1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Matokeo ya uchaguzi wa Saarland yahanikiza magazetini

Oumilkheir Hamidou
3 Aprili 2017

Mada kuu magazetini inahusu matokeo ya uchaguzi wa bunge katika jimbo dogo kabisa miongoni mwa majimbo 16 ya Ujerumani, Saarland . Hata hivyo wahariri wa magazeti ya Ujerumani wamemulika pia miaka 60 ya Umoja wa Ulaya .

https://p.dw.com/p/2a1GX
Infografik Prognose Wahl Saarland 2017 ENG

Tunaanzia katika jimbo la Saar, ambako matokeo ya uchaguzi wa bunge yamepindua makadirio yote ya awali na kuvunja ndoto ya kuundwa serikali ya mrengo wa kushoto. Uchaguzi katika jimbo la Saar ulitajwa kuwa kipimo cha matokeo ya uchaguzi mkuu msimu wa mapukutiko unaokuja. Gazeti la "Die Rheinpfalz" lina maoni tofauti kabisa na kuanadika: "Hasha, uchaguzi wa Saarland haukuwa kipimo, si kipimo kwa chaguzi zinazokuja za majimbo na wala si kipimo kwa uchaguzi mkuu. Kwanza hali yenyewe ni tofauti kabisa, kuanzia waziri mkuu anaetabasamu  hadi kufikia mrengo wa kushoto, die Linke wenye nguvu na walinzi wa mazingira waliodhoofika kupita kiasi. Licha ya yote hayo lakini matokeo ya uchaguzi wa Saarland yatakiuka mipaka ya jimbo hilo. Matokeo hayo ya uchaguzi yatakipatia imani kubwa zaidi na kukifaanya kizidi kujiamini  chama cha CDU, ambacho wiki za nyuma kilionekana kutojua la kufanya mbele ya sumaku ya chama cha SPD na mgombea wake Martin Schutz,

 

Uchaguzi wa jimbo la Northrhine Westphalia ndio kipimo cha kweli

Juhudi za Martin Schulz katika jimbo alikozaliwa babaake hazikusaidia kitu na matumaini ya kuundwa serikali ya muungano ya vyama vya mrengo wa kushoto yamesalia kuwa ndoto katika jimbo hilo ambako CDU wako madarakani tangu miaka 18 iliyopita. Hata hivyo gazeti la "Hannoversche Allgemeine" linatahadharisha na kuandika: "Kansela Merkel anabidi atahadhari asiyatathmini vibaya matokeo ya uchaguzi katika jimbo la Saar. Ni sawa kabisa kwamba  matokeo hayo ya uchaguzi ni mwanzo mwema kwa CDU kwa mwaka huu muhimu utakaoshuhudia chaguzi tatu kabla ya uchaguzi mkuu. Hata hivyo matokeo hayo hayaashirii mengi . Kansela Angela Merkel atabidi azindukane pamoja na chama anachokiongoza . Mtihani wa kweli ni pale uchaguzi utakaöaoitishwa katika jimbo la Northrhine Westphalia,mwezi may unaokuja.

Miaka 60 ya Umoja wa ulaya

 Mada yetu ya mwisho magazetini inahusu maadhimisho ya miaka 60 ya Umoja wa ulaya. Viongozi wa mataifa 27 ya Umoja wa ulaya ,bila ya Uingereza, wameelezea dhamiri yao ya kuuimarisha Umoja wao. Gazeti la "Frankfurter Rundschau" linaandika: "Mtu angependa hadi kuamini ahadi zao. Viongozi 27 wa taifa na serikali wanataka umoja wa Ulaya unaozingatia zaidi mahitaji ya jamii, usawa na kuhakikisha usalama wa ndani na nje pamoja na kuimarisha umoja wa kiuchumi na sarafu. Lakini pekee mivutano kuhusu baadhi ya maneno yaliyotumika katika "Ratiba ya Roma" huku baadhi wakitishia kutotia saini waraka huo, inadhihirisha kwa mara nyengine tena ukosefu wa umoja miongoni mwa viongozi wa Umoja wa ulaya. Hata hivyo kuna la kutia moyo linalotokana na sherehe za Rome. "Ratiba ya Roma" inazungumzia mada kadhaa zinazobidi kufanyiwa marekebisho.

 

Mwandishi:Hamidou Oumilkheir/Inlandspresse

Mhariri:Yusuf Saumu