1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mivutano yachomoza Mkutanoni

4 Desemba 2015

Mkutano wa kilele wa mameya na wabunge kuhusu hali ya hewa umefunguliwa mjini Paris na rais Francois Hollande pembezoni mwa mkutano wa mabadiliko ya tabia nchi mashuhuri kwa jina la COP21.

https://p.dw.com/p/1HHP7
Wanaharakati wamebeba bango linalotahadharisha dhidi ya madhara ya mabadiliko ya tabianchiPicha: Reuters/E. Gaillard

Mbali na rais Francois Hollande na meya wa jiji la Paris Anne Hidalgo,mkutano huo wa kilele kuhusu hali ya hewa unahudhuriwa pia na meya wa zamani wa jiji la New-York Michael Blomberg ambae pia ndie mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa anaeshughulikia masuala ya miji na mabadiliko ya tabianchi ,mcheza sinema wa kimarekani Robert Redford na gavana wa zamani wa jimbo la California Arnold Schwarzenegger.

Wawakilishi wa mataifa 195 katika mkutano wa mabadiliko ya tabianchi yanayojulikana kama COP21,wataendelea kwa upande wao na majadiliano yao makali hadi decemba 11 ijayo lengo likiwa ni kufikia makubaliano ya kupunguza hali ya ujoto katika sayari yetu.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki Moon,amerejea Paris akiwa na matumaini mema ya kufanikiwa mazungumzo hao anasema:"Nimepata moyo kwa kile nilichokiona na kukisikia katika ufunguzi wa CP21.Viongozi wa dunia wamefanya kile wanachopaswa kukifanya-yaani kuyapa msukumo majadiliano.Takriban nchi zote zimewasilisha mipango ya kimkakati inayojulikana kama INDC(au michango inayodhamiriwa kutekelezwa kitaifa). Mataifa mengi tajiri yametoa ahadi thabiti za kupunguza moshi wa sumu na nchi nchi zilizoendelea zimetoa ahadi ziada kuzisaidia nchi maskini na zile, zinazoweza kuathirika,kukabiliana na madhara ya mabadiliko ya tabia nchi."

Mivutano imeanza kuchomoza kati ya nchji za kaskazini na zile za kusini

Hata hivyo dalili za mivutano zimeanza kuchomoza; nchi zinazoinukia zinaonyesha kukasirishwa na mkondo wa mazungumzo.Nchi hizo zimeyalaumu mataifa tajiri kupuuza "hofu za nchi masikii zaidi na zinazoweza kuathirika zaidi.

Frankreich Cop21 Klimagipfel in Paris - Laurent Fabius
Mwenyekiti wa Mkutano wa Mabadiliko ya Tabianchi,Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Ufaransa,Laurent FabiusPicha: picture-alliance/Pacific Press via ZUMA Wire/J. Raa

"Risala tunayopokea kutoka mataifa tajiri linapohusika suala la msaada wa fedha ili kujiambatanisha na mabadiliko ya tabianchi ni "kwamba hamna kitu" amesema mjumbe wa Bolivia Juan Hoffaister kwa niaba ya kundi la mataifa 77 pamoja na China.

Mataifa yanayoinukia yanataka fedha bilioni 100 zilizoahidiwa hadi ifikapo mwaka 2020 na mataifa ya kaskazini,zisisalie ahadi tupu na zizidishwe pia baada ya muda huo na kwamba sehemu kubwa ya fedha hizo zitumike katika kugharimia madhara ya mabadiliko ya tabia nchi.

Katika wakati ambapo wajumbe mkutanoni wanabidi wamkabidhi mwenyekiti wa COP21,Laurent Fabius,mapendekezo yao hadi disemba tano mchana,mjumbe wa Norway Aslak Brun ameukosoa ukosefu wa nia ya kuijongeza misimamo ya kila upande.

Kwa vyovyote vile iwavyo, nitakabidhiwa mapendekezo yote saa sita mchana."Amesema waziri wa mambo ya nchi za nje wa Ufaransa,ambae ndie mwenyekiti wa mkutano wa mabadiliko ya tabianchi COP21.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/AFP

Mhariri:Josephat Charo