1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yafanya kumbukumbu ya mashambulizi ya Nairobi, Dar

7 Agosti 2023

Marekani leo imefanya kumbukumbu ya miaka 25 tangu balozi zake kushambuliwa na magaidi katika miji ya Dar es Salaam nchini Tanzania na Nairobi nchini Kenya na kusababisha vifo vya mamia ya raia.

https://p.dw.com/p/4UsCR
Iran Abdullah Ahmed Abdullah Al-Qaidas Nummer zwei getötet | Anschlag in Dar es Salaam
Picha: AMR NABIL/AFP

Marekani imesema mashambulizi hayo yaliyofanyika kwa wakati mmoja katika miji ya Dar es Salaam na Nairobi tarehe 7 Agosti 1998 yanaendelea kukumbusha madhila na kuifanya dunia kuchukuwa mwelekeo mpya kuhusu usalama na amani.

"Dunia inapaswa kuendelea kushikamana ili kukabiliana na vitendo vya kigaidi. Usalama wa dunia utaimarika tu iwapo mifumo na sheria zake zitachukuwa sura inayolenga kupiga vita mienendo ya kigaidi," alisema Balozi Michael Bitte wa Marekani aliyeongoza kumbukumbu hizo.

Soma zaidi: Kenya: Waathirika wa mashambulizi ya ubalozi wa Marekani bado kufidiwa

Kundi la kigaidi la al-Qaida liliyafanya mashambulizi hayo yaliyosababisha vifo vya watu 11 wakiwamo Watanzania waliokuwa wakifanya kazi ubalozini hapo.

Vita dhidi ya ugaidi

Tangu wakati huo, Marekani kwa kushirikiana na jumuiya ya kimataifa ilianzisha operesheni kali kukabiliana na makundi ya watu wanaojihusha na vitendo vya kigaidi.

Syrien Ort einer Bombenexplosion in Damaskus
Mashambulizi ya kigaidi nchini Syria.Picha: SYRIAN TV/AFP

Katika miji ya Dar es Salaam na Nairobi, watu kadhaa walitiwa mbaroni katika siku za mwanzo mwanzo na kisha kukabidhiwa kwa Marekani.

Soma zaidi: Miaka 20 baada ya mashambulizi ya pamoja Kenya na Tanzania, Ugaidi bado ni kitisho

Hadi kufikia mwaka 2010 watu watano walihukumiwa kifungo cha maisha jela, huku pia kukiwa na tuhuma nzito za uvunjwaji wa haki za binaadamu vilivyofanywa na vyombo  vya usalama kwenye ukamataji na utesaji wa washukiwa wa ugaidi.

Fidia kwa wahanga

Baadhi ya wale waliokuwepo karibu ya eneo la tukio wakati wa mashambulizi hayo walielezea jinsi maisha yao yalivyoathirika na tukio hilo miaka 25 baadaye.

Megastädte in Afrika |  Dar es Salaam in Tansania
Sehemu ya jiji la Dar es Salaam lilivyo sasa.Picha: Ericky Boniphace/AFP/Getty Images

Shaban Saidi Mtulya, ambaye alimpoteza mwenza wake katika shambulizi hilo, anasema kunatakiwa juhudi za pamoja kukabiliana na vitendo vya kigaidi.

Soma zaidi: Miaka mitano baada ya kuuliwa Osama bin Laden

Mnamo mwezi Aprili 2014 jaji katika mahakama ya Washington DC nchini Marekani alitowa uamuzi kwamba Watanzania na Wamarekani 23 waliowawa au kujeruhiwa katika shambulizi hilo walipaswa kulipwa fidia ya dola za Kimarekani milioni 957.

Karibu waathirika wote wa tukio hilo walilipwa kifuta machozi.

Imetayarishwa na George Njogopa/DW Dar es Salaam