1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yawasilisha pendekezo la kuwekewa vikwazo vya kusafiri kwa Rais Mugabe.

Nyanza, Halima4 Julai 2008

Marekani inaushinikiza Umoja wa Mataifa kumuwekea vikwazo vya kusafiri na Rais Robert Mugabe pamoja na maafisa wake 12, na kuzuia mali zao, kutokana shutuma zinazotolewa kupinga duru ya pili vya uchaguzi nchini mwake.

https://p.dw.com/p/EWIF
Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, Zalmay Khalilzad, awasilisha pendekezo la vikwazo vya kusafiri dhidi ya Rais Mugabe.Picha: AP

Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, Zalmay Khalilzad amewasilisha rasmi muswada wa pendekezo la vikwazo hivyo ikiwemo vya silaha kwa utawala huo wa Zimbabwe na kuongezea kuwa ana matumaini kwamba wajumbe 15 wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, watapigia kura muswada huo, wiki ijayo ili nchi hiyo iwekewe vikwazo hivyo.

Pendekezo hilo pia linataka serikali ya Rais Mugabe, kuanza mara moja mazungumzo na vyama vingine kwa lengo la kufikia amani.

Aidha balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa, amesema pendekezo hilo la vikwazo pia, linawalenga wale wote wenye kuwajibika na mzozo wa kisiasa nchini humo.

China ya pendekezo hilo la Marekani, Rais Mugabe, Waziri wa Sheria wa nchi hiyo, Patrick Chinamasa na maafisa wengine 12 wa serikali ya nchi hiyo, kutokana na nafasi zao ni walengwa wa vikwazo hivyo, kutokana na kudaiwa kuchochea ghasia dhidi ya upinzani, ikiwemo uvunjaji wa haki za binadamu na ukandamizaji wa demokrasia.

Idadi ya viongozi hao wanaotakiwa kuwekewa vikwazo hivyo imeongezeka jana, baada ya kujumuishwa pia Waziri wa Ulinzi wa nchi hiyo Sydney Sekeramayi na Waziri wa Kilimo Joseph Made.

Muswada huo pia unashutumu uamuzi wa serikali ya Zimbabwe kuendelea na uchaguzi wa mgombea mmoja na kampeni za ghasia dhidi ya viongozi wa upinzani, hali ambayo imedaiwa kusababisha idadi kubwa ya vifo, maelfu ya majeruhi na kusababisha kufanyika kwa uchaguzi usio huru na wa haki.

Kiongozi wa Upinzani nchini Morgan Tsvangirai aliyemzidi kwa kura Rais Mugábe katika uchaguzi wa Rais March 29, lakini hakuweza kufikisha asilimia inayotakiwa kikatiba kumuwezesha kutangazwa mshindi, hali iliyopelekea kurudiwa tena kwa uchaguzi huo wiki iliyopita, lakini hata hivyo kiongozi huyo wa upinzani alijitoa kwa madai kwamba wafuasi wake wapatao 90 waliuawa, na maelfu kujeruhiwa katika ghasia ambazo anatupia lawama mgambo wanaomuunga mkono Rais Mugabe.

Aidha kiongozi huyo wa chama cha upinzani cha Movement for Democratic Change MDC, alisema yuko tayari kwa mazungumzo, lakini kwa masharti ya kutomtambua Rais Mugabe kama kiongozi aliyechaguliwa katika duru hiyo ya pili ya uchaguzi na kusisitiza kuwa majadiliano hayo yajikite zaidi duru ya kwanza ya uchaguzi.

Kwa upande wa Rais Mugabe alisema wao nao wako tayari kwa mazungumzo ili kumaliza mzozo huo wa kisiasa iliokumba nchi hiyo.

Muswada uliowasilishwa na Balozi wa Marekani unapendekeza pia, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon kuchagua mwakilishi wake maalum, kumwakilisha katika mazungumzo ya vyama hivyo ambapo duru za kidiplomasia zinaonesha kuwa aliyekuwa Katibu Mkuu wa zamani wa Umoja wa Mataifa Koffi Annan ambaye alishiriki kukomesha mzozo wa Kenya na hatimaye kupatikana suluhu.

Wengine wanaotegemewa ni Rais wa zamani wa Msumbiji Joaquim Chissano, Rais wa zamani wa Nigeria Olusegun Obasanjo ama Rais wa Ghana John Kufuor.