1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Matamshi ya Rais Medvedev yatekelezwe kwa vitendo

I.Mannteufel/P.Martin6 Juni 2008

Kidiplomasia,ziara ya rais mpya wa Urusi Dmitry Medvedev nchini Ujerumani imefanikiwa.Sasa yaliyotamkwa na kiongozi huyo yatimizwe kwa vitendo,ama sivyo hatoaminika.

https://p.dw.com/p/EEoS
Bundeskanzlerin Angela Merkel begruesst am Donnerstag, 5. Juni 2008, den Praesidenten Russlands, Dimitri Mewedew, vor dem Bundeskanzleramt in Berlin. (AP Photo/Eckehard Schulz)
Kansela wa Ujerumani Angela Merkel(kulia)akimkaribisha Rais wa Urusi Dmitry Medvedev mjini Berlin Juni 5,2008.Picha: AP

Ziara rasmi ya kwanza iliyofanywa Ujerumani na Rais mpya wa Urusi Dmitry Medwedew ni ishara ya kuendeleza uhusiano uliopo kati ya Ujerumani na Urusi.Medvedev na Kansela wa Ujerumani Angela Merkel wamekariri misimamo yao inayojulikana kuhusu masuala ya pande hizo mbili na ya kimataifa.

Medvedev amekosoa mpango wa Shirika la Kujihami la Nchi za Magharibi NATO kupanuka hadi Ulaya ya Mashariki na mfumo wa Marekani kuweka makombora ya kujihami katika nchi za Ulaya ya Mashariki.Na kama mtangulizi wake Vladimir Putin,Rais Medvedev pia ametoa wito kwa Ujerumani na nchi zingine za Ulaya kufungua zaidi masoko yao kwa vitega uchumi vya Urusi.

Lakini Rais Medvedev na Kansela Merkel walikuwa na msimamo mmoja waliposisitiza umuhimu wa kila nchi kwenye uhusiano wa kiuchumi.Kwa hivyo Merkel alitetea mpango unaohusika na ujenzi wa mabomba ya kusafirishia mafuta kupitia Bahari ya Mashariki na ameahidi kuondosha wasiwasi wa nchi zingine katika eneo hilo.Viongozi wote wawili wanatumaini kuendeleza uhusiano uliopo hasa kupitia makubaliano mapya ya ubia na ushirikiano kati ya Urusi na Umoja wa Ulaya.Kimsingi hakuna kilicho kipya:Ujumbe wa ziara ya Medvedev ni huu: kuendelea na siasa za Urusi na kuimarisha uhusiano kati ya Ujerumani na Urusi.

Lakini jambo moja lililobainika katika ziara hii ni yale mazingira ya kirafiki,hata ulipokosolewa mpango wa NATO kujipanua hadi mashariki mwa Ulaya au ule mfumo wa makombora ya kujihami ya Marekani.Lugha iliyotumiwa na Medvedev ilikuwa tofauti kabisa na vile mtangulizi wake Vladimir Putin alivyohotubia mkutano wa ulinzi wa kimataifa mjini Munich mwaka 2007.Na Kansela Merkel pia alijitahidi kufuata mkondo huo wa kirafiki.Tofauti za maoni kuhusu haki za binadamu nchini Urusi ziligubikwa na matamshi ya kidiplomasia. Hata kwenye mkutano wa waandishi wa habari alipoulizwa kuhusu tajiri wa Kirusi Mikhail Chodorkowski alie jela nchini Urusi,Merkel alikuwa na tahadhari.Ni dhahiri kuwa Kansela Merkel na mgeni wake Rais Medvedev hawakutaka kuchafua mazingira ya kirafiki.

Kwa kweli,ziara ya kwanza ya Dmitry Medvedev kama rais wa Urusi nchini Ujerumani,haikutazamiwa kuleta matokeo thabiti.Hata hivyo,ziara hiyo fupi mjini Berlin imeweka msingi mzuri kuimarisha na kuendeleza uhusiano kati ya Ujerumani na Urusi katika miezi ijayo.