1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Martti Ahtisaari mshindi wa tuzo la amani la Nobel la mwaka 2008

Kalyango Siraj10 Oktoba 2008

Aliwahi kukaa Tanzania kwa miaka mitano

https://p.dw.com/p/FXrX
Martti AhtisaariPicha: AP

Rais wa zamani wa Finland Martti Ahtisari ametunukiwa tuzo la mwaka huu la Nobel kutokan na juhudi zake za kutafuta amani barani Afrika, mashariki ya Kati,Ulaya,pamoja na Asia. Lakini Ahtisaari ni nani?

Huu hapa wasifa wake.

Martti Ahtasaari mwenye umri wa miaka 71 aliwahi kuliongoza taifa la Finalnd kuanzaia mwaka wa 1994 hadi 2000.Alizaliwa Juni 23 mwaka wa 1937 katika kijiji cha Viipuri ambacho sasa kinaitwa Vyborg kikipatikana katika nchi ya Urusi.

Babu zake walihamia Finland kutoka Norway ya kusini wakati huo na hatimae Ahtisaari kuchukua uraia wa Finland mwaka wa 1929.

Babake anaitwa Oiva huku make ni Tyyne. Martti mnamo mwaka wa 1935 alibadilisha jina lake kutoka kwa Adolfsen na kuitwa Martti Oiva Kalevi Ahtisaari, lakini wengi wanamjua kama Martti Ahtisaari.

Amefanya kazi mbalimbali kama vile ualimu aliosomea na kuhitimu mwaka wa 1959..Pia aliwahi kuwa mwanajeshi mwenye cheo cha Captain.

Mbali na lugha yake mama Ahtisaari huzungumza Kiswiden,Kifaransa, kiingereza pamoja na Kijerumani.

Uwezekano wa kukielewa kiswahili ni mkubwa kwani aliwahi kuwa balozi wa Finland nchini Tanzania kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka wa 1973 hadi 1977.

Kabla ya hapo mwaka wa 1965 alijiunga na idara ya maendeleo ya kimatifa ya wizara ya kigeni ya Finland.

Wakati wa ubalozi wake nchini Tanzania,ambapo pia alikuwa anaiwakilsha nchi yake kati nchi za Zambia, Somalia,na Msumbiji, Ahtisaari,aliwasiliana na kundi la kisiasa la wazalendo wa Namibia la SWAPO mjini Darisalam.

Mwaka wa 1977 aliteuliwa kama kamishna wa Umoja wa Mataifa anaehusika na Namibia akikaa mjini New York Marekani hadi mwaka wa 1981.

Januari mwaka wa 1987, katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa wa wakati huo,Javier Perez de Cuellar alimteua Ahtisari kama katibu mkuu mdogo anaehusika na utawala pamoja na manejimenti hadi mwaka wa 1991.

Mwaka wa 1989 alitumwa Namibia kama mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa akiwa mkuu wa kundi la Umoja huo lililokuwa linasaidia utawala wa mpito UNTAG.

Baada ya Namibia kujipatia uhuru wake mwaka wa 1989 Ahtisaari alipewa uraia wa heshima wa nchi hiyo.

Baada ya hapo ndio akajitosa katika nyanja ya siasa kwao mwaka wa 1993, na mwaka uliofuatia chama chake cha Social Democratic Party kikashinda. Na yeye kama kiongozi wa chama hicho akashika hatamu za urais.

Rais Ahtisaari aliunga mkono hatua za nchi yake kujiunga na Umoja wa ulaya na katika kura ya maoni ya mwaka 1994.

Wakati wa enzi yake kama rais marais Bill Clinton wa Marekani pamoja na Boris Yeltsin wa Urusi walikutana kwa mazunguzo katika mkutano wa kihistoria nchini Finnland.

Aidha anasifiwa, pamoja na Viktor Chernomyrdin na vilevile Slobodan Milosevic kufanikisha kukomesha mapigano ya mkoa wa Yugoslavia wa Kosovo mwaka wa 1999.

Ahtisaari hakugombania tena uongozi katika uchaguzi wa mwaka wa 2000. Baada ya hapo alikubali nyadhifa mbalimbali katika mashirika mbalimbali ya kimataifa. Mfano mwaka wa 2000 aliteuliwa na Uingereza kuongoza ujumbe uliosimamia ukaguzi wa silaha za kundi la IRA katika Ireland kaskazini. Mwaka wa 2005 katibu wa Umoja wa Mataifa wa siku hizo, Koffi Annan, alimteua kuwa mjumbe wake maalum katika eneo la Kosovo.

Mapema mwaka huu Ahtisaari, alipewa shahada ya kiheshima ya Chuo kikuu cha University College cha mjini London Uingereza. Pia mwaka huo alipewa tuzo la amani la mwaka wa 2007 la UNESCO la Felix Houphouet-Boigny kutokana na mchango wake wa kuleta amani duniani.

Na leo Ijumaa pia amepewa tuzo la amani la Nobel la mwaka huu, kutokana na juhudi zake za kujaribu kutanzua migogoro katika mabara yote .