1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkutano mkuu wa Umoja wa Ulaya kuanza leo

8 Desemba 2011

Viongozi wa Ufaransa na Ujerumani wanatafuta uungwaji mkono miongoni mwa viongozi wenzao wa jumuiya ya ulaya ili kutatua mgogoro wa madeni unaokumba jumuiya hiyo. Viongozi hao wanakutana kwa siku mbili kuanzia leo.

https://p.dw.com/p/13Oel
Rais Sarkozy wa Ufaransa na Kansela Merkel wa Ujerumani
Rais Sarkozy wa Ufaransa na Kansela Merkel wa UjerumaniPicha: dapd

Kansela wa Ujerumani Bi Angela Merkel na rais wa Ufaransa Bw Nicolas Sarkozy wanaelekea mjini Marseille kukutana na viongozi wengine na serikali ya mrengo wa kati wa kulia wa chama cha European People's kabla ya kuelekea mjini Brussels kwa ajili ya mkutano huo wa kutatua mgogoro wa madeni unaolikumba bara la Ulaya.

Viongozi hao watajadili namna ya kupata uungwaji mkono katika mpango wao wa kushinikiza mataifa ya ulaya kukubali kutekeleza nidhamu ya matumizi, mpango huu unanuiwa kutoa hali ya wasiwasi katika soko la hisa kutokana na uwezekano wa kudorora kwa sarafi ya euro.

Waziri mkuu wa Uingereza, David Cameron
Waziri mkuu wa Uingereza, David CameronPicha: dapd

Awali waziri mkuu wa Uingereza David Cameron alisema kuwa uingereza inaathirika kiuchumi pamoja na mataifa mengine barani Ulaya.

Kansela wa Ujerumani Angela Merkel amesema wana nia ya uhakika ya kuiletea utulivu sarafu ya euro na kuimarisha ushindani katika kanda ya euro.

Awali Ufaransa na Ujerumani zilikubaliana juu ya mabadiliko kadhaa yenye lengo la kuinusuru sarafu ya euro na utekelezaji wa nidhamu ya matumizi miongoni mwa wanachama wa Kanda ya Sarafu ya Euro.

Mabadiliko hayo yanajumuisha vikwazo vya moja kwa moja kwa wanachama watakaokiuka kanuni. Kimsingi mkataba huo utaidhinishwa na nchi zote 27 za Umoja wa Ulaya lakini Sarkozy alisema saini za nchi 17 zinazotumia sarafu ya euro zitakubaliwa.

Benki kuu ya Ulaya baadaye itazungumzia kwa kina makubaliano ya mkutano huu wa EU katika mkutano wake wa mwezi. Tayari wachambuzi wa uchumi wanasema kuwa benki hiyo inaweza kutoka katika kuyumba ambapo sasa iko katika asilimia moja wakati inapotarajia kupanda kwa uchumi wa mataifa ya bara Ulaya.

Mwandishi: Amina Abubakar

Mhariri: Mohammed Khelef