1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

MECCA : Wapalestina wakubali kuunda serikali ya kitaifa

9 Februari 2007
https://p.dw.com/p/CCTl

Makundi hasimu ya Wapalestina ya Fatah na Hamas yamefikia makubaliano ya kuunda serikali ya umoja wa kitaifa katika mazungumzo yaliokuwa chini ya upatanishi wa Saudi Arabia katika mji mtakatifu wa Mecca.

Makubaliano hayo yanayojulikana kama Azmio la Mecca yametiwa saini na Rais Mahmoud Abbas wa Palestina ambaye analiongoza kundi la Fatah na Khaled Meshaal kiongozi wa Hamas anayeishi uhamishoni nchini Syria ambaye kundi lake limeshinda uchaguzi wa Palestina mwaka jana.Waziri Mkuu Ismail Haniyeh ataendelea kushikilia wadhifa wake.

Hamas itakuwa na nyadhifa nane za mawaziri wakati Fatah itakuwa na nyadhifa sita.Wizara muhimu za mambo ya nje na mambo ya ndani zitashikiliwa na watu huru.

Hakuna tamko rasmi juu ya sera ya serikali hiyo mpya hususan iwapo Hamas imekubali dai kuu la Kundi la Kimataifa la Pande Nne juu ya amani ya Mashariki ya Kati linalojumuisha Marekani, Umoja wa Ulaya,Umoja wa Mataifa na Urusi kutaka iitambuwe Israel.

Maafisa wa Fatah wamesema serikali hiyo mpya itaheshimu makubaliono yaliyopita ya Israel na Wapalestina lakini haijulikani kwa kiasi gani. Mapambano ya kuwania madaraka kati ya makundi hayo mawili tokea mwezi wa Desemba yamegharimu maisha ya watu 100.

Katika Ukanda wa Gaza ambapo ndiko umwagaji mkubwa wa damu umetokea kati ya makundi hayo Wapalestina wamesheherekea kufikiwa kwa makubaliano hayo kwa kufyatuwa risasi hewani sherehe hizo pia zimefanyika katika mji wa Ukanda wa Magharibi wa Ramallah.