1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mengi yamechambuliwa na wahariri

Oumilkher Hamidou25 Oktoba 2010

Malalamiko ya FDP sawa na maandamano ya Ufaransa na nyaraka za siri zilizochapishwa na Wikileaks ni miongoni mwa mada zilizochambuliwa magazetini hii leo

https://p.dw.com/p/PnLK
Ilikua October 28 mwaka 2009 pale Westerwelle (kulia) alipompongeza kansela Merkel baada ya kuchaguliwa na bunge la shirikisho kuendelea na wadhifa wakePicha: AP

Tuanzie lakini mjini Berlin ambako jungu la serikali ya muungano wa vyama vya CDU/CSU na waliberali wa FDP linatokota.Chanzo, linaandika gazeti la "Südkurier Konstanz", ni :

Ahadi alizotoa kansela Angela Merkel nchini Ufaransa bila ya kukubaliana na waziri wa mambo ya nchi za nje.FDP wanalalamika-na si bure.Kansela alibidi atilie maanani kwamba:Mwaka 2011 unakurubia pakiwepo chaguzi sita za majimbo-na kishindo kikubwa zaidi kinakutikana katika uchaguzi wa jimbo la kusini Baden Wurttemberg.Hakuna kinachochukiwa na wapiga kura kama mvutano miongoni mwa washirika serikalini.Jambo hilo ndilo linalowalazimisha waliberali wameze machungu na wajiepushe kunyunyizia mafuta katika cheche za moto.Katika muungano huu pia kuna utaratibu wa nani anafanya nini,kama ilivyokuwa katika enzi za Helmut Kohl na Gerhard Schröder.Katika siasa ya Ulaya ,kansela ndie anaeshika usukani,waziri wa mambo ya nchi ya nje ni msaidizi tu.Westerwelle kwa hivyo hana budi isipokua kumeza machungu yanapotokea.

Kuhusu mageuzi katika jeshi la shirikisho Bundeswehr,gazeti la "Nordwest-Zeitung" linaandika:

Kile ambacho katika makampuni ya kibinafsi ni jambo la kawaida kufanyika,yaani kutathmini upya miundo mbinu, na jeshi la shirikisho Bundeswehr pia haliwezi kukwepa.Kutokana na changamoto ya kitisho cha ugaidi wa kimataifa na kubadilika medani ya usalama,jeshi la shirikisho Bundeswehr halina budi isipokua kuzidisha uwezo wake na kubuni aina mpya ya uongozi.Waziri wa ulinzi zu Guttenberg atakabiliana na hali hiyo na kama ajulikanavyo,atatekeleza mageuzi yanayohitajika.

Frankreich Protest Streik Blockade Rentenreform Sarkozy Paris
Wapinzani wa mageuzi ya muda wa kustaafu huko Ivry-sur-Seine karibu na ParisPicha: AP

Ama kuhusu maandamano ya Ufaransa,gazeti la "Emder Zeitung" linaandika:

Wote,tangu wajerumani mpaka wafaransa watalazimika miaka ijayo,kufanya kazi miaka miwili zaidi kabla ya kustaafu.Katika nchi zote hizi mbili kuna watu tena wengi tuu wanaohisi hali hiyo si ya haki.Hisia hizo lakini misingi yake ni tofauti toka nchi moja hadi nyengine.Katika wakati ambapo hapa nchini umri wa kustaafu utarefushwa na kuwa miaka 67,wafaransa wanaweza kustaafu wakiwa na umri wa miaka 62.Kwa hivyo wajerumani wanashindwa kuelewa ghadhabu za wafaransa.Zaidi ya hayo watu wameingiwa na wasi wasi kutokana na kile kinachoendelea upande wa pili.Katika zoni ya Euro watu hawawezi kufumba macho ikiwa watu maarufu kama hao wa Ufaransa wanaona bora pensheni yao ilipwe kupitia madeni makubwa makubwa kuliko kuzidisha muda wa kufanya kazi.Madhara yake yanajulikana-tuchukue mfano wa Ugiriki.Wafaransa wakicheza na moto,na majirani pia wataungua.

Ripoti yetu ya mwisho inahusu kufichuliwa nyaraka za siri kuhusu maovu yaliyofanyika wakati wa vita vya Iraq.Gazeti la "Der neue Tag" linaandika

Kilichosalia ni matumaini kwamba tovuti kama hiyo ya Wikileaks,siku za mbele,sio tuu zitatathmini yanayotokea vitani bali pia zitasaidia kuepusha vita visiripuke.Ingekua Wikileaks ilikuwepo katika mwaka 2003,pale waziri wa mambo ya nchi za nje wa Marekani Collin Powell,aliposimama mbele ya Umoja wa mataifa na kuzungumzia eti kuhusu silaha za maangamizi za Sadam Hussein,pengine Marekani isingeanzisha vita kabisa nchini Iraq.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/inlandspresse

Mpitiaji:Othman Miraji