1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tillerson atafuta msaada wa Waarabu kuitenga Iran

Iddi Ssessanga
23 Oktoba 2017

Saudi Arabia na Iraq zimezindua baraza la ushirikiano kwa msaada wa Marekani, katika juhudi za kukabiliana na ushawishi wa Iran katika kanda ya Mashariki ya Kati.

https://p.dw.com/p/2mKo1
Saudi-Arabien Besuch Rex Tillerson bei König Salman
Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Rex Tillerson akikutana Mfalme wa Saudi Arabia, Salma bin Abdul-Aziz mjini Riyadhi Oktoba 22,2017.Picha: picture-alliance/dpa/A. Brandon

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Rex Tillerson amepeleka hoja ya utawala wa Rais Donald Trump kutaka kuitenga na kuidhibiti Iran katika kanda ya Mashariki ya Kati na zaidi ya hapo kwa mataifa mawili ya Ghuba ya Kiarabu kwa kuzishinikiza Saudi Arabia na Iraq kuungana ili kukabiliana na ushawishi wa Iran unaozidi kuongezeka.

Akiwa nchini Saudi Arabia na baadae Qatar, Tillerson alishutumu kile alichokiita tabia ya uovu ya Iran, na kuyahimiza mataifa ya kanda hiyo na kwingineko, hasa Ulaya, kuungana na utawala wa Marekani kusitisha biashara zozote wanazofanya na kikosi maalumu cha jeshi la Iran, cha Ulinzi wa Mapinduzi au Revolutionery Guard. Pia alitaka wapiganaji wa Kiirani na wale wanaoungwa mkono na Iran nchini Iraq, warudi nyumbani, wajumlishwe katika jeshi la Iraq au waondoke nchini humo.

"Wapiganaji hao wanapaswa kurudi nyumbani," alisema Tillerson. Mpiganaji yeyote wa kigeni anapaswa kurudi nyumbani."

Saudi-Arabien Treffen von König Salman mit US-Außenminister Rex Tillerson und irakischer Ministerpräsident Haider Al-Abadi
Waziri Mkuu wa Iraq Haider al-Abadi akiwa katika uzinduzi wa Baraza la Uratibu kati ya Iraq na Saudi Arabia mjini Riyadh, Oktoba 22,2017.Picha: Reuters/Saudi Press Agency

Mjini Riyadh alikohudhuria mkutano wa ufunguzi wa Baraza la Uratibu kati ya Saudi Arabia na Iraq - ambalo ni chombo ambacho maafisa wa Marekani wanaamini kinaweza kuitoa Iraq katika ushawishi wa Iran - Tillerson alimuambia Mfalme wa Saudi Arabia Salman na Waziri Mkuu wa Iraq Haider al - Abadi, kwamba ushirikiano mchanga kati ya mataifa yao unabeba matumaini makubwa kwa ujenzi mpya wa Iraq, baada ya vita mbaya vya kuyakomboa maeneo ya nchi hiyo kutoka mikononi mwa wapiganaji wa kundi la Dola la Kiislamu, na uhuru wake kutoka ushawishi wa kigeni.

''Na nadhani hii inahitaji kukarabati na kujenga tena kilichokuwa uhusiano wa kihistoria kati ya Iraq na majirani zake ya wa Kiarabu, ambao umepotea katika kipindi cha miongo miwili au mitatu kutokana na mgogoro. Na nadhani ushirikiano huu ni muhimu sana kwa watu wa Iraq, Wasunni, Washia na Wakurd. Kwamba sasa wanaweza kutangamana tena na jirani zao Waarabu.''

Mchango wa mataifa ya Ulaya

Tillerson alisema mataifa ya nje ya kanda pia yanaweza kutoa mchango fulani, hasa kwa kuepukana na kikosi cha Ulinzi wa Jamhuri, kinachotoa mchango muhimu katika uchumi wa Iran na kilichojumlishwa kwenye orodha ugaidi mapema mwezi huu.

Alisema kampuni na na nchi zinazofanya biashara na kikosi hicho zinafanya hivyo kwa kujihatarishia zenyewe. Katika mkutano huo Tillerson aliwasifu Mfalme Salman na wairi mkuu Abadi kwa kufungua tena kivuko kikuu cha mpakani na kurejesha safari za moja kwa moja za ndege kati ya Riyadh ba Baghdad wiki iliyopita.

Katar Rex Tillerson und US-Außenminister Mohammed bin Abdulrahman Al Thani
Tillerson akipokelewa na waziri wa mambo ya nje wa Qatar Muhammad bin Abdul-Rahman al-Thani mjini Doha, Oktoba 22,2017.Picha: picture alliance/AP Photo

Mgogoro kati ya Qatar na jirani zake

Baada ya mazungumzo yake mjini Riyadhm Tillerson alielekea mjini Doha, ambako alifanya mazugumzo na waziri mwenzake wa Qatar Muhammad bin Abdul-Rhaman al-Thani. Tillerson amejaribu kufanya upatanishi kati kati ya pande zinazozozana na kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Kuwait lakini mpaka sasa hakujawa na mafanikio. Alirejea wito wake wa kutaka mazungumzo lakini alikiri kuwa hakuna uwezekano mkubwa wa mafanikio.

''Hatuwezi kulazimisha mazungumzo kwa watu ambao hawako tayari kuzungumza. Lakini tutaendelea kufanya kazi kufanikisha majadiliano na miadi. Lakini kama nilivyosema awali, hatuwezi na hatutolaazimisha suluhu kwa yeyote.''

Tillerson alibanisha kuwa nchi pekee inayonufaika na mgogoro huo ni Iran, ambayo kwa sasa ndiyo tegemeo la Qatar mnamo wakati nchi jirani zimefunga mipaka yake ya nchi kavu, angani na baharini na Qatar. Alisema utegemezi huu mpya wa Qatar kwa Iran ndiyo faida ya hivi sasa na ya wazi zaidi iliyonayo Iran.

Mwandishi: Iddi Ssessanga/AFPE, APE, DPAE.

Mhariri: Grace Patricia Kabogo