1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mapinduzi yafuatia kifo cha Lansana Conte

Oumilkher Hamidou23 Desemba 2008

Muimla wa Guine Conacry aiaga dunia na kuiacha Guine ya Conacry katika hali ya ufukara

https://p.dw.com/p/GLsC
Picha ya mwaka 1998 ya rais wa Guine Conacry Lansana ContePicha: picture-alliance/dpa



Serikali ya Guine,na taasisi zake zimevunjwa huku katiba ikibatilishwa muda mfupi baada ya rais Lansana Conte aliyeitawala nchi hiyo ya Afrika magharibi tangu mwaka 1984 kuiaga dunia.



"Kuanzia leo katiba imesimamishwa pamoja pia na harakati zote za kisiasa na za vyama vya wafanyakazi" amesema kepteni Moussa Dadis Camarra kupitia Radio Conacry.


"Serikali na taasisi zote zimevunjuwa" ameongeza kusema kepteni huyo  aliyetangaza kundwa hivi karibuni "baraza la mashauriano -wakijumuishwa wanajeshi na raia wa kawaida.


"Taasisi za serikali zimeshindwa kuipatia ufumbuzi mizozo inayoikaba nchi hii" amesisitiza kepteni huyo aliyezungumzia juu ya "kuvunjika moyo wananchi " ,umuhimu wa kuupiga jeki uchumi na mapambano dhidi ya rushwa.


Nani wako nyuma ya mapinduzi haya ya kijeshi na dhamiri zao ni zipi hakuna ajuaye bado.Kinachojulikana ni ule ukweli kwamba mapinduzi hayo yamejiri saa sita tuu baada ya  spika wa bunge Aboubakar Sompare kutangaza  kifo cha rais Lansana Conte jana usiku kupitia televisheni ya taifa, aliyekua na umri wa miaka 74. Alikua mgonjwa kwa muda mrefu.


Umoja wa Afrika umesema unafuatilizia kwa makini hali ya mambo nchini Guine.

Kamishna anaeshughulikia masuala ya amani na usalama,Ramtane Lamamra ameliambia shirika la habari la Ufaransa AFP tunanukuu:"Tunamuombea rais aliyeiaga dunia,lakini tunaifuatilizia kwa makini na wasi wasi mkubwa hali namna ilivyo na nani atakabidhiwa nafasi ya rais Conte."Mwisho wa kumnukuu bwana Lamamra aliyewatolea mwito wanasiasa wote na taasisi zote,zikiwemo za kijeshi zidhamini kipindi cha mpito kwa amani na masikilizano na kuheshimu demokrasia.


Utawala wa kimabavu wa miaka 24 wa Lansana Conte umeifilisi moja kwa moja nchi hiyo ya Afrika magharibi,inayotajikana kua miongoni mwa nchi zenye utajiri mkubwa wa mali ghafi barani Afrika.


Mara baada ya tangazo la kifo chake,waziri mkuu Ahmed Tidiane Souare alitoa mwito kupitia televisheni akiwasihi wananchi watulie.


Hakuna fujo zozote zilizoripitiwa hadi sasa.Itafaa kusema hapa kwamba machafuko ya umma yaliyoripuka mapema mwaka jana kulalamika dhidi ya utawala wa Lansana Konte yalivunjwa nguvu na jeshi nas kugharimu maisha ya watu zaidi ya 186.1200 walijeruhiwa.


Mwezi uliopita pia maandamano yalihanikiza katika miji mkuu Conacry na mikoani wananchi wakilalamika dhidi ya ughali wa mafuta na kukatiwa umeme kila wakati.


Kwa mujibu wa shirika linalopigania haki za binaadam Human Rights Watch,watu wasiopungua wanne wameuwawa vikosi vya jeshi vilipoingilia kati na kufyetua risasi.