1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani na India kuwa wandani wa karibu zaidi

25 Novemba 2009

Marekani imefungua ukurasa mpya wa uhusiano na India kwa kuahidi kuishirikisha kwa karibu zaidi katika masuala ya kupambana na ugaidi,nishati mbadala na kuzuwia utapakazaji wa silaha za nuklia.

https://p.dw.com/p/KfO5
Rais Barack Obama na Waziri Mkuu Manmohan Singh wa IndiaPicha: AP

Kauli hizo zimetolewa wakati wa ziara ya Waziri Mkuu wa India Manmohan Singh huko Marekani alipofanya mazungumzo na Rais Barack Obama.Hii ni mara ya kwanza Rais Obama anamkaribisha rasmi kiongozi wa taifa tangu aushike wadhifa huo.Ajenda ya kikao chao hicho ilijikita zaidi katika harakati za kuuimarsha uhusiano wao kiuchumi hasa baada ya biashara ya India kukua kwasababu ya mageuzi makubwa katika sekta hiyo yaliyofanyika mwanzoni mwa miaka ya tisaini.

Rais Barack Obama alizielekeza zaidi juhudi zake kumhakikishia mgeni wake wa kwanza rasmi Waziri Mkuu wa India Manmohan Singh kuwa ataendelea kuuimarisha uhusiano kati ya mataifa yao mawili,''Leo hii tunajitahidi kuutimiza wajibu wetu wa kuuimarisha uhusiano kati ya mataifa yetu mawili.Leo hii tunaufurahia mwelekeo utakaouimarisha ushirikiano wetu na urafiki kati ya watu wetu,''alieleza.

US-Präsident Barack Obama in Indien
Rais Barack Obama na Waziri Mkuu Manmohan Singh wakiwa na wake zaoPicha: AP

Itakumbukwa kuwa Rais Obama amekuwa akikosolewa nchini mwake kwa kuyapa kipa umbele mataifa hasimu wa India yaani China na Pakistan hasa baada ya kuikamilisha ziara yake ya bara la Asia hivi karibuni.Kwa upande wake serikali ya India ililitaraji hilo kwani uhusiano kati ya mataifa yao ulikuwa mzuri tangu wakati wa utawala wa George W Bush.Pindi baada ya karamu ya chakula cha jioni kufunguliwa rasmi, alipopanda jukwaani, Waziri Mkuu wa lndia Manmohan Singh alisisitiza kuwa kuna umuhimu wa kuwa na mbinu mpya za ushirikiano wa kimataifa kwasababu ya changamoto,''Tunahitaji kuwa na mbinu mpya za kuuimarisha ushirikiano wa kimataifa zitakazoweza kupambana na changamoto kubwa zinazojitokeza kwasababu ya nchi kutegemeana.''

Katika hotuba yake ya ufunguzi Rais Obama alisema kuwa India ni mshirika muhimu katika masuala ya usalama kote ulimwenguni na ustawi,''Mafanikio tunayoyasherehekea leo ni hatua muhimu…nafasi ya kujiendeleza ukizizingatia changamoto na mafanikio ya baadaye.Ya kale yamepita…tugange yajayo,'' alisisitiza.

Kwa upande wake Waziri Mkuu wa India Manmohan Singh alimshukuru mwenyeji wake na akamuelezea kuwa mfano kwa watu wa India kwani anawawakilisha wote wanaoiheshimu demokrasia,mchanganyiko wa watu mbalimbali na usawa.

Ajenda ya mazungumzo ya viongozi hao wawili ilijikita katika masuala ya kuuimarisha ushirikiano wa kiuchumi hasa baada ya sekta ya biashara ya India kukua kwasababu ya mageuzi iliyofanyikwa.Kwa mujibu wa takwimu za mwaka uliopita biashara kati ya mataifa hayo mawili inakadiriwa kuongezeka hadi kiasi cha dola bilioni 50 ikilinganishwa na kile cha mwaka 1990 cha bilioni 5.

Viongozi hao waliwaeleza waandishi wa habari kuwa wanajitahidi kuyakamilisha makubaliano ya mwaka 2005 ya kutengeneza nishati ya nuklia ya matumizi ya kawaida.Kwasababu ya hilo India itaweza kuwekeza katika soko la nishati lililo na thamani ya dola bilioni 150.Maelezo kamili ya hatua hiyo bado hayajabainika.

Hata hivyo India bado inatiwa wasiwasi na msimamo wa Marekani na Pakistan inayoilaumu kuwa chanzo cha ghasia zinazosababishwa na wapiganaji wa kiislamu kama lile shambulio lililotokea Mumbai mwaka 2008.Suala jengine linaloisumbua India ni uhusiano unaopewa uzito mkubwa kati ya Marekani na China iliyo hasimu wake wa jadi.Kulingana na afisa wa serikali wa Marekani fikra hizo ni potofu.

Krieg in Afghanistan Flash-Galerie
Wanajeshi wa kigeni walioko AfghanistanPicha: AP

Wakati huohuo Rais Obama anasubiriwa kuutangaza msimamo wake kuhusu suala la kuviongeza vikosi zaidi Afghanistan jambo ambalo huenda likaubadili mtazamo wa washirika wake wakuu wa Jumuiya ya Kujihami ya NATO.Kiongozi huyo wa Marekani aliweka bayana kuwa ana azma ya kupunguza mivutano kati ya India na Pakistan,mataifa yaliyo jirani.Marekani inataraji kuwa Jeshi la Pakistan litauimarisha uwezo wake ili kupambana na wapiganaji wa kiislamu wanaoutishia ustawi wake pamoja na wa nchi jirani ya Afghanistan.

Baada ya mazungumzo yao Rais Obama na Waziri Mkuu Manmohan Singh walisisitiza kuwa wana imani makubaliano ya msingi yatafikiwa katika kikao cha kilele cha mazingira kijacho cha Copenhagen,Denmark. Hata hivyo viongozi hao hawakuonyesha ishara yoyote kuwa wameibadili misimamo yao inayotofautiana kuhusu suala la kupunguza viwango vya gesi za viwanda zinazochangia katika athari za mabadiliko ya hali ya hewa.

Mwandishi:Thelma Mwadzaya/RTRE

Mhariri:Abdul-Rahman