Mashambulio yapamba moto Syria
28 Januari 2012
Nchini Syria, vikosi vya usalama hapo jana viliimarisha ukandamizaji wake, huku wanaharakati wakiripoti vifo vya watu 120 katika kipindi cha siku mbili na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, likishinikizwa na Ulaya na nchi za Kiarabu kutoa mwito kwa Rais Bashar al-Assad kuondoka madarakani.
Mkuu wa tume ya waangalizi wa Umoja wa Nchi za Kiarabu, Jenerali Mohammed Ahmed Mustafa al-Dabi amesema, machafuko yamepamba moto, hasa katika miji ya kati ya Homs na Hama, iliyo ngome ya upinzani pamoja na eneo la Idlib kaskazini mwa nchi. Jenerali huyo amesema, mashambulio hayo hayasaidii kuyaleta pamoja makundi yote katika meza ya majadiliano.
Siku mbili mfululizo, vikosi vya Syria viliendelea kuushambulia mji wa Homs, wakati Morocco hapo jana ikiwasilisha mswada wa azimio lililotayarishwa na Uingereza, Ufaransa na Ujerumani pamoja na nchi za Kiarabu . Azimio hilo linatoa mwito kwa Umoja wa Mataifa hatimae kuchukua hatua ili kuumaliza ukandamizaji nchini Syria. Katika mswada wa azimio hilo, serikali ya Syria inatakiwa moja kwa moja kukomesha ukandamizaji, ambao Umoja wa Mataifa unasema, umesababisha zaidi ya vifo 5,400 tangu mwezi Machi.
Lakini balozi wa Urusi katika Umoja wa Mataifa, Vitaly Churkin amesema, mswada huo hauambatani na msimamo wao. Urusi inapinga cho chote kuhusiana na vikwazo, marufuku ya silaha au mabadiliko ya serikali nchini Syria. Mwezi wa Oktoba, Urusi na China zilitumia kura ya turufu kupinga azimio lililopendekezwa na Ulaya, zikituhumu kuwa nchi za magharibi zinataka mabadiliko ya serikali. Majadiliano rasmi kuhusu azimio hilo jipya, yanatazamiwa kuanza jumatatu ijayo mjini New York.