1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mashambulizi ya Israel yauwa wanamgambo saba wa Hamas

7 Julai 2014

Mashambulizi ya anga ya Israel yamewauwa wanamgambo saba wa kundi la Hamas huko Gaza na kundi hilo limeapa kulipiza kisasi kufuatia mapambano makali kuwahi kushuhudiwa hivi karibuni.

https://p.dw.com/p/1CWs4
Wanajeshi wa Israel nje ya Ukanda wa Gaza. (07.07.2014)
Wanajeshi wa Israel nje ya Ukanda wa Gaza. (07.07.2014)Picha: Reuters

Mashambulizi ya anga yaliendelea usiku kucha huko Gaza kwa kile Israel ilichosema kuvilenga vituo vya kigaidi kufuatia kuvurumishwa kwa maroketi nchini Israel yakitokea Gaza.

Kundi la Hamas lenye kutawala Ukanda wa Gaza limesema adui atalipa kwa gharama kubwa wakiikusudia Israel.Kundi hilo limesema wanachama wake wameuwawa kutokana na mashambulizi ya Israel yaliofanywa kwenye handaki moja lililokuwa linatumiwa na wanamgambo.

Wanamgambo wawili kutoka kundi jengine tafauti pia wameuwawa katika shambulio tafauti.Jeshi la Israel limesema wanamgambo hao walikuwa wamehusika na mashambulizi ya maroketi kwa wakaazi wa Israel wanaoishi kusini mwa nchi hiyo.

Vituo vya kigaidi vyalengwa

Israel imesema imefanya mashambulizi ya anga katika maeneo 14 ya kigaidi likiwemo eneo la siri la kufyetulia maroketi huko Gaza wakati wa usiku kujibu mapigo kwa makambora yaliokuwa yakivirumishwa Israel kutokea Gaza.

Wanajeshi wa Israel wakiwa nje ya eneo la Gaza ya Kati.(06.07.2014)
Wanajeshi wa Israel wakiwa nje ya eneo la Gaza ya Kati.(06.07.2014)Picha: Reuters

Takriban maroketi 12 yamevurumishwa Israel kutoka Gaza wakati wa usiku na mwanajeshi mmoja wa Israel amejeruhiwa na hapo Jumapili maroketi 25 yamevurumishwa Israel na wanamgambo hao wa Gaza.

Doria ya jeshi la Israel imeshambulia leo asubuhi kwenye uzio wa mpaka wa Gaza lakini hakuna aliejeruhiwa katika shambulio hilo.

Chanzo cha ghasia

Ghasia za Gaza zinakuja wakati machafuko yakipamba moto katika eneo la Jerusalem ya Mashariki lililotwaliwa na Israel na miji ya Waarabu ilioko Israel kufuatiwa kutekwa nyara na kuuwawa kwa kijana wa Kipalestina katika mauaji ya kisasi yanayotuhumiwa kufanywa na Wayahudi wa sera kali za utaifa.

Wapalestina wakiwavurumishia mawe polisi wa Israel katika kitongoji cha Shuafat.
Wapalestina wakiwavurumishia mawe polisi wa Israel katika kitongoji cha Shuafat.Picha: Getty Images

Rais Mahamud Abbas wa Mamlaka ya Palestina akiyalaani mauaji hayo amesema "Nieomba kuundwa kwa kamati ya kimataifa kuhusiana na uhalifu wa kigaidi unaotendwa dhidi ya wananchi wa Kipalestina hususan kuteketezwa kwa mtoto Mohamed Abud Khder wakati akiwa hai."

Israel hapo jana imewakamata watuhumiwa sita ya Kiyahudi kuhusiana na mauaji hayo na viongozi wa Israel wametowa wito wa kuwepo kwa utulivu kutokana na kuwepo ishara kwamba mauaji hayo yalikuwa ya kulipiza kisasi kwa mauaji ya hivi karibuni ya vijana watatu wa Israel.

Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu ametowa rambi rambi zake kwa baba wa kijana huyo na kuahidi kuwafikisha wahusika wa mauaji mbele ya mkono wa sheria.

Mwandishi : Mohamed Dahman/ AP/dpa

Mhariri : Mohammed Abdul-Rahman