1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Misri: Hosni Mubarak aachiwa huru

Lilian Mtono
24 Machi 2017

Hosni Mubarak, rais wa zamani wa Misri aliyehudumu kwa muda mrefu zaidi na kupinduliwa mnamo mwaka 2011 katika mapinduzi ya umma, ameachiwa huru kutoka kizuizini baada ya miaka sita

https://p.dw.com/p/2ZuRd
Hosni Mubarak, Rais wa zamani wa Misri
Picha: picture-alliance/AP Photo/A. nabil

Mwanasheria wa Mubarak Farid al-Deeb ameliambia gazeti binafsi la al-Masry al-Youn kwamba Mubarak amerejea katika makazi yake yaliyoko katika kitongoji cha Heliopolis, Mashariki mwa mji wa Cairo baada ya kuachiwa kutoka hospitali ya kijeshi ambako alikuwa akizuiliwa. Kulingana na afisa usaalam wa Misri, Mubarak aliondoka kwenye hospitali ya kijeshi iliyopo Cairo mapema asubuhi ya leo. Alielekea nyumbani kwake akiwa chini ya ulinzi mkali. Mubarak alirejea nyumbani akiwa na watoto wake wawili, Alaa na Gamal, na baadae kuungana pamoja na familia yake nzima ikiwa ni pamoja na mkewe Suzanne. 

Mubarak alikamatwa mwezi Aprili, 2011, ikiwa ni miezi miwili baada ya kuondoka madarakani, na tangu hapo amekuwa akishikiliwa gerezani na hospitali hiyo ya kijeshi akiwa chini ya ulinzi mkali, kwa tuhuma za kuagiza mauaji ya waandamaji wakati wa uasi wa umma uliyosababisha kuangushwa kwake.

Wakati akishtakiwa kwa makosa hayo, tayari alikuwa ametumikia kifungo cha miaka mitatu kwa makosa ya matumizi mabaya ya fedha za serikali. Mnamo mwezi May mwaka 2015, mahakama ya uhalifu iliamua kumfunga kwa miaka miatu jela na kumpiga faini ya Mamilioni ya Pauni za Misri kufuatia kosa hilo la matumizi mabaya ya fedha zilizoainishwa kwa ajili ya ukarabati wa makazi ya rais. Mahakama nyingine ilithibitisha hukumu hiyo mwaka 2016.

Wananchi wa Misri wataka haki

Maelfu ya Wamisri waliandamana mwaka 2011 kumpinga Rais Mubarak
Maelfu ya Wamisri waliandamana mwaka 2011 kumpinga Rais MubarakPicha: ap

Mapema mwezi huu, mahakama ya juu ya rufaa ya nchini Misri ilitoa hukumu ya mwisho iliyofuta makosa ya Mubarak mwenye umri wa miaka 88 ya mauaji ya waandamanaji katika vuguvugu la mageuzi lililohitimisha utawala wake uliodumu kwa miaka 30. Mubaraka amekuwa kizuizini tangu mwaka 2011. Makundi mawili ya majeshi ya usalama yalisafisha njia kutoka hospitali hadi nyumbani kwake, amesema mmoja wa afisa wa usalama kwa sharti la kutotajwa jina kwa kuwa hakuwa na ruhusa ya kuzungumza na vyombo vya habari. Wanaharakati hata hivyo wanasema, kuachiwa kwa Mubarak kutokana na makosa ya mauaji ya waandamanaji kunathibitisha hisia zilizodumu kwa muda mrefu kwamba kesi yake pamoja na askari polisi wanaokabiliwa na mashtaka ya kesi hiyo hayataweza kuleta haki waliyoidai. 

Raia wengi wa Misri waliokuwepo wakati wa utawala wake walikichukulia kipindi hicho kama cha kilio, utawala wa mabavu na ubepari uliohusisha maafisa wa serikali kushirikiana kwa karibu na wafanyabiashara katika njia ya upendeleo. Waarabu walionesha kufurahishwa wakati picha zinazomuonyesha kamanda huyo wa zamani wa jeshi la anga zilipoonyeshwa moja kwa moja kwenye televisheni, akiwa amefungwa kitandani kwenye kizingo cha chumba cha mahakama.

Kuangushwa kwa Mubarak, mmoja wa msururu wa wanajeshi waliotawala Misri tangu kukomeshwa kwa utawala wa kifalme mnamo mwaka 1952 kulibeba matumaini uasi wa umma katika mataifa ya Kiarabu uliotikisa watawala wa kimabavu kuanzia Tunisia hadi Ghuba na kwa muda mfupi kuibua matumaini ya enzi mpya ya demokrasia na haki za kijamii.

Mwandishi: Lilian Mtono

Mhariri: Iddi Ssessanga