1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marubani Lufthansa wakataa pendekezo la malipo

Sekione Kitojo
26 Novemba 2016

Chama cha wafanyakazi marubani kimekataa pendekezo la malipo la shirika  la ndege la Ujerumani la hivi karibuni jana Ijumaa, lakini kimeondoa mara moja kitisho cha kuongeza mgomo wao kupindukia leo Jumamosi(26.11.2016).

https://p.dw.com/p/2THj9
Deutschland Lufthansa-Pilotenstreik  in München
Safari zilizofutwa katika shirika la ndege la LufthansaPicha: picture-alliance/dpa/M. Balk

Shirika  la Lufthansa limesema  hapo  mapema  limetoa  pendekezo kujaribu  kuvunja  mkwamo  katika  mzozo  wa  muda  mrefu  wa malipo  ya  nyongeza  ya  mshahara  na marubani  wa  shirika  hilo ambao  wamekuwa  katika  mgomo  tangu Jumatano.

Mgomo  wa  wiki  hii, wa 14 tangu  mapema  mwaka  2014, tayari umesababisha  kusitishwa  kwa  karibu  safari 2,600 na  kuathiri zaidi  ya  wasafiri 315,000. Lufthansa  imesema hali  hiyo  ya kuvurugika  kwa  safari  imeanza  kuathiri maombi  ya  safari kwa kipindi  cha  kati.

Deutschland Lufthansa-Pilotenstreik  in Berlin
hakuna kazi katika uwanja wa ndege wa FrankfurtPicha: picture-alliance/dpa/R. Jensen

Wasi wasi  kwa  wawekezaji

Marubani  walitishia  kurefusha  mgomo  wao  kupindukia  leo Jumamosi, wakiongeza  wasi  wasi  miongoni  mwa  wawekezaji  kwa kupanda  kwa  gharama  za  kampuni  hiyo na  athari  kubwa  zaidi katika  nchi  ya  Ujerumani  yenye  uchumi  mkubwa  katika  bara  la Ulaya.

Lakini chama  hicho  cha  wafanyakazi  marubani  kimesema  jioni ya  jana  Ijumaa  kwamba  haina  mpango wa  kuendelea  na  mgomo kupindukia  siku ya  Jumamosi.

Haikuondoa  hata  hivyo  uwezekano  wa  kuchukua  hatua  nyingine kama  hiyo hapo  baadaye,  lakini  chama  hicho  kimesema  mgomo mwingine  wowote  utatangazwa  masaa  24  kabla.

Deutschland Lufthansa-Pilot im Flughafen von Frankfurt am Main
Marubani wamegoma wanataka nyongeza ya mshaharaPicha: picture alliance/dpa/B. Roessler

Chama  hicho  kimepuuzia  pendekezo  la  hivi  karibuni la  shirika hilo  la  ndege   na  kusema  ni "hatua  ya kimahusiano na umma tu" na  kusema  si  jambo  jipya.

Lufthansa imesema  imetoa  pendekezo  la  kuongeza  mshahara kwa  asilimia  4.4 kwa awamu  mbili , pamoja  na  malipo  ya  mwezi mmoja  sawa  na  mshahara  wa  mwezi  kwa  asilimia  1.8.

Lufthansa  yaahidi

Shirika  hilo  pia  lilisema  limependekeza  kutengeneza  nafasi  za kazi 1,000 kwa  marubani  vijana  na  hadi  nafasi  600  za  marubani wanafunzi  katika  muda  wa  miaka  mitano ijayo. Shirika  limesema linaweza  kuingia  katika  mazungumzo  ya  upatanishi na chama  cha wafanyakazi  marubani  kuanzia  Novemba  29.

Kwa  upande  wake , marubani  watalazimika  kukubali  kubadilika kwa  mpango  wa  mafao yao  ya  uzeeni , ambapo  Lufthansa itawakikisha  malipo  ya  mchango  wao  tu.

Deutschland Flughafen Frankfurt
Ndege za shirika la ndege la Ujerumani LufthansaPicha: picture alliance/dpa/B. Roessler

Wafanyakazi  wa  kutoa huduma  katika  ndege  pamoja  na wafanyakazi  wa  uwanja  wa  ndege  tayari  wamekubaliana  na mabadiliko  haya.  Bettina  Volkens , mkuu  wa  idara  ya  nguvu  kazi katika  shirika  hilo, amesema  mabadiliko  hayo  yatasaidia  shirika hilo  kuhifadhi  fedha.

Chama  cha  wafanyakazi  kinataka  wastani  wa  ongezeko  la mishahara  kwa  mwaka  la  asilimia  3.7  kwa  marubani  5,400 nchini  Ujerumani  katika  kipindi  cha  miaka  mitano  kuanzia  mwaka 2012.

Lufthansa  linasema  linabidi  kupunguza  gharama  za  uendeshaji  ili kuweza  kushindana  na  mashirika  mengine  kama  Ryanair  katika njia  za  safari  fupi na  Emirates  katika  safari  ndefu, licha  ya kupata  faida  kubwa katika  mwaka  2015.

Ryanair
Shirika la ndege la RyanairPicha: picture-alliance/dpa/B. Roessler

Marubani  wa  Lufthansa  wanalipwa  vizuri  kwa  kiwango  cha tasnia  hiyo ya  safari  za  anga. Rubani  katika  shirika  la  Lufthansa analipwa  kiasi  cha  euro 180,000 kwa  mwaka  kabla  ya  kodi , licha  ya  kuwa  rubani  katika  kiwango  cha  juu  cha  malipo anaweza  kupata  hadi  euro  22,000  kwa  mwezi  kabla  ya  kodi.

Shirika  la  Lufthansa  limesema  hapo  kabla  kwamba  litalazimika kufuta  safari   nyingine  137  zaidi  leo  Jumamosi, ikiwa  ni  pamoja na  safari 88  za  mbali , na  kuwaathiri kiasi  ya  wasafiri 30,000. Shirika  hilo  pia  limesema  baadhi  ya  safari  fupi na  za  kati  pia zitaathirika.

Mwandishi: Sekione  Kitojo  / rtre

Mhariri: Sylvia  Mwehozi