1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mdahalo wa taifa nchini Ukraine.Wanaoshiriki ni Nani

14 Mei 2014

Nchini Ukraine,matumaini ya nchi za magharibi yanawekewa "mdahalo wa taifa" unaotarajiwa kuitishwa leo na serikali ya Ukraine licha ya matumizi ya nguvu yanayoendelea masharikia ya nchi hiyo

https://p.dw.com/p/1BzTM
Waziri mkuu wa mpito wa Ukraine Arseni Yatszenyuk akipeana mkono na mwenyekiti wa halmashauri kuu ya Umoja wa ulaya Jose Manuel Barroso katika makao makuu ya Umoja huo mjini BrusselsPicha: Georges Gobet/AFP/Getty Images

Kansela Angela Merkel wa Ujerumani ameshauri "midahalo "itakayoitishwa hivi karibuni nchini Ukraine iwajumuishe wawakilishi wengi zaidi,akishadidia hata hivyo na hapa tunanukuu"weye kuchochea matumizi ya nguvu" wasipewe nafasi ya kushiriki.""Nnaamini uwezekano wa kuitishwa meza ya majadiliano ni fursa nzuri,ili kujaribu kusaka njia ya kupunguza makali ya mzozo wa Ukraine,inayokabiliwa na kitisho cha kugawika" amesema kansela Angela Merkel wakati wa mkutano na waandishi habari mjini Berlin.

Meza ya majadiliano isiyo bayana imepangwa kuitishwa leo jioni.Kwa mujibu wa waziri mkuu wa Ukraine Arseniy Yatsenyuk marais watatu wa zamani wa Ukraine,wagombea wa uchaguzi wa rais wa May 25 ijayo pamoja pia na wabunge na wakuu wa kimkoa ni miongoni mwa watakaohudhuria meza hiyo ya majadiliano.Wakuu wa waasi wanaopigania kujitenga eneo la mashariki ambao serikali ya mjini Kiev inawataja kuwa ni "magaidi" wanaonyesha hawajaalikwa licha ya miito ya mara kwa mara ya Moscow kutaka mikutano kama hiyo iitishwe.

Hatima ya mazungumzo haijulikani,Juhudi zinazoendelezwa ni tete

Majadiliano yatasimamiwa na mwanadiplomasia wa zamani wa Ujerumani Wolfgang Ischinger na yatatuwama zaidi katika masuala kuhusu mfumo wa kueneza madaraka majimboni na juhudi za kupambana na rushwa.

Steinmeier im Elysee Palast Kabinettssitzung 14.05.2014
Waziri wa Mambo ya nchi za nje wa Ujerumani akizungumzia suala la Ukraine mbele ya baraza la mawaziri la Ufaransa mjini Paris.(kulia) rais Francois Hollande wa UfaransaPicha: Reuters

Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ujerumani Frank-Walter Steinemeier aliyewasili Kiev jana,na kutazamiwa baadae kwenda Odessa kusini mwa Ukraine anasema "huu ni mwanzo tu.

Juhudi zinazoendelezwa za kidiplomasia ni tete" amekiri waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ujerumani Steinmeier ambae ameshaitembelea mara tatu UKraine tangu alipokabidhiwa wadhifa huo.Anasema"Sio wote wanaotaka kuzungumza,baadhi wanapendelea matumizi ya nguvu-amemaliza kusema mwanadplomasia huyo mkuu wa Ujerumani

Frank-Walter Steinemeier anatazamiwa kuwasili Paris baadae hii leo ambako ataonana na waziri mwenzake wa Ufaransa Laurent Fabius na katika tukio linaloangaliwa kuwa ni la aina pekee kabisa anatazamiwa"kuzungumzia matokeo ya ziara yake nchini Ukraine mbele ya baraza la mawaziri la Ufaransa."

Matumaini ya kufanikiwa mdahalo wa taifa ni finyu

Zikikabiliwa na kitisho chengine cha kuiona Ukraine inagawika kufuatia kile kinachoitwa kura ya maoni iliyoitishwa jumapili iliyopita katika maeneo ya mashariki ya Ukraine,nchi za magharibi pamoja na jumuia ya Usalama na ushirikiano barani Ukaya OSCE zinafanya juhudi za kuzileta katika meza ya mazungumzo pande zinazohasimiana.Lakini matumaini ya kufanikisha juhudi hizo yanaonyesha kumwagiwa mchanga baada ya ripoti za kuuliwa wanajeshi sabaa wa serikali karibu na mji wa Kramatorsk,katika jimbo la Donetsk.

Barrikaden Regionalverwaltung 12.05.2014 Donezk
Jengo la serikali ya mkoa huko Donetsk lazingigwa na waasiPicha: DW/K. Oganesian

Urusi pia inaonyesha kuvuta wakati ikihoji masharti ya kuitishwa mdahalo kama huo bado hayajakamilika.

Urusi inaitaka serikali ya mjini Kiev isitishe hujuma dhidi ya waasi wanaotaka kujitenga.

Mwandishi: Hamidou Oummilkheir/AFP

Mhariri: Josephat Charo