1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mazungumzo juu ya kugawana wizara yaendelea leo.

Mtullya, Abdu Said15 Oktoba 2008

Rais Robert Mugabe na kiongozi wa upinzani Morgan Tsvangirai bado hawajafikia mapatano juu ya kugawana mamlaka nchini Zimbabwe.

https://p.dw.com/p/FZmh
Waziri mkuu mteule wa Zimbabwe Morgan Tsvangirai.Picha: AP


Mazungumzo ya kuyaokoa mapatano yaliyofikiwa hapo awali juu ya kugawana madaraka nchini Zimbabwe yanatarajiwa kuendelea leo baada ya kushindikana jana mjini Harare.

Mjumbe wa serikali ya Rais Robert Mugabe na kiongozi wa upinzani Morgan Tsvangirai wanakutana tena leo chini ya usuluhishi wa aliekuwa rais wa Afrika Kusini Thabo Mbeki.

Mapatano yaliyofikiwa mwezi mmoja uliopita juu ya kugawana madaraka baina ya rais Robert Mugabe na kiongozi wa chama cha MDC bwana Tsvangirai sasa yapo hatarini kusambaratika kutokana na tofauti zilizojitokeza kuhusu ugawanaji wa wizara. Bwana Tsvangirai ametishia kususua mazungumzo hayo baada ya rais Mugabe kuamua kuchukua wizara zote muhimu kwa ajili ya chama chake cha Zanu- PF.

Hatahivyo rais Mugabe amesema kuwa mazungumzo yanasonga mbele madam yanaendelea leo.Amesema hatua zimepigwa katika vipengere fulani.

Mjumbe mwengine anaeshiriki kwenye mazungumzo hayo ,bwana Arthur Mutambara anaeongoza kikundi kilichojitenga na chama cha MDC pia amesema kuwa mazungumzo ya jana yalikuwa ya kutia moyo.

Mjumbe wa chama cha ZANU- PF kwenye mazungumzo hayo waziri wa sheria bwana Patrick Chinamasa ameeleza matumaini kwamba huenda mpatanishi wa mazungumzo hayo bwana Thabo Mbeki akatoa mapendekezo mapya. Hatahivyo wadadaisi wanasema bwana Mbeki hana uzito tena.

Wakati huo huo Marekani imemlaumu rais Mugabe kwa kukiuka mapatano yaliyofikiwa juu ya kugawana madaraka na mpinzani wake MorganTsvangirai. Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Marekani Sean McCormack amewaambia waandishi habari kuwa rais Mugabe amevuka mipaka kwa kuamua kujichukulia wizara zote muhimu kinyume cha mapatano yaliyofikiwa.

Rais Robert Mugabe aliukasirisha upande wa upinzani mwishoni mwa wiki iliyopita baada ya kuamua kujichukulia wizara za ulinzi, mambo ya ndani inayosimamia polisi na wizara ya fedha.Hatahivyo bunge la Zimbabwe lilianza kukutana jana kwa mara ya kwanza baada ya kufunguliwa rasmi na rais Mugabe.