso Blaise Compaore aliyetimuliwa madarakani oktoba mwaka jana na kukimbilia nchi jirani ya Côte d'Ivoire alipotaka kujaribu kubadilisha katiba baada ya miaka 27 madarakani.

Burkina Faso Ex-Präsident Compaore Archiv 2011
Rais wa Zamani wa Burkina Faso Blaise CompaorePicha: picture alliance/AP Photo/R. Blackwell

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/AFP/Reuters/

Mhariri: Gakuba Daniel