1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mgombea wa upinzani ajitangazia ushindi Gabon

29 Agosti 2016

Mgombea mkuu wa upinzani amejitangazia ushindi katika uchaguzi wa urais uliofanyika Gabon wakati kambi ya rais Ali Bongo ikisema kauli yake hiyo ni hatari na sio halali kabla ya kutangazwa kwa matokeo rasmi.

https://p.dw.com/p/1JrZs
Picha: picture-alliance/dpa/E.Laurent/L.JinMan

Wafuasi wa mgombea mkuu wa upinzani katika uchaguzi wa rais wa Gabon wameingia mitaaani mjini Brazaville kusheherekea ushindi hapo Jumamosi lakini wanahofu rais anayetetea wadhifa wake Ali Bongo yumkini akatumia nguvu kuendelea kubakia madarakani.

Jean Ping mwanasiasa mkongwe mwenye umri wa miaka 73 hapo jana amejitangazia ushindi kwa kutamka kwamba amechaguliwa na anasubiri rais anayemaliza muda wake ampongeze kauli ambayo imewafanya wafuasi waibuke kwa vifijo na kumshangilia kwa kauli ya Ping ni rais.

Matokeo rasmi yanatarajiwa kutolewa hapo kesho na baadhi ya wapiga kura wana hofu kutokea tena kwa ghasia zilizoshuhudiwa baada ya uchaguzi wenye utata hapo mwaka 2009.

Kujitangazia ushindi ni hatari

Msemaji wa Bongo amesema tangazo hilo la kujitangazia ushindi ni la hatari wakati waziri wa mambo ya ndani Pacome Moubelet Boubeya akionya kwamba ni kinyume na sheria kutangaza matokeo kabla ya mamlaka husika kufanya hivyo.

Mgombea wa urais Jean Ping akipiga kura yake.
Mgombea wa urais Jean Ping akipiga kura yake.Picha: Reuters/E. W. Obangome

Inadaiwa kwamba Ping amemshinda Bongo kwa asilimia 60 kwa 40 ya kura ambazo zilikuwa zimehesabiwa haikuwezekana kuyakinisha madai hayo moja.

Kwa mujibu wa timu ya Ping mgombea huyo amekutana na balozi wa Ufaransa mkoloni wa zamani wa nchi hiyo muda mfupi baada ya kujitangazia ushindi.

Wagombea wakuu wote wawili walikuwa wamejitabiria ushindi na wamekuwa wakishutumiana kwa kufanya udanganyifu katika uchaguzi huo.

Muda mfupi baada ya kumalizika kwa uchaguzi huo hapo Jumamosi msemaji wa rais amesema "Bongo atashinda na kwamba tayari walikuwa njiani kuelekea kwenye muhula wa pili madarakani."

Bongo asubiri matokeo rasmi

Bongo mwenyewe akizungumza hadharani kwa mara ya kwanza tokea uchaguzi huo wa Jumamosi amesema anasubiri kutangazwa kwa matokeo.

Rais anayetetea wadhifa wake Ali Bongo akipiga kura yake.
Rais anayetetea wadhifa wake Ali Bongo akipiga kura yake.Picha: Getty Images/AFP/M. Longari

Amesema "Wananchi wenzangu tutafuata sheria na tutasubiri kwa utulivu tume ya uchaguzi ya taifa itangaze matokeo. Tutasubiri kwa utulivu na kwa kujiamini nataka kumshukuru kila mtu tuwe na matumani mambo mazuri yanakuja."

Mkuu wa kundi la Uangalizi wa Demokrasia la Umajumui wa Kiafrika ambalo ni shirika lisilo la kiserikali lenye makao yake nchini Togo amepuuza uzito wa kauli ya Ping kujitangazia ushidi.

Mitaa katika mji mkuu wa Libreville hapo jana ilikuwa mitupu na maduka ambayo kawaida hufunguliwa siku ya Jumapili yalikuwa yamefungwa.

Mwandishi : Mohamed Dahman /AFP

Mhariri : Iddi Ssessanga