1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mashambulio ya Boko Haram yalaaniwa vikali

Martin,Prema/rtre,afpe26 Desemba 2011

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon amelaani vikali mashambulio yanayolenga makanisa ya Wakristo nchini Nigeria na ametoa mwito wa kusitisha machafuko hayo

https://p.dw.com/p/13ZL1
Onlookers gather around a car destroyed in a blast next to St. Theresa Catholic Church in Madalla, Nigeria, Sunday, Dec. 25, 2011. An explosion ripped through a Catholic church during Christmas Mass near Nigeria's capital Sunday, killing scores of people, officials said. A radical Muslim sect claimed the attack and another bombing near a church in the restive city of Jos, as explosions also struck the nation's northeast. (Foto:Sunday Aghaeze/AP/dapd)
Mripuko mkubwa nje ya Kanisa la Mtakatifu Teresa mjini MadallaPicha: dapd

Mfululizo wa mashambulio ya bomu, yaliyolenga makanisa wakati wa ibada za Krismasi na shambulio jingine la kujitoa mhanga, yaliyoua hadi watu 40 nchini Nigeria yamelaaniwa na jumuiya ya kimataifa. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon ametoa rambirambi kwa watu wa Nigeria na familia zilizofiwa. Msemaji wake amesema, Ban ametoa mwito wa kukomesha mashambulio yote ya kimadhehebu nchini humo. Amesisitiza, hakuna kinachoweza kuhalalisha vitendo vya aina hiyo. Marekani pia imeyalaani mashambulio hayo na Ikulu yake mjini Washington imesema, serikali imeshazungumza na maafisa wa Nigeria na imeahidi kusaidia kuwafikisha mahakamani wale waliohusika na mashambulio hayo. Nae Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani Guido Westerwelle amesikitika kuwa hata siku kama ya Krismasi, ulimwengu hauwezi kujiepusha na vitendo vya uwoga na ugaidi.
Mripuko wa kwanza ulitokea kwenye Kanisa la Mtakatifu Teresa katika mji wa Madalla ulio kama kilomita 20 kutoka mji mkuu Abuja. Majengo yaliyo karibu na kanisa hilo yaliteketezwa katika mripuko huo mkubwa. Mashahidi wanasema, mripuko huo ulitokea, pale watu walipokuwa wakitoka kanisani. Kabla ya shambulio la hapo jana, mji wa Madalla haukudhaniwa kuwa katika hatari ya kushambuliwa. Mripuko wa pili ulitokea karibu na kanisa jingine katika mji wa machafuko Jos, katikati ya nchi huku mashambulio mengine yakiripotiwa kutoka eneo jingine la machafuko kaskazini mashariki ya Nigeria. Kanisa moja lililengwa mjini Gadaka katika jimbo la Yobe. Maafisa wa polisi wamesema, wataimarisha usalama katika maeneo ya ibada ili kuzuia mashambulio ya kulipiza kisasi katika kipindi hiki cha siku kuu.

Kundi la Kiislamu la Boko Haram linalotaka sheria za Kiislamu kutumiwa kote Nigeria, limedai kuwa ndilo lililohusika na mashambulio ya jana. Kundi hilo lilichomoka mwaka 2009, lakini lilishindwa na serikali katika kampeni inayodaiwa kukiuka haki za binadamu. Hata hivyo, likaibuka upya mwaka mmoja baadae, likishambulio majengo ya serikali. Mwaka mmoja uliopita zaidi ya watu 80 waliuawa katika mashambulio yaliyolenga sherehe za Krismasi. Mji mkuu Abuja ulilengwa mkesha wa mwaka mpya na hadi watu 30 waliuawa katika shambulio hilo. Kundi hilo linalaumiwa pia kuhusika na shambulio lililolenga ofisi za Umoja wa Mataifa mjini Abuja na kusababisha vifo vya watu 24. Rais wa Nigeria, Goodluck Jonathan alie Mkristo amesikitishwa na matukio ya jana na amesema, kundi la Boko Haram halitokuwepo milele. Litatokomea siku moja.