1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mgomo wa upinzani Zimbabwe waambulia patupu

Mwakideu, Alex16 Aprili 2008

Hakuna anaeamini Mugabe alishinda uchaguzi wa Zimbabwe, asema Waziri mkuu wa Uingereza Gordon Brown

https://p.dw.com/p/DjAv
Rais wa Afrika Kusini Thabo Mbeki na Robert Mugabe wa ZimbabwePicha: AP

Baada ya mgomo uliopangwa na Chama cha upinzani nchini Zimbabwe Movement for Democratic Change kuambulia patupu, Chama hicho kinalalama kwamba wafuasi wake hamsini wamekamatwa tangu mgomo huo uanze jana.


Walinda asalama mjini Harare wamepunguzwa leo kufuatia kutofaulu kwa mgomo huku Marekani ikipanga kujadili mgogoro wan chi hiyo katika kikao cha leo cha baraza la usalama la Umoja wa Mataifa nchini Africa Kusini.


Wafanyikazi nchini Zimbabwe wameendelea na shughuli zao kama kawaida katika siku ya pili ya mgomo uliotishwa na upinzani nchini humo kwa nia ya kushinikiza kuwekwa wazi kwa matokeo ya uchaguzi wa Urais.


Hali barabarani inaendelea vizuri huku vizuizi vilivyokuwa vimewekwa hapo jana vikipunguzwa na usafiri ukiendelea bila wasi wasi licha ya mgomo huo.


Baadhi ya sababu ambazo huenda zimepelekea kutofaulu kwa mgomo huo ni uoga, umuhimu wa kutafuta pato la jamii na hata uamuzi binafsi wa wafanyikazi waliotarajiwa kugoma.


Chama cha upinzani nchini Zimbabwe kinadai kwamba wafuasi wake zaidi ya hamsini akiwemo mbunge wamekatwa na polisi tangu mgomo huo uanze hapo jana; jambo ambalo linapingwa na polisi wakisisitiz kwamba wamekamata watu 33 tu kwa mashtaka ya kujaribu kuvuruga amani.


Wakati huo huo muungano wa chama cha madaktari nchini Zimbabwe umetoa ripoti yao inayoonyesha watu zaidi ya 150 walipigwa na kuteswa tangu uchaguzi ulipomalizika mwezi machi.


Chama hicho kinachojulikana kama The independent Zimbabwe Association of Doctors for Human Rights kinasema watu hao walitibiwa majeraha yanayodhibitisha waliteswa. Theluthi ya watu hao ni wanawake akiwemo msichana mwenye miaka 15.


Kufuatia hali hii Mjumbe wa Umoja wa Mataifa kutoka Marekani Zalmay Khalilzad amesema sharti Zimbabwe itajwe katika kikao cha baraza la usalama la Umoja wa Mataifa kinachofanyika leo nchini Africa Kusini licha ya nchi hiyo kupinga hatua hii.


Mjumbe wa Africa Kusini katika Umoja huo Dumisani Khumalo ametetea nchi yake.


Kwa upande mwengine Mwenyekiti wa chama cha ANC nchini Africa Kusini Jacob Zuma amesema mgogoro unaoendelea nchini Zimbabwe unatisha na akatoa wito wa suluhisho la dharura kwa nchi jirani.


Asilimia themanini ya raia nchini Zimbabwe hawana kazi na mfumuko wa bei nchini humo unazidi asilimia laki moja.


Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon anasema Zimbabwe inahitaji uwazi na kutolewa kwa matokeo ya uchaguzi kwa njia ya maelewano ili watu wa nchi hiyo waweze kufurahia hatu hiyo ya demokrasia na pia wanatakiwa waweza kufaulu katika hali hii.


Vyombo vya habari vya serikali nchini Zimbabwe vimezishutumu Uingereza na Marekani kwa madai kwamba zinatafuta azimio la Umoja wa Mataifa la kutumia jeshi kuung'oa utawala wa Rais Mugabe.


Kiongozi wa chama cha upinzani nchini humo Morgan Tsvangirai anadai kwamba ameshinda uchaguzi wa Urais wa machi tarehe 29 huku chama cha ZANU PF kinachoongozwa na Mugabe kikiitisha kurejelewa kwa uchaguzi huo au kuhesabiwa tena kwa kura hizo.


Kwa upande mwengine mwandishi wa habari raia wa Marekani na raia mwengine wa Uingereza ambao walishtakiwa kwa kuripoti uchaguzi wa Zimbabwe bila idhini wameachiliwa huru baada ya mahakama kukosa ushahidi wa kutosha kuhusu sheria walizovunja.