1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
HistoriaUjerumani

Miaka 60 iliyopita: Ujenzi wa ukuta wa Berlin

Iddi Ssessanga
13 Agosti 2021

Kisiasa, mji huo mkuu wa Ujerumani ulikuwa umegawika tangu mwishoni mwa vita kuu ya pili ya dunia, lakini watu waliweza bado kutembea kwa uhuru, hadi Agosti 13, 1961.

https://p.dw.com/p/3yvW7
Deutschland Geschichte Berlin Mauer DDR Mauerbau Grenztruppen
Picha: ullstein bild - Georgi(L)

"Lango kuu la Brandenburg lafungwa" - kwa kichwa hiki cha habari shirika la habari la Marekani, Associated Press, liliutangazia ulimwengu juu ya tukio lenye umuhimu wa kihistoria katika majira ya asubuhi ya Agosti 13, 1961, juu ya ujenzi wa ukuta wa Berlin.

Katika siku hii, kiashiria muhimu cha mji huo, kilichoko katika mpaka kati ya Mashariki na Magharibi kimefungwa. Wakati huo huo, wanajeshi wa jeshi la taifa la watu NVA na makandarasi wa ujenzi kutoka serikali ya Kikomunisti ya Ujerumani Mashariki, GDR, walifunga njia zote nyingine za kuelekea Berlin Magharibi - awali kwa kutumia uzio.

Kile kilichofahamika kama "operesheni ya usalama wa mpakani" iliyoongozwa na aliekuja kuwa mkuu wa serikali Eric Honecker ndiyo lilikuwa jengo la mwisho kukamilisha mgawanyo wa Berlin kwa maana halisi ya neno hilo. Muda mchache baadae, kazi ilianza ya kujenga ukuta wa mawe na zege wenye urefu wa mita 3.6 kwenda juu kwenye mpaka wa Berlin Magharibi.

Zentrale Gedenkveranstaltung zum 60. Jahrestag des Mauerbaus | Bundespräsident Steinmeier
Rais wa Shirikisho la Ujerumani Frank-Walter Steinmeier akizungumza katika kumbukumbu ya miaka 60 tangu kuanza ujenzi wa ukuta wa Berlin.Picha: Frederic Kern/Geisler-Fotopress/picture alliance

Hii ingeziba mwanya wa mwisho na mkubwa zaidi ambamo idadi kubwa ya wakimbizi wapatao milioni 2.6 walipitia kuitoroka GDR tangu kugawanywa kwa Ujerumani mwaka 1949. Katika Jamhuri ya Shirikisho la Ujerumani FRG, walikuwa na matumaini ya maisha bora, kifedha, kitamaduni na hata kisiasa.

Soma pia: Mamilioni ya Wajerumani Mashariki wahamia Magharibi

Vita baridi kati ya Mashariki na Magharibi

Uhamaji huo wa watu wengi uliipeleka Ujerumani Mashariki kwenye kingo za kusambaratika kiuchumi. Juu ya yote, kulikuwa na uhaba wa wafanyakazi wenye ujuzi uliohitajika haraka pamoja na madaktari. Ili kuzuwia kuendelea kwa hali hiyo, watawala Berlin Mashariki waliona njia moja pekee: Ukuta wa Berlin.

Katika propaganda rasmi hata hivyo, ufungaji wa mpaka ulihalalishwa kwa njia tofauti kabisaa: Kwamba kutunzwa kwa amani kunahitaji kuzuwia shughuli za walipizaji kisasi wa Ujerumani Magharibi.

Matamshi hayo ya ushari, mashuhuri hasa katika wakati ambapo dola la kikomunisti lenye nguvu zaidi, la Umoja wa Kisovieti na hasimu wake wa kibepari Marekani, yalikuwa yanashindana kuhusu ruwaza bora ya kijamii. GDR ilikuwa upande na chini ya ushawishi wa Umoja wa Kisovieti huku FRG ikiwa kambi ya Marekani.

Hatari ya vita kuu ya tatu na ya nyuklia ya dunia ilikuwa halisi. Pande zote zilikuwa zinajihami kijeshi, na kulikuwepo na mazungumzo juu ya urari wa vitisho. Zama hii, ambayo ilimalizika tu na kuanguka kwa ukuta wa Berlin mwaka 1989, iliingia katika historia kama Vita Baridi.

Mauertod von Peter Fechter
Moja wa watu aliepigwa risasi na askari polisi wa Ujerumani Mashariki wakati akijaribu kuruka ukuta huo kuelekea upande wa magharibi.Picha: dpa/picture-alliance

Berlin Magharibi: "Kisiwa cha uhuru katika bahari ya Ukomunisiti"

Katika muda wa miongo kadhaa, mji uliogawika wa Berlin ulikuwa kitovu cha mapambano ya mifumo. Nembo ya kisiasa ya utawala wa Wanazi kuanzia 1935 hadi 1945 iligawanywa katika sekta nne na mataifa washindi wa vita kuu ya pili ya dunia: Wasovieti walikuwa na usemi katika sehemu ya mashariki, katika sehemu ya Magharibi walikuwepo Wamarekani, Waingereza na Wafaransa. Majaribio yote ya Wakomunisti kuiweka Berlin nzima chini ya ushawishi wao yalishindwa kutokana na upinzani wa washika wa Kimagharibi.

Soma pia: Marienborn: Kumbukumbu ya historia ya Ujerumani iliyogawika

Rais wa Marekani wa wakati huo John F. Kennedy, aliitaja Berlin Magharibi ya kidemokrasia kuwa "kisiwa cha uhuru ndani ya Bahari ya Kikomunisti." Lakini alilaazimika kukubaliana na ukweli juu ya ujenzi wa ukuta wa Berlin, kama ilivyokuwa kwa wakaazi zaidi ya milioni tatu wa pande zote mbili walioathirika na "ukuta wa ulinzi dhidi ya mabeberu," kama utawala wa DDR ulivyokuwa ukiutaja rasmi ukuta huo wenye urefu wa takribani kilomita 155.

Eneo la kuogofya na kumbukumbu: Mtaa wa Bernauer

Katika miaka 28 ya uwepo wake, watu wasiopungua 140 walikufa kwenye ukuta wa Berlin. Hatma yao inakumbukwa hii leo katika kituo kikuu cha kumbukumbu kilichoko mtaa wa Bernauer, ambako kuna mita 200 zilizosalia kwenye ukuta huo.

Bau der Berliner Mauer | Bernauer Straße
Ujenzi wa ukuta ukiendelea katika eneo la mtaa wa Bernauer mjini Berlin, Agosti 1961.Picha: dpa/picture alliance

Wageni kutoka maeneo mbalimbali duniani huja hapa kuchora taswira hasa ya nini mgawanyo huo ulimaanisha. Mashuhuda wa zama hizo wanasimulia uzoefu wao.

Miongoni mwao ni simulizi za kijasiri kama za Joachim Rudolph, ambaye baada ya kutoroka alichimba handaki yenye urefu wa mita karibu 140 kutoka Magharibi kwenda Mashariki, ili kuwasafishia wengine njia ya uhuru chini ya ardhi. Miaka 60 baada ya ukuta kujengwa Agosti 13, 1961, Joachim Rudolph ni mtu anaeuliziwa kwa namna ya kipekee.

Soma pia: Kipi kilivisibu vilabu vya Ujerumani Mashariki?

Katika mjadala ulioandaliwa na wakfu wa shirikio unaotathmini utawala wa kidikteta wa SED, msaidizi huyo wa zamani watoro wa utawala huo, anasimulia pia uzoefu wake katika mtaa wa Bernauer wakati alipokuwa akikagua eneo hilo muda mfupi baad ya mpaka kufungwa. "Tuliona uzio wa senyenge ukikatiza kwenye mtaa wa Bernauer. Mbele yake walisimama wlainzi watano au sita wakiwa na bunduki aina ya Kalashanikov shingoni mwao na kofia ya chuma kichwani."

Njia ya Ukuta: "Kwanini ipo?"

 Kisha ghafla wakasikia sauti kali ya kutisha. Nini kingewasibu, iwapo wasingeweza kusoma? Hapa ni eneo la mpaka! Hakuna kupita bila ruhusa! Katika wakati huo Joachim Rudolph anajua kilichojiri - kwa sababu walinzi wa mpakani hawaachi shaka yoyote juu ya hilo. Iwapo yeye na rafiki hawangegeuka mara moja na kuondoka katika eneo hilo, wangelaazimika kutumia silaha zao.

Gedenkstätte Berliner Mauer | Maueropfer
Picha za baadhi ya wahanga wa ukuta wa Berlin.Picha: Ingo Schulz/imageBROKER/picture alliance

Mashuhuda wa nyakati hizi na vituo vya kumbukumbu kama mtaa wa Bernauer ni nukta za mawasiliano, hasa kwa vijana wanapotaka kujifunza kuhusu historia ya ukuta wa Berlin. Lennart Siebels, mzaliwa wa mwaka 1995, alikuwa na faida ya kieneo, kwa sababu mwanaume huyo mdogo anaesomea uhandisi wa michezo katika chuo kikuu cha Chemnitz (Saxony), alikulia pembezoni mwa Berlin kwenye alama ya ukuta iliyopo sasa.

Soma pia: STASI-Idara ya usalama ya iliokuwa Ujerumani Mashariki

"Kwa kuishi karibu sana na msitu na kuwepo huko njia hii na ukanda huu wa mchanga karibu yake, unajiuliza mapema: kwanini ipo huko?" Hivyo ndivyo maswali yalivyoibuka mapema utotoni, anasema akikumbuka. "Nadhani hii ilichochea shauku mapema zaidi kuliko wakati unapoishi mjini."

Masalia ya ukuta: Fikira juu ya Ujerumani- na ulimwengu

Ilikuwa simulizi tofauti kabisaa kwa Lena Quincke mwenye umri wa miaka 22, aliezaliwa Cameroon na kukulia Ehtiopia. Aliwasili Ujerumeni ambako anasomea sheria mjini Halle (Saxony-Anhalt), mwaka 2017. Kwa sababu alihudhuria shule ya Kijerumani Afrika, alisoma kwa kufuata mtaala wa Ujerumani. 

Ukuta wa Berlin ilikuwa mada pia. Ulinganishaji na kuta na uimarishaji wa mipaka katika mataifa mengine? Hakuna! Ni Ujerumani tu iliyokuwa inajadiliwa. "Na kila kitu kilichokuja kabla na baada: Vita kuu ya kwanza ya Dunia, Vita kuu ya pili ya Dunia, Ukuta na Vita Baridi.

Lena Quincke - 22 jährige Studentin
Lena Quincke, mwanfunzi mwenye umri wa miaka 22 aliezaliwa Cameroon na kukulia Ethiopia, alihamia Ujerumani 2017.Picha: Privat

Kwa kuwa Lena Quicke amekuwa akiishi Ujerumani, taswira yake ya mji wa Berlin uliokuwa umegawika zamani imekuwa ya mitazamo tofauti: "Unapoona mabaki hayo ya ukuta na kujua kwamba kuliwahi kuwa na ukuta hapa na kwamba watu walikuwa hawawezi kuvuka kwa urahisi, hii inaamsha hisia ndani yako," anasema binti huyo wa baba wa Kijerumani.

Soma pia: Ni miaka 50 tangu kujengwa ukuta wa Berlin

Ghafla, maswali mapya yanaibuka kuhusu mgawanyiko wa nchi: Ikiwa wakati wote ulijiona kama Mjerumani, ghafla unafikiria juu ya "Ujerumani ipi ulikuwa."

Kuta mpya na nyuzio za mipakani katika karne ya 21

Licha ya historia zao tofauti, Lena Quicke na Lennart Siebels wameshughulikia suala la ukuta wa Berlin kwa njia inayofanana: shuleni, katika familia. Na juu ya yote katika eneo la tukio hilo la kihistoria - Lena kama mwanamke kijana, na Lennart kama mtoto. "Kila nilipokuwa na swali, nilikuwa nawauliza wazazi wangu," anasema Lennart. Au alikuwa anatafuta mahala, na mada hiyo ilifundishwa shuleni. Hali ilikuwa hivyo kwa Lena.

Soma pia: Viongozi wa kimataifa wakusanyika mjini Berlin

Na kuna jambo jengine la kufanana kwa watu hao wawili - Moja ambalo ni mashuhuri kwa kizazi chao: Wanaposikia neno "Ukuta," hawafikirii tu juu ya ule uliokuwepo Berlin kuanzia 1961 hadi 1989. Lennart anasema haufikirii mara moja wakati wote. Ukuta wa mpakani uliopangwa kujengwa na rais wa zamani wa Marekani Donald Trump kati ya Marekani na Mexico pia unakuja akilini. Siyo Ukuta wa Berlin, "kwa sababu sikuuona hata katika maisha yangu. Na ndiyo haupo kwake kama wengine.

Lennart Siebels wuchs am nördlichen Berliner Stadtrand auf
Lennart Siebels alikulia kaskazini mwa Berlin, mita chache kutoka ulikopita ukuta wa Berlin.Picha: Privat

"Inaishia kuwa hatari kwa wengi"

Lena anaona ulinganifu kati ya kuta za zamani na mpya. Juu ya yote, anasema hatari zinafanana. Palipo na ukuta mara zote kuna kasoro za namna fulani. Na mara zote watu hutafuta namna ya kutumia kasoro hizo kwa manufaa yao.

"Na hilo linaishia kuwa maafa au hatari kwa wengi." Mfano mmoja unaokuja akilini kwake ni mpaka kati ya Israel na maeneo ya Wapalestina, hasa ukuta wa Jerusalem. Huko, anasema, unaweza kuona athari yake kwa wakazi, hasa raia wa kawaida.

Haijalishi ukuta gani unazungumziwa duniani, Lena anaitikia kihisia juu yake. "Kwa vyovyote vile, kwangu ni hisia mbaya ninaposikia kuhusu ukuta mahala popote.

Makala hii imetafsiriwa kutoka Kijerumani