1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Miaka 60 tangu kuundwa kwa taifa la Israel

P.Philipp - (P.Martin)8 Mei 2008

Israel,katika historia yake ya miaka 60,haikuja kuwa nyumbani kwa maelfu ya watu walionusurika maafa ya Wayahudi,bali imekuwa nchi ya kisasa,kidemokrasi na iliyoendelea. Lakini,inagubikwa na mgogoro wa Mashariki ya Kati.

https://p.dw.com/p/Dwqm
Kijana mjini Tel Aviv akisherehekea miaka 60 tangu kuundwa kwa taifa la Israel.Picha: AP

Ni miaka 60 tangu kuundwa kwa taifa la Israel; Mara nyingine Waisraeli na Wapalestina huketi na hukumbuka jinsi yote yalivyoanza hapo mwaka 1948.Kwa mmoja,tena ni wakati mwingine wa kusherehekea nguvu zake-na kwa mwingine, ni wakati wa kuandamana na kuonyesha uchungu na huzuni wake.

Kwa hivyo fikra za Wayahudi zilizochomoza kuhusu matukio hayo zinastaajabisha.Kwani kile kilichoandikwa katika gazeti la Haaretz kuhusu sherehe za miaka 60 ya Israel,kisingedhaniwa kabisa hiyo miaka michache iliyopita yaani kuchapisha hivi: "Miaka sitini ya maafa - Miaka sitini ambayo haikuleta chochote."

Wapalestina ndio huieleza siku ya kuundwa taifa la Israel kama ni siku ya maafa.Bila shaka mhariri wa makala hayo hahisi kuwa kuanzishwa kwa taifa la Israel ni maafa,bali yale yaliyotokea baadae pamoja na yale ambayo hayakutokea - yaani hakuna amani iliyopatikana.

Wakati wa sherehe kubwa za mwisho za Israel hiyo miaka kumi iliyopita,watu walikuwa na matumaini kuwa Makubaliano ya Oslo huenda yakaleta amani ya aina fulani.Lakini makubaliano hayo hayakuleta cho chote.Na hakuna anaetaraji mafanikio katika jiuhudi mpya za Rais wa Marekani George W.Bush anaetaka makubaliano ya amani ya Mashariki ya Kati yatiwe saini kabla ya yeye kuondoka madarakani.Kama asilimia 80 ya Waisraeli hawaamini hilo na Wapalestina wengi zaidi ndio hawana matumani kabisa.

Mashaka kama hayo kwa sehemu kubwa hugubika historia ya mafanikio mbali mbali ya Israel.Hiyo haikujakuwa tu nchi kwa wale walionusurika maafa ya Wayahudi,bali imepiga hatua kuwa nchi ya kisasa na kidemokrasia licha ya mikasa ya siasa za kijamii;inaongoza katika sekta ya sayansi na tiba;ina uchumi unaostawi na jeshi linalozidi kuwa na nguvu.

Lakini hayo yote yanasaidia nini ikiwa hakuna amani ili kuweza kufaidi matunda ya mafanikio?Katika historia ya ya miaka 60 ya Israel,ipo mifano mingi ya nafasi zilizokosa kutumiwa kujipatia amani ya aina hiyo.Nafasi hizo hazikutumiwa vilivyo na pande zote mbili.Wapalestina -ikiwa ni pamoja na ulimwengu wa Kiarabu- wakizidi kuchukua wakati kuzingatia amani na wakipinga kuitambua Israel,basi serikali mbali mbali za Israel pia zimeona ni bora kutegemea nguvu zake za kijeshi badala ya diplomasia na kuwa tayari kuafikiana.

Israel,inakumbuka matamshi yaliyotolewa na Waarabu kufuatia vita vya siku sita:Yaani-hakuna majadiliano na Israel;hakuna kuitambua Israel na hakuna amani na Israel.Lakini hata orodha ya Waisraeli ni ndefu.Kwa muda mrefu Israel ilipinga kuwatambua Wapalestina kama ni watu wa kundi moja;baadae ikapinga fikra ya kuwepo taifa la Kipalestina.Sasa kwa Israel,miko mikubwa ni kurejea kwa wakimbizi wa Kipalestina na kuafikiana kuhusu jiji la Jerusalem.Hayo ni yalio muhimu tu miongoni mwa yale yanayopingwa na Israel.Tena,ni maafa kwa pande zote mbili.Bila ya kusita wanapeleka nyuma gurudumu la historia.