1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkutano wa viongozi wa Umoja wa Ulaya

S.Henn - (P.Martin)11 Desemba 2008

Viongozi wa nchi 27 wanachama wa Umoja wa Ulaya wanakutana kwa majadiliano ya siku mbili mjini Brussels Ubeligiji chini ya uenyekiti wa Rais wa Ufaransa Nikolas Sarkozy.

https://p.dw.com/p/GDW0
French President Nicolas Sarkozy gestures as he speaks during a ceremony marking the 60th anniversary of the the Universal Declaration of Human Rights at the Elysee Palace in Paris, Monday, Dec. 8, 2008. (AP Photo/Michel Euler)
Rais wa Ufaransa Nicolas Sarkozy.Picha: AP

Huu ni mkutano wa kilele wa mwisho kufanywa chini ya uongozi wa Ufaransa,iliyoshika wadhifa wa urais unaozunguka katika Umoja wa Ulaya.Kuanzia Januari mosi 2009 Jamhuri ya Czech itapokea wadhifa huo.Ni dhahiri kuwa majadiliano mjini Brussels yatakuwa marefu na magumu.

Rais Nikolas Sarkozy anataka kuhitimisha kipinidi chake kama rais wa Baraza la Umoja wa Ulaya kwa kupata makubaliano katika masuala matatu muhimu :uchumi,ulinzi wa mazingira na mageuzi ya katiba.Kwa maoni ya Rais wa Halmashauri ya Umoja wa Ulaya José Manuel Barroso yawezekana kuwa huu ni mkutano muhimu kabisa kupata kufanywa katika miaka ya hivi karibuni na kuongezea:

"Kwangu binafsi huu ni mkutano muhimu kabisa ninaohudhuria kama rais wa Kamisheni ya Umoja wa Ulaya.Utakuwa mtihani mkubwa kwa Ulaya."

Lakini suala ni kwa umbali gani maslahi ya kitaifa yataweza kwenda sambamba na changamoto za Ulaya na ulimwengu kwa jumla.Licha ya hali mbaya ya uchumi,nchi za Ulaya zimeshikamana kuikabili mizozo ya uchumi na fedha.Mpango wa Euro bilioni 200 uliopendekezwa na Halmashauri ya Umoja wa Ulaya katika jitahada ya kufufua uchumi,ni miongoni mwa mada zitakazojadiliwa.Miradi ya kusaidia uchumi wa taifa iliyopitishwa na baadhi ya serikali itazingatiwa pia.

Ujerumani imeidhinisha msaada wa Euro bilioni 32,Ufaransa bilioni 26.Lakini Kansela wa Ujerumani Angela Merkel anasita linapozuka suala la kutoa mchango zaidi katika Umoja wa Ulaya.Licha ya kushinikizwa na Brussels,London na Paris,Merkel anasema,ikiwa Ujerumani itasaidia zaidi basi hiyo haitokuwa kabla ya mwaka 2009.Lakini viongozi hao wanakubaliana katika masuala ya kimsingi amesema Rais Nicolas Sarkozy.

Bila shaka Merkel na Sarkozy watakuwa na kazi ngumu wakati wa kujadili malengo ya Umoja wa Ulaya kupambana na mabadiliko ya hewa duniani. Malengo hayo yalijadiliwa Machi mwaka 2007 chini ya uongozi wa Ujerumani wakati ambapo ilishika wadhifa wa urais wa Baraza la Ulaya. Sasa malengo hayo ndio yanahitaji kuidhinishwa na kutiwa saini.Kuambatana na makubaliano hayo,uzalishaji wa gesi zinazochafua mazingira unapaswa kupunguzwa kwa asilimia 20 ifikapo mwaka 2020 na matumizi ya nishati pia yapunguzwe kwa asilimia 20.Bila shaka kutakuwepo majadiliano makali mpaka usiku wa manane.Kwa mfano Poland kwa inangángánia kuwekewa masharti tofauti kwa sababu asilimia 95 ya nishati yake inatoka kwenye mitambo inayotumia makaa ya mawe ambayo huchafua sana mazingira.

Tatizo jingine linalowangojea viongozi mkutanoni Brussels linahusika na katiba mpya ya Umoja wa Ulaya inayojulikana kama Mktaba wa Lisbon.Miongoni mwa mageuzi yanayotazamiwa kufanywa ni kupunguza idadi ya wawakilishi katika halmashauri ya umoja huo.iLakini Ireland inataka kuwa na mwakilishi wa kudumu mjini Brussels.Itakuwa shida iwapo kila nchi itashikilia kubakisha wawakilishi wake.

Hata hivyo Rais Sarkozy angependa kupata makubaliano katika masuala yote matatu,ikisemekana kuwa kiongozi huyo huenda hata akaurefusha mkutano hadi Jumamosi.