1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yatumia dola billioni 1 kuwapa silaha zaidi Wakurdi

31 Mei 2017

Wakati Marekani ikipambana na mgogoro wa Syria, kumezuka hali ya wasiwasi kuwa huenda hali ikawa kama ile ya Iraq, ambapo hadi sasa dola bilioni 1 zimetumika kwa silaha za wapiganaji wa ndani.

https://p.dw.com/p/2duwg
Syrien Rebellen bei Al-Bab
Picha: Reuters/K. Ashawi

 

Silaha, mafunzo na mashambulizi ya anga yamewaongezea nguvu majeshi ya Iraq, wapiginaji wa Kikurdi wa nchi hiyo wa wale wa Syria katika kudhibiti tena eneo la kiliomita 55,000 za mraba kutoka kwa kundi lenye itikadi kali lijiitalo Dola la Kiislamu (IS) katika kipindi cha mapigano ya miaka mitatu.

Uamuzi wa serikali ya Rais Donald Trump wa Marekani kuwapa Wakurdi wa Syria silaha zaidi umezusha wasiwasi miongoni mwa washiriki wanaopigana vita nchini Syria.

Maafisa wa Marekani wamesema  silaha hizo mpya zitakazotolewa ni pamoja na bunduki, mabomu na pengine makombora yanayoweza kukabiliana na vifaru vya kivita.

Msemaji wa muungano wa majeshi yanayoongozwa na Marekani, Kanali John Dorrian, amesema silaha hizo hazitakiwi kurudishwa baada ya matumizi yake kumalizika nchini Syria, lakini ameongezea kusema kuwa Marekani itafuatilia kwa umakini jinsi gani na wapi zitatumika baada ya kukamilisha lengo lake.

"Tunahisabu kila silaha tutakayoitoa, na Marekani itahakikisha kuwa silaha hizo zinatumika katika kupambana na kundi la IS, " alisema msemaji huyo.

Amnesty International waonesha wasiwasi

Deutschland PK Amnesty International Report 2016/2017
Ripoti ya shirika la Amnesty International yaonesha mapungufu makubwa kwa mpango wa Marekani kuwasaidia wapiganaji wa Kikurdi wanaopambana na kundi lijiitalo Dola la Kiislamu (IS).Picha: DW/N. Jolkver

Shirika la haki za binadamu la Amnesty International limetoa ripoti inayoonesha kuwa Marekani imetumia dola bilioni 1 kwa ajili ya  silaha watakazopewa wanajeshi wa Iraq ili zitumike katika kupambana na IS. "Makamanda wa Iraq lazima wasaini kuwa wamepokea silaha zote na Marekani itaendelea kuwasimamia kwa matumizi ya siku zijazo," linadai shirika hilo.

Wakati huo huo, gazeti la Ujerumani la Der Spiegel limeripoti kuwepo kwa mateso, ubakaji na mauaji kwa wale wanaofikiriwa kuwemo katika kundi la IS katika mikono ya kitengo cha wizara ya mambo ya ndani ya Iraq ambayo inajishuhulisha na utoaji usaidizi wa dharura.

Wanajeshi wa Iraq, vikosi vya Kikurdi na polisi wote wanatuhumiwa kuvunja sheria za mahabusu kwa wafungwa vijana na wanaume watu wazima waliowakamata.

Sheria ya Marekani ya haki za binaadamu inakataza idara ya ulinzi kusaidia majeshi ya nje ambayo hayaheshimu haki za binaadamu.

Kundi la kijeshi la kaskazini mwa Iraq linalojulikana kama PESHMERGA linaendelea kupata msaada kwa muda mrefu sasa kutoka muungano wa kijeshi wa Marekani. Misaada hiyo ni pamoja na mafunzo, silaha na mashambulizi ya anga.

Lakini wapiganaji wake wanashutumiwa kufanya uharibifu kwa Waarabu na kuwalazimisha kutoka majumbani mwao katika maeneo ambayo wameyachukuwa kutoka kwa IS.

Shirika la habari la AP limetembelea kijiji kimoja nje ya Kirkuk ambako wakaazi wa Kiarabu wanasema majeshi ya Kikurdi yameziandika nyumba zao "zimekamatwa", wamenyang'anywa  vitambulisho na kufanya uharibu kijijini hapo, madai yanayokanushwa na serikali ya ndani ya jimbo la Kurdistan.

Mwandishi: Najma Said/AP

Mhariri: Saumu Yusuf