1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Oliver Kahn aiaga rasmi Bundesliga

Liongo, Aboubakary Jumaa19 Mei 2008

Ni jumatatu nyingine tunakutana katika ukurasa huu wa michezo,ambapo miongoni mwa habari tulizomudu kukusanyia, ni Bundesliga ligi ya Ujerumani yakamilika kwa kumuaga rasmi mlinda mlango mkongwe Oliver Kahn, huku FC Kolh

https://p.dw.com/p/E2Yt
FC Bayern Munich wakishangilia ushindi wa taji la Bundesliga msimu huuPicha: AP

Bundesliga mwishoni mwa wiki ilimalizika kwa Werder Bremen kukamata nafasi ya pili, Nurengburg kuungana na Duisburg pamoja na Hansa Rostok kushuka daraja, huku mabingwa Bayern Munich wakimpa mkono mzuri wa kwaheri nahodha na mlinda mlango wao Oliver Kahn kufuatia ushindi wao wa mabao 4-1 dhidi ya Hertha Berlin.


Bremen imekamata nafasi ya pili kufuatia ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Bayer Leverkusen, huku Schalker 04 ikipigilia msumari wa mwisho katika jeneza la Nurenburg kwa kuichapa mabao 2-0 na kukamata nafasi ya tatu na hivyo kuungana na Bremen pamoja na mabingwa Bayern Munich katika ligi ya mabingwa barani Ulaya.


Kwa Oliver Kahn hiyo ilikuwa mechi yake ya mwisho katika bundesliga baada ya kuwa dimbani kwa dakika 557.


Luka Toni jogoo wa kitaliano aliyejiunga na Bayern Munich msimu huu alihitimisha ubabe wake wa kupachika  mabao pale alipoweka wavuni mabao 3 na kumfanya kuwa mtia mabao bora wa bundesliga akiwa na mabao  24.


Kwa upande mwengine, Borussia Monchengladbach, FC Koln na Hoffenheim zilipanda daraja.Monchengladbach ilipanda mwaka mmoja baada ya kushuka, huku FC Koln baada ya kuhangaika misimu kadhaa.


Ilikuwa ni shamra shamra kwa wakaazi wa Koln pamoja Bonn kwa timu yao hiyo kupanda daraja na  wiki nzima hii mitaani ni oyee fc koln.


Kwengineko hapa Ulaya, nchini Italia  Inter Milan hapo jana ilifanikiwa kurejesha  taji lake la ligi ya seria A kufuatia ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Parma katika siku ya mwisho ya ligi ya nchi hiyo.


Nchini Ufaransa Olympic Lyon iliendeleza ubabe wake wa kutawala soka la nchi hiyo pale ilipotwaa kwa mara ya saba ubingwa wa ligi ya daraja la kwanza nchini humo.


Hata hivyo msimu huu haukuwa mteremko kwa Lyon kwani iliwalazimu kusubiri mpaka siku ya mwisho juzi Jumamosi kuweza kutetea taji lake kwa ushindi wa mabao  3-1 dhidi ya Auxerre.

---------

Kutoka hapa barani Ulaya na sasa tuelekee huko afrika mashariki, tukianzia nchini Tanzania ambako timu ya taifa ya kandanda ya nchi hiyo mwishoni mwa wiki ilifanikiwa kusonga mbele kuelekea fainali za afrika kwa wanasoka wasiyo wa kulipwa baada ya kutoka sare ya  1-1 na Uganda.Tanzania katika mechi ya kwanza iliifunga Uganda mabao 2-0, na sasa itakumbana na Sudan iliyoiondosha Rwanda.


Katika nchi jirani ya Kenya, kama anavyoarifu mwanamichezo wetu wa mjini Mombasa Eric Ponda ligi kuu ya kandanda ya nchi hiyo inakaribia ukiongoni,huku timu ya Mathare United ikiongoza.


Aidha timu ya taifa ya riadha ya nchi hiyo imeingia kambini hii leo kwa ajili ya mawindo ya michuano ya Olimpiki nchini China.


Na kwa kumazia turejee hapa Ulaya ambapo mji wa Moscow huko katika maandalizi makubwa ya fainali ya klabu bingwa barani Ulaya keshokutwa Jumatano kati Manchester United na Chelsea zote za Uingereza.


Hiyo itakuwa ni mara ya kwanza kwa jiji hilo la Moscwo kuwa mwenyeji wa fainali ya klabu bingwa, baada ya kuwa mwenyeji wa fainali ya UEFA miaka tisa iliyopita, pale Parma ya Italia ilipoifunga Olympique Marseille ya Ufaransa mabao 3-0.


Ni fainali inayoitwa ya kukata na shoka kama si kuvunja na nyundo, kila mtu akiisubiri kwa hamu kubwa, lakini kwa hapa KölnBonn, bado kupanda daraja kwa FC Köln kumegubika mioyo ya washabiki.


Hongera FC Köln Ni a.Liongo hadi wakati mwengine kwaheri kutoka Bonn